Mwanamuziki mashuhuri
nchini Senegal na mwanaharakati wa kisiasa,Youssou N'dour, ametangaza kuwa
atawania kiti cha urais katika uchaguzi wa mwezi Februari nchini humo.
Mwanamuziki huyo
amesema kuwa anaitikia wito wa kumtaka agombee kiti hicho dhidi ya rais wa sasa
Abdoulaye Wade, ambaye anapania kuwania kiti hicho kwa muhula wa tatu.
Youssou N'dour
amehusika na maswala ya kibinadamu kwa siku nyingi na pia ni balozi wa shirika
la umoja wa matataifa kuhusu maswala ya watoto (UNICEF).
Mwandishi wa BBC mjini
Dakar, Thomas Fessy, anasema hatua ya bwana Youssou N'dour kutangaza kuwa
atawania kiti cha urais, haijawashangaza wengi. Hii ni kufuatia tangazo
alilotoa mwisho wa mwaka uliopita kuwa atajitosa katika ulingo wa kisiasa.
Katika hotuba
iliyopeperushwa kupitia kituo chake cha redio na televisheni, mwanamuziki huyo
amesema atapunguza matuzi ya serikali na kuahidi kuzalisha chakula na umeme kwa
wote iwapo atachaguliwa kuwa rais wa Senegal.
''kuwa rais ni kazi sio taaluma''
Youssou N'dour
anakubali kuwa yeye sio msomi lakini anaelezea wadhifa wa rais kama ''kazi na
sio taaluma''.
Youssou N'dour alikuwa
rafiki wa karibu wa rais Abdoulaye Wade, lakini baada ya Wade kutangaza nia ya
kuwania kiti cha urais kwa muhula wa tatu, aligeuka na kuwa mpinzani wake mkuu.
Lakini haitakuwa kazi
rahisi kwa Bw. Youssou Ndour kuwabadili maelfu ya wafuasi wake wa muziki
kumpigia kura.
Aidha, Youssou N'dour
amewahi kuwashutumu viongozi wa nchi za Afrika kuhusu jinsi walivyoshughulikia
janga la njaa nchini Somalia.
Comments