WAKE WA VIONGOZI WAIPIGA TAFU TAIFA QUEENS
MKE wa Waziri
Mkuu, Mama Tunu Pinda amewashukuru Watanzania kwa michango yao kwa ajili ya
kuiandaa timu ya Taifa ya Netiboli (Taifa Queens) iweze kushiriki mashindano ya
Afrika yanayotarajiwa kuanza Mei 8-12, mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Ametoa shukrani
hizo leo mchana (Jumanne, Mei Mosi, 2012) wakati alipokuwa akizungumza na
wachezaji wa timu hiyo katika kambi yao iliyoko Shule ya Filbert Bayi, Kibaha,
mkoani Pwani. Mama Pinda ni Mwenyekiti wa Kamati ya Iwezeshe Taifa Queens
Ishinde.
Mama Pinda
ambaye amewaongoza wake wa viongozi mbalimbali zaidi ya 20 ambao ni wanachama
wa New Millenium Group, alikabidhi katoni 40 za maji ya kunywa kwa Mwenyekiti
wa Chama cha Netiboli (CHANETA), Bibi Anna Bayi na mbele ya wanamichezo hao.
Mama Pinda alisema
wamebakiza kiasi cha sh. milioni 27 tu ambazo ni ahadi na kwamba kama zote
zitatimizwa wiki hii, hakutakuwa na taabu ya kufanikisha mashindano hayo.
“Gharama za kuwatayarisha wachezaji na kuendesha mashindano haya hapa
nchini zilikuwa jumla ya sh. 158,430,000/-.
Kati ya hizo, gharama za kuwaweka wachezaji kambini kwa matayarisho ni sh. 82,650,000/-
na gharama ya kuendesha mashindano kwa siku tano ni sh. 75,780,000/-,” alisema.
Aliwashukuru baadhi ya wafadhili ambao
walijitolea kulipia moja kwa moja gharama zilizokuwa kwenye bajeti kama vile
kulipia gharama za usafiri, uwanja wa michezo, viatu vya michezo, mipira, jezi,
track-suits na vifaa vingine.
Akitoa mchanganuo wa fedha ambazo zimekwishapokelewa, Mama Pinda alisema:
“Kwa waliojitolea vifaa mbalimbali, hadi sasa tunakiri kupokea vitu vyenye
thamani ya sh. 53,080,000/- na wale waliojitolea kwa fedha taslimu tumeshapokea
jumla ya sh. 77,800,000/-. Vilevile, tunazo ahadi zenye thamani ya sh. 27,550,000/-.
Kwa kifupi hali ya kifedha kwa sasa si mbaya kwani tunaamini walioahidi watatimiza
ahadi zao ndani ya wiki hii kabla mashindano hayajaanza”.
Mapema, katika
risala yao, wachezaji hao walisema wanakabiliwa na uhaba wa vifaa vya mbalimbalim
kama vile raba, kamba za kuruka, mipira na chupa maalum za maji. Timu ya Taifa
Queens ambayo ina wachezaji 16 na maafisa sita, inatarajiwa kuhitimisha kambi
Mei 6, 2012 na Mei 7, 2012 itahamia jijini Dar es Salaam ili kushiriki
mashindano hayo.
Baadhi ya
wake wa viongozi walioambatana na Mama Tunu Pinda ni Wake wa Makamu wa Rais, Bi
Zakia na Bi Asha Bilal, Mama Anna Mkapa, Mama Husana Kawawa, Mama Regina
Lowassa, Mama Sophia Mukama, Mama Janet Magufuli, Mama Josephine Makamba, na
baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Iwezeshe Taifa Queens Ishinde.
Comments