WAGONJWA WENGI WANAKUFA MUHIMBILI

BAADHI ya wagonjwa na madaktari katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), wamesimulia adha wanazopata kutokana na kufukuzwa kwa madaktari wanafunzi waliokuwa wamegoma na wameiomba Serikali ifanye kila linalowesekana kunusuru hali hiyo.

Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti jana, walisema mgomo huo umefanya hali katika hospitali hiyo  kuwa mbaya, kiasi cha baadhi ya wagonjwa kupoteza maisha kwa kukosa huduma.

Mmoja wa wagonjwa hao Godliver Alfonsi aliyetokea mkoani Kigoma alisema ana wiki moja tangu afike hospitalini hapo lakini hajaweza kuonana na daktari.

"Tangu nije leo (jana) tu ndio nawaona madaktari wakipita, lakini kwangu hawakupita kwa kuwa muda ni mdogo na wameniahidi kuwa watakuja kwangu kesho (leo)," alisema.

Mama wa mtoto Fatma Iddi katika wodi ya jengo la watoto, Hidaya Idrisa alisema madaktari hawaonekani wodini hapo kama ilivyokuwa awali.

Alisema kabla ya mgomo madaktari walikuwa wakikaa katika moja ya vyumba vya wodi hiyo, hivyo ilikuwa rahisi kuwapata kunapotokea tatizo.

“Madaktari hapa walikuwa hawaondoki kila wakati wapo na wakati wowote ukiwa na shida unapata msaada lakini hivi sasa chumba chao kitupu, hawapo” alisema Hidaya.

Hali katika wodi ya Kibasila pia ni mbaya na muuguzi wa zamu katika moja ya wodi za jengo hilo alisema; "Inawachukua muda wagonjwa kuonana na daktari kutokana na uchache wa madaktari."

“Mfano daktari ambaye yupo sasa aliingia kazini jana (juzi) mpaka sasa ninavyoongea hajaondoka maana yuko peke yake,” alisema muuguzi huyo.

Mgonjwa mwingine hospitalini hapo ambaye hakutaka kutajwa gazetini alisema: “Tangu asubuhi sijaonana na daktari sasa ni mchana (saa 12.30) na sina tumaini la kupata huduma”.

“Kama ningekuwa mahututi pengine hata wewe mwandishi usingenikuta, tungekuwa tunaongea mengine hapa,” alisema mgonjwa huyo.

Mmoja kati ya wanafunzi (jina limehifadhiwa), ambaye yupo katika mafunzo kwa vitendo tatu mwezi Desemba mwaka jana hosipitalini hapo, anasema hali si nzuri na kwamba ikiendelea hivyo huenda idadi ya vifo ikaongezeka.

“Idadi ya vifo vya sasa huwezi kuvihusisha na mgomo moja kwa moja lakini sina shaka kabisa kuwa vipo ambavyo vinachangiwa na hali hii,”alisema daktari huyo mwanafunzi.

Alisema kwa sasa madaktari bingwa hawana wasaidizi hali ambayo inawafanya wafanye kazi muda mrefu na kushindwa kuwafikia baadhi ya wagonjwa.

“Madaktari wanachoka, hata sisi wachache ambao tunasaidiana nao tunakuwa katika wakati mgumu” alisema na kuongeza kuwa hali hiyo inawafanya wawazungukie wagonjwa hadi saa nane mchana badala ya muda wa kawaida wa saa mbili asubuhi.

Madaktari
Katibu wa Chama cha Madakitari Tanzania (MAT) Dk. Rodrick Kabangila alisema tabia ya Serikali kuingiza siasa katika taaluma inaathiri huduma kwa umma.

Alisema kila jambo hivi sasa linachukuliwa kisiasa kwa kupiga porojo badala ya utekelezaji na kwamba sasa siasa zimeingia katika taaluma ya udaktari na uuguzi.

Kabangila alisema serikali inatumia mamilioni ya shilingi kuwatibu viongozi nje ya nchi lakini inashindwa kutumia pesa hizo kuwalipa madaktari stahili zao na kununua vifaa tiba vya kisasa.

Alisema Tanzania inaongoza kwa kupeleka wagonjwa nchini India, sifa ambayo alisema si nzuri na kwamba hatari zaidi viongozi serikalini wanajivunia hali hiyo.

Katibu huyo alisema wamekaa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na viongozi wengine wa serikali na wamewataadharisha juu ya mwenendo huo.

Kabangila alisema chama cha madaktari kitafanya mkutano wake mkuu Jumamosi ijayo, ambao pamoja na mambo mengine utajadili masuala ambayo yamejitokeza katika mgomo huo na kufikiria hatua zaidi za kuchukua.

Alisema wanaishangaa wizara ambayo baada ya kulipa posho za madaktari wanafunzi wamewaita wahusika wizarani na kwamba hatua hiyo ni kukwepa hoja ya msingi.

Kauli ya Serikali
Madaktari hao 229 walianza mgomo Jumanne wiki iliyopira, wakiishinikiza Serikali iwalipe posho zao za Desemba mwaka jana ambazo ni zaidi ya Sh179 milioni.

Kwa mujibu wa madaktari hao, uamuzi huo ulifikiwa baada ya wizara kushindwa kuwalipa posho zao kwa wakati hali iliyowafanya waishi kwa tabu.

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Hadji Mponda, alikiri hali hiyo na kusema kuwa imesababishwa na ukata ulioikumba wizara hivyo kushindwa kuwalipa madaktari hao kwa wakati.

Dk Mponda alisema kwa kawaida posho hizo hulipwa tarehe 22 ya kila mwezi na kwamba kiasi cha fedha ambacho hulipwa ni Sh900 milioni kwa madaktari wanafunzi nchi nzima.

Pamoja na maelezo hayo, serikali iliwapa barua za kujieleza madaktari wote waliokuwa wamegoma licha ya kwamba baadhi yao walishaanza kurejea kazini baada ya kuwa wamelipwa posho hizo.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA