JK KATIKA MSIBA WA MBUNGE WA CHADEMA MAREHEMU REGIA MTEMA , TABATA

Rais Jakaya Kikwete akijiunga na waombolezaji katika msiba wa Mbunge wa Viti Maalumu (CHADEMA) Mh Regia Mtema leo January 15, 2012 nyumbani kwa marehemu Tabata jijini Dar es salaam ambako Waziri Mkuu Mh Mizengo Pinda, Spika Anne Makinda na Mwenyekiti wa CHADEMA Mh Freeman Mbowe walikuwapo.
PICHA NA IKULU
Rais Jakaya Kikwete akiwafariji wafiwa katika msiba wa Mbunge wa CHADEMA Mh. Regia Mtema leo.
Rais Jakaya Kikwete akizungumza na Mwenyekiti wa Chama Cha CHADEMA Mh Freeman Mbowe wa tatu kutoka kulia pamoja na jamaa wa Marehemu Regia Mtema.
Rais Jakaya Kikwete akiteta jambo na Waziri Mkuu Mizengo Pinda katikati pamoja na Spika wa Bunge Mh. Anne Makinda.
HABARI KAMILI
RAIS Jakaya Kikwete jana alikuwa miongoni mwa mamia ya watu wa kada mbalimbali waliokwenda Tabata, Chang’ombe, Dar es Salaam kuifariji familia ya marehemu Regia Mtema aliyefariki juzi katika ajali ya gari eneo la Ruvu, Pwani.  Mbali na Rais Kikwete, wengine waliofika msibani hapo kutoa pole ni Spika wa Bunge, Anne Makinda; Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na mkewe Tunu na Mwenyekiti wa Chadema na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.

Marehemu Mtema ambaye alikuwa Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), alifariki juzi wakati akitokea Dar es Salaam kuelekea mkoani Morogoro.  Jana katika msiba huo, msemaji wa familia, Canutte Mtema alisema ibada ya kuuaga mwili wa marehemu itafanyika leo katika Kanisa Katoliki Parokia ya Segerea kuanzia saa 9:00 alasiri.

 Alisema kesho, mwili wa marehemu Mtema utaagwa katika Viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam kisha kusafirishwa kuelekea Ifakara, ambako atazikwa Jumatano.  Mbali ya viongozi, viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa wakiwemo wabunge walifika msibani hapo kuwapa mkono wa pole kwa wafiwa wakiwemo Baba wa marehemu, Estelatus Mtema na mama yake, Catherine Kilaule.

  Rais Kikwete atoa neno  Akitoa pole kwa wafiwa, Rais Kikwete alisema Marehemu Mtema amefariki akiwa bado kijana mdogo na aliitaka familia kuwa na uvumilivu kwani kila mtu ana siku na mkataba wake na Mungu. Marehemu Mtema amefariki akiwa na umri wa miaka 32.  “Poleni sana, tupo pamoja katika msiba. Nasi tutaangalia eneo gani tutaweza kuwa pamoja,” alisema Rais Kikwete.

Spika na wabunge  Kwa upande wake, Spika Makinda alisema Bunge limepoteza mbunge kijana ambaye alikuwa na hulka kipekee. Alisema marehemu alikuwa na uwezo mkubwa wa kujenga hoja licha ya ugeni wa kazi bungeni.  Kutokana na msiba huo, Spika Makinda alisema Kamati ya Uongozi ya Bunge itakaa na kupanga taratibu za jinsi ya kushiriki msiba huo ikiwa ni pamoja na kuchagua wawakilishi wa Bunge watakaokwenda katika mazishi.

 “Tunasikitika kuondokewa na mbunge kijana Regia, alikuwa mchapakazi hodari na alikuwa na marafiki wengi bila kujali itikadi za vyama na kikubwa zaidi, alikuwa anakubali kukosolewa,” alisema Spika.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alisema chama na Bunge kwa ujumla vimepata pigo kubwa kwa kuondokewa na marehemu Mtema. Alisema kutokana na uzito wa msiba huo, wabunge wote wa Chadema watashiriki mazishi yake huko Ifakara. Mnyika alisema wabunge wa chama hicho wameshaanza kuwasili kwa ajili ya msiba huo.

Aliyejeruhiwa asimulia
Mmoja wa majeruhi saba, Rogers Abdallah alisema ingawa ameruhusiwa, bado ana maumivu makali kifuani na kitu kibaya zaidi  hakupata kipimo cha X-Ray... “Nimeruhusiwa lakini sikufanyiwa X-Ray,  nina maumivu kifuani na ninashukuru nimetoka mzima nafikiri mkanda niliokuwa nimefunga umenisaidia,” alisema.  Kati ya majeruhi hao, sita wameruhusiwa kutoka hospitalini isipokuwa mama mdogo wa marehemu, Bernadeta Mtema ambaye bado yupo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

Kilombero kwazizima
Wakazi wa Wilaya ya Kilombero humo wamezipokea kwa masikitiko na majonzi makubwa taarifa za kifo cha mbunge huyo.  Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda, Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Francis Miti, Mbunge wa Jimbo la Kilombero Abdu Mteketa, Mwenyekiti wa Halmashauri Ramadhani Kiombile, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kilombero, Abdallah Kambangwa na viongozi mbalimbali walifika nyumbani kwa marehemu kwa maandalizi ya mazishi.

Wakati hali ikiwa hivyo nyumbani kwake, ofisini kwa mbunge huyo nako kulikuwa na shughuli mbalimbali za maandalizi ya mazishi na viongozi wa Chadema na wanachama wa chama hicho, walikusanyika ili kuunda kamati maalumu itakayoshughulikia mazishi hayo.

 Akizungumzia msiba huo, Dk Mponda alisema: “Namfahamu vizuri marehemu ukizingatia sisi wabunge wa wilaya hizi mbili za Kilombero na Ulanga tupo karibu sana katika ushirikiano bila kujali itikadi zetu na marehemu alikuwa makini katika kutetea wananchi punde anaposikia matatizo,” alisema Dk Mponda.

Kwa upande wake, Mteketa alisema: “Unajua nilikuwa nashirikiana naye vizuri sana tofauti na baadhi ya wananchi walivyokuwa wanadhani kutokana na sisi kuwa vyama viwili tofauti na ndiye aliyekuwa akinipa changamoto zaidi ili niweze kutekeleza ahadi zangu kwa wakati kwa wananchi walionichagua.”

 Naye Kiombile alisema msiba wa Regia ni pengo kubwa ndani ya wilaya ya Kilombero hasa ikizingatiwa kwamba alikuwa mbunge kijana kama alivyo yeye na mara kwa mara alikuwa akimpigia simu ili kumpa ushauri naye kupokea ushauri kutoka kwake.  Kambangwa alisema mbunge huyo alikuwa mwanasiasa kijana aliyekuwa akijali zaidi maslahi ya wananchi aliokuwa akiwaongoza na hakufuata itikadi za chama chake pekee.

Rafiki wa karibu wa marehemu Regia, Amina Simbamkuti alisema amempoteza mtu wa karibu aliyeshirikiana naye katika kutatua kero mbalimbali za wananchi.  Mbunge huyo alifariki dunia baada ya gari alilokuwa akiendesha kupinduka saa 5:30 asubuhi karibu na Shule ya Sekondari Ruvu. 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA