UTATA WATANDA AFYA YA LOWASSA

                                                              Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa
ATHIBITISHA YUKO HOSPITALINI, ASEMA ASINGEPENDA KUELEZEA KWA UNDANI KUHUSU AFYA YAKE
Ramadhan Semtawa
UTATA umegubika afya ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa baada ya taarifa mbalimbali kueleza kuwa yuko hospitalini nchini Ujerumani kwa matibabu.Takriban juma moja sasa kumekuwa na taarifa mbalimbali zikizungumzia afya ya Lowassa lakini hakukuwa na taarifa rasmi kutoka chanzo chochote kati ya Serikali, familia yake au Bunge kuzungumzia afya ya Mbunge huyo wa Monduli.

Jana, Lowassa akizungumza na mwandishi wetu kwa simu alisema kwamba yuko hospitali, bila kufafanua kuwa ni nje au ndani ya nchi, wala kueleza kinachomsibu.

Mahojiano hayo kati ya Lowassa na mwandishi wetu yalikuwa kama ifuatavyo:

Swali: Asalaam alaykum Mheshimiwa Lowassa.
Jibu: Waalaykum Salaam.

Swali: Mimi naitwa... (jina la mwandishi) kutoka gazeti la Mwananchi. Kwanza pole kwa matatizo ya kiafya yanayokusumbua.
Jibu: Ahsante.

Swali: Nimekupigia pamoja na kukupa pole, nilitaka kujua unaendeleaje na matibabu?
Jibu: Niko hospitalini kwa sasa naomba niache mambo mengine tutaongea baadaye.

Swali: Lakini, ni matibabu gani hasa unayopata?
Jibu: ... (akimtaja mwandishi) naomba niache niko hospitalini sasa hivi mambo mengine tuongee baadaye.

Lowassa alitoa majibu hayo majira ya saa nane mchana na alipopigiwa tena saa 10.20 jioni, alijibu kama ifuatavyo:

Swali: Naam, Mheshimiwa Lowassa nimekupigia tena mimi... (mwandishi akajitambulisha).
Jibu: ... Unataka nikuambie nini tena? Nilishakwambia niko hospitalini niache!

Swali: Sawa, natambua uko hospitalini, lakini wewe ni kiongozi ambaye umewahi kuwa Waziri Mkuu, hivyo Watanzania wangependa kujua maendeleo ya afya yako kutokana na utata ulioibuka na kama je, umelazwa hapo hospitalini au uko katika matibabu ya kawaida?
Jibu Niache, ninachokwambia niko hospitalini sasa unataka nini tena? Nisingependa kuzungumzia afya yangu kwa undani.

Bunge

Akizungumzia suala hilo juzi, Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashillilah alisema ofisi hiyo haijapata maombi rasmi ya mbunge huyo kwenda nje kwa ajili ya matibabu.

Dk Kashillilah alisema kwa utaratibu, Ofisi ya Bunge inashirikiana na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kuwapeleka wabunge wanaoumwa nje ya nchi baada ya kupata rufaa ambayo inatokana na ushauri wa kitaalamu wa madaktari wa ndani.

Alisema hadi juzi, hakuwa akijua aliko Lowassa na kama ana matatizo ya kiafya kama inavyozungumzwa au la: “Mimi ndiyo Ofisi ya Bunge na ndiyo nakwambia hatujapata maombi ya kutaka mheshimiwa Lowassa apelekwe nje ya nchi.”

Mtendaji huyo mkuu wa Bunge alisema wapo baadhi ya wabunge ambao huwa wanakwenda nje kwa vipindi maalumu kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kawaida wa afya baada ya matibabu lakini, katika orodha hiyo Lowassa hayumo.

“Tunao utaratibu wa baadhi ya waheshimiwa wabunge kwenda nje kwa mujibu wa ratiba zao kwa ajili ya kufanyiwa uangalizi wa kawaida wa afya zao. Lakini, hadi sasa (juzi) katika orodha hiyo mheshimiwa Lowassa hayumo,” alisema Dk Kashillilah.

Hata hivyo, kwa mujibu wa nafasi yake ya utumishi serikalini aliyokuwa nayo, Lowassa anaweza kupata matibabu nje ya nchi kwa kupitia utaratibu wa Serikali bila ya kuhusisha Bunge.

Juhudi za kupata Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda au Naibu wake, Dk Lucy Nkya zilishindikana kutokana na simu zao kufungwa na kutopatikana ofisini.Chanzo;gazeti la Mwananchi.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*