Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI
ya Msama Promotions, imemkamata mmoja wa watuhumiwa wa mtandao wa
kundi la wanyonyaji wa kazi za wasanii wa muziki wa injili, Seleman
Mtupwa.
Mtuhumiwa huyo aliyekamatwa juzi kwa kurudufu kanda ambaye ni mkazi wa Dar es Salaam, alipelekwa Kituo cha Polisi Magomeni.
Kukamatwa
kwa Mtupwa kumetokea baada ya kiongozi wao, Francis Kamalamu,
aliyekuwa akifanya biashara hiyo katika eneo la Ubungo Maziwa, Dar es
Salaam, naye kutiwa mbaroni, akiwamo Mwakwi Yahya.
Baadhi
ya wanyonyaji waliokwishakamatwa ni Fred Jumbe, Martin Mkinga,
Abdallah Kijemi, Abdallah Salum, Yahya Salum, Lazaro John, Amir Kassim,
Faraj Amir, Rashid Juma na Mustafa Rashid.
Harakati
za kuwakamata wanyonyaji hao zilianza mwishoni mwa mwaka jana, ambapo
maofisa usambazaji wa Kampuni ya Msama Promotions, walianza harakati
za kuwasaka wanyonyaji hao na kufanikiwa kuwanasa vijana kadhaa
wakiziuza CD za muziki wa Injili.
Wanapozikuta, maofisa hao wamekuwa wakiweka mtego kwa kujifanya ni wateja wa CD hizo kisha wanawakamata wahusika.
Imeelezwa
kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa akiiuza CD moja kwa sh. 1,700, na
alikamatwa na mali zenye thamani ya zaidi ya sh. milioni 1.2 huku
wenzake wakikimbia.
Mkurugenzi
wa Msama Promotions, Alex Msama alisema mtuhumiwa huyo alikuwa
akijikusanyia zaidi ya sh. milioni 2.1 kutokana na kurudufu kanda hizo.
Mtuhumiwa
bado anaendelea kushikiliwa kwenye Kituo cha Polisi Magomeni, Dar es
Salaam, na Kamanda wa Polisi Mkoa wa kipolisi Kinondoni, ACP Charles
Kenyela, alisema uchunguzi zaidi unaendelea.
Msama
alisema vijana wake wa kikosi kazi wanaendelea na msako dhidi ya
maharamia hao Dar es Salaam na hivi karibuni watahamia mikoani.
Comments