Harry Redknapp amewaonya mahasimu wao wakubwa wa Kaskazini mwa London Arsenal kwamba Tottenham itapigana kiume kuishikilia nafasi ya tatu ya msimamo wa Ligi Kuu ya England.
Wakiwa wametoka sare ya 0-0 katika uwanja wa Stamford Bridges, Spurs ambao wapo katika nafasi ya nne wameweza kupanua wigo wa pointi hadi kufikia tano dhidi ya Chelsea katika mbio za kuwania nafasi nne bora na hivyo kujipatia upenyo wa kucheza Ligi ya Ubingwa wa Ulaya.
Lakini kwa sasa wapo pointi tatu nyuma ya Arsenal, wakati mwezi mmoja tu uliopita walikuwa wameipiku Arsenal kwa jumla ya pointi 10.
"Nahisi hali inatupendelea, Arsenal inakabiliwa na baadhi ya michezo migumu," alisisitiza Redknapp.
"Watacheza na Man City nyumbani kwao, vile vile Chelsea nyumbani kwao. Mechi zote hizo ni ngumu.
"Ghafla tumejikuta tukipitwa na Arsenal ambao tuliwazidi kwa pointi 10.
"Hali inaweza kubadilika. Hatuna budi kupigana kiume na kushinda michezo inayofuata."
Redknapp amewapa changamoto wake wa Tottenham kushinda angalao mechi zao sita kati ya nane zilizosalia za Ligi Kuu na kujipatia nafasi ya nne bora na hivyo kujihakikishia kurejea tena katika hekaheka za Ubingwa wa Ulaya msimu ujao.
"Tunakabiliwa na michezo afueni, ninavyohisi," aliongeza Redknapp.
Naye meneja wa muda wa Chelsea Roberto di Matteo alikiri kikosi chake huenda kinahitaji kushinda mechi zilizosalia ili kuiengua Spurs katika nafasi nne bora.
Di Matteo alisema: "Kuziba pengo, hatuna budi tushinde mechi zote zilizosalia."
"Itakuwa kibarua kigumu lakini kutoka siku ya kwanza nilipoteuliwa, tulifahamu kazi itakuwa ngumu.
"Kuna michezo minane imesalia na tutajaribu kushinda mechi nyingi kadri iwezekanavyo kujaribu kupata nafasi ya nne."
Di Matteo pia alionesha kukerwa kwa kikosi chake kunyimwa mkwaju wa penalti baada ya Ramires kuangushwa alipogongana na mlinzi wa Spurs Benoit Assou-Ekotto.
Comments