· Waziri waghembe aambiwa Wizara
imemshinda
· Serikali Mbeya yajitenga, yasema
isiingiliwe
· Wakurugenzi wajitoa, wawaachia
wanasiasa
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbozi
mkoani hapa Aloyce Mdalavuma ambaye ni muhanga wa kura za maoni za Ubunge
katika uchaguzi Mkuu 2010, amesema kuwa chama chake ni legelege ndiyo maana
kimeunda Serikali legelege
Hayo aliyasema jana katika kikao cha pamoja kati ya
Waziri huyo, Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro, wakuu na wakurugenzi wa wilaya
za Mbozi, ileje, Mbeya Vijijini na Rungwe, wafanyabiashara na wakulima wa zao la
Kahawa.
Mdalavuma alisema kuwa, wakulima wilayani Mbozi wamekosa
pembejeo msimu wa mwaka 2010-2011 na Serikali imekaa kimya jambo ambalo
linamkumbusha kauli ya kwamba chama legelege huunda Serikali
legelege.
‘’Ndugu waziri, umekuja hapa tukifikiri kuwa utazungumzia
mustakabali wa uuzaji na ununuzi wa kahawa mbivu na upatikanaji wa pembejeo
lakini tunashangaa hakuna majibu ya namna hiyo na hii nakumbuka kauli isemayo
chama legelege huzaa serikali legelege’’alisema Mdalavuma huku wadau wakiguna na
Prof, Maghembe akishika tama.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo ya Mbozi Erick Ambakisye
alimtisha Waziri Maghembe kuwa endapo anguthubutu kutekeleza kanuni za wizara
yake zinazoruhusu kununua kahawa mbivu wilayani humo ambayo wakulima wanaitaka
wakati Halmashauri haihitaji atakuwa tayari kwenda kwa Rais Jakaya Kikwete ili
waziri huyo achunguzwe.
Alisema kuwa anavyomfahamu Waziri huyo, anaamini kuwa
wizara hiyo ya Kilimo chakula na Ushirika imemshinda na Jimbo lake pia
limemshinda ndiyo maana wananchi wake hawana uchumi
imara.
Kwa upande wao, wakulima zaidi ya 400 waliofika katika
ukumbi wa Halmashauri hiyo ya Mbozi walimzuia Waziri Maghembe kuingia ukumbini
hapo kwa madai kuwa waliokuwa ndani ya ukumbi walikuwa ni wafanyabiashara ya
kahawa na wala si wakulima na ndiyo maana wao kama wakulima halisi walikataliwa
na viongozi wa Halmashauri kuingia ukumbini.
Baada ya hali hiyo ya vuta nikuvute huku Afisa usalama wa
wilaya hiyo akijaribu kuwasukuma wakulima hao ili Waziri aingie ndani na
kuzungumza na ‘’wakulima maalum’’ waliokuwa wameandaliwa bila mafanikio huku
asijue kuwa kulikuwa na wakubwa zake katika msafara huo, ndipo Mkuu wa mkoa wa
Mbeya Abbas Kandoro alitumia busara ya kuwataka wateue
wawakilishi.
Wakulima wengi walisema kuwa taarifa aliyokuwa amepewa na
viongozi wa Mkoa wa Mbeya iliyosema kuwa uuzaji wa kahawa mbivu inawaingizia
hasara siyo ya kweli bali ililenga kuwanufaisha watu wachache wakiwemo vigogo wa
Halmashauri zinazolima zao la kahawa mkoani Mbeya.
Mkulima Abrahamu Nzowa alisema kuwa, wakati Serikali na
baadhi ya watendaji wa Halmashauri hizo zikiwa zinaipiga vita biashara hiyo hasa
kampuni ya Lima Ltd inayonunua zao hilo kwa bei kubwa kuliko vikundi ambavyo
viongozi hao wanamanufaa navyo, vikundi vinaendelea kuwanyonya wakulima hali
ambayo wamesema inaleta kutoelewana miongoni mwao.
Aidha walisema kuwa kwasababu kahawa ni mali yao
hawataacha kuuza kahawa hiyo mbichi kwa kampuni ambayo itakuwa inanunua kwa bei
nzuri licha ya wilaya na mkoa kukataza kuuza kahawa
hiyo.
Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro alimweleza Waziri
Maghembe kuwa msimamo wa Serikali ya mkoa wa Mbeya ni kwamba haitaki kusikia
uuzaji na ununuzi wa kahawa mbivu mkoani hapa mpaka pale wakulima
watakapoandikishwa na kutambulika.
‘’Sisi kama mkoa wa Mbeya tuliazimia katika vikao halali
vya wadau wa mkoa na kwamba hatutaki biashara ya kahawa mbivu na kwasababu hapa
hakuna wakulima walioandikishwa hawa wote si wakulima halali kisheria hivyo
mpaka hapo tutakapokamilisha zoezi la kuwaadikisha ndipo tutakapochukua maoni
yao’’ alisema Kandoro kwa kujichanganya.
Akizungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi huo
baada ya kuogopa hoja za Wakuu wa wilaya, wenyeviti wa Halmashauri za wilaya
hizo Nne huku wakurugenzi wote wakikataa kuzungumzia suala hilo lililochukuliwa
kisiasa zaidi, Waziri Maghembe alisema kuwa hatengui kanuni zenye baraka za
Wizara bali anachotaka bei ziboreshwe kwa wakulima.
‘’Mimi sijatengua kanuni za Wizara na Bodi ya kahawa juu
ya ununuzi wa kahawa m,bivu bali nilichokuwa nasema ni kwamba lazima wilaya
zisimamie sheria na kuhakikisha bei kwa wakulima wa kahawa zinasimamiwa na
kulipwa vema lakini Serikali ya mkoa nyie mmeisikia haitaki biashara hiyo’’
alisema Waziri Maghembe.
Alisema licha ya hayo yote kila mfanyabiashara wa kahawa
ama mnunuzi ni lazima awe na leseni ya biashara na haruhusiwi kununua kahawa kwa
mkulima ambaye hajaandikishwa ili kudhibiti ukwepeji mapato ya Serikali kupitia
biashara hiyo kama ilivyo sasa wilayani humo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa bodi ya kahawa nchini
Adolph Kumbulu na mwanasheria wa Wizara ya kilimo walisema kuwa ununuzi wa
kahawa mbivu umeongeza tija ya ubora wa kahawa Tanzania kutokana na ubora wa
usindikaji wake tofauti na usindikaji unaofanywa na
wakulima.
Hali hiyo ya mkanganyiko wa uuzaji na ununuzi wa kahawa
mbivu (Cherry) imeleta utengano wa baadhi ya wakulima ambapo Serikali hasa
vyombo vya usalama vinatakiwa kuliangalia kwa umakini kutokana na hali ilivyo ya
wananchi kujengeana chuki ikiwa ni pamoja na kuijengea chuki
Serikali.
Ubora wa kahawa upo katika ngazi nne ambazo ni P1,P2,P3
na Ponds, ambapo P1 inatoa madaraja Nane ambayo ni AA, A, B, PB, C, AF na F
ambapo madaraja yanayouzwa nje ya nchi ni AA,A,B, PB na daraja C.
Habari na pastor
|
Comments