Skip to main content

MWANASHERIA MKUU ZANZIBAR AJIBU MAPIGO YA TUNDU LISU, NI KUHUSU MABADILIKO KATIBA YA ZANZIBAR.


Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Othman Masoud Othman (Pichani) ameshangazwa na mwanasheria mwenzake Tundu Lisu kwa kutofahamu madhumuni na malengo ya mabadiliko ya katiba ya Zanzibar yaliozaa serikali ya umoja wa kitaifa. Kauli ya Mwanasheria huyo aliitoa katika baraza la wawakilishi wakati akifafanua baadhi ya mambo ya kisheria baada ya wajumbe wa baraza hilo kumtaka afanye hivyo kufuatia kauli ya ya Tundu Lisu aliyoitoa bungeni wiki hii.
“Sasa kuja kwa haya yametuonesha kwamba kuna wenzetu kumbe wana fikra kwamba Zanzibar iliwahi kutawaliwa. Maana mtu anaposema marekebisho ya 10 ya Zanzibar yamjitangazia uhuru maana yake ana fikra na huyu ni mwanasheria mtu kafika mpaka kuwa mbunge anayeaminika na chama chake lakini anasema kwa kufanya hivyo Zanzibar imejitangazia kuwa huru kwani tuliwahi kutawaliwa?,” alihoji Othman.
Akijadili bajeti ya wizara ya makamu wa rais wa jamhuri ya muungano, huko Dodoma Mbunge wa Singida Mashariki wa Chama Cha (CHADEMA) Tundu Lisu alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa Zanzibar imefanya katiba kwa kujitangazia kuwa ni nchi.
Othman alisema marekebisho ya katika ya Zanzibar yalikuja baada ya hoja nyingi ambazo hazikuwa na majibu katika muungano ambayo ilikuwa ikisema ni Zanzibar ni sehemu ya muungano, lakini kama nini mkoa? Shehia? Kata? au kijiji?, haya hayakuwa na jibu katika katiba ya muungano.
Kufuatia maridhiano Zanzibar ndipo wazanzibari wakamaua kufanya kukufikia marekebisho ya 10 ya katiba yao ambayo ilifafanua kuwa zanzibar ni nchi na ndivyo ilivyo kwa sababu haikuwahi kutawaliwa kama ambavyo baadhi ya wanasiasa wanavyofikiria.
“Marekebisho ya 10 ilichofanya ni kusema kwamba ikiwa mtu hatambui, maana ilikuwa imeshaonesha dalili kwamba kuna wengine hawatambui hilo tena wakubwa. Sasa marekebisho ya 10 yalipokuja ni kufafanua tu, kama kuna mtu hatambui sisi wenyewe tunajitambua” alisema mwanasheria huyo huku akiungwa mkono na wajumbe kwa kupigiwa makofi.
Huku akishangiriwa na wajumbe wa baraza hilo mwanasheria mkuu alisema hakuna mtu ambaye atawazuwia kusema “Aaah katiba yenu isiwe namna gani au isiwe hivi na ndio maana unakuta katiba za muungano zipo nyingi lakini kila mmoja ina muundo wake kwa mujibu mlivyokubaliana nyinyi wenyewe.”
Mwanasheria mkuu alisifu muungano wa miaka mingi wa Uswizi ambao unatambulika na kuigwa duniani kutokana na kufuata misingi imara iliyowekwa na wananchi wenyewe.
Alisema muungano ambao umedumu na unasifiwa ni Swiss Federation kwa sababu umeanza tokea mwaka 1292 na umekwenda kwa mafahamiano hadi mwaka 1874 wakatunga katiba ambayo wameifanyia mapitio upya mwaka 1999 na nchi hiyo ina serikali 26, lugha nne rasmi na ndio muungano amabo umedumu na nchi ambayo ni imetulia duniani.
Mwanasheria huyo alisema mashirika yoye ya kimataifa yapo Uswizi kwa sababu ya muungano huo uliotumilia na kwa sababu umekuwa na misingi imara ya kuhakikisha muungano ule unaweza kuhimili mabadiliko yoyote yatakayokuja ya kisiasa.
“Mheshimiwa Naibu Spika nitumie fursa hii hapa hapa niseme wakati tupo katika mchakato wa maoni ya katiba nadhani ni wakati mzuri kuiweka sawa ile misingi ya muugano kama Uswizi,”na kuongeza: “Wakati mwengine napata wasiwasi nasema hii khofu yangu niiseme hapa kwamba tunaanza kubishana kuhusiana na watunza nyumba wawe wangapi, waendeshaji nyumba wawe wangapi, wawili, watatu, wanane au watano? Lakini tatizo letu la msingi mimi nadhani ni nyumba yenyewe iweje. Kama tunaamua kuishi, maana mfumo wa sasa hivi mmoja anaishi nyumba kubwa na mwengine mabandani huko uwani huo sio utaratibu tunao.”
Aidha aliwaambia wajumbe hao kwamba wanzanzibari wana mambo ya msingi ya kujadili kuliko kuzungumzia idadi ya watunza nyumba akimaanisha kero za muungano zilizopo na kushindwa kuafikiwa.
“Kwa hivyo mimi niwaombe sana waheshimiwa wajumbe, niwaombe na wazanzibari wenzangu na wananchi wote, kwamba huko mbele tusije tukalaumiana kwamba tumefanya marekebisho ya 10 kimakosa na tumejitangazia uhuru. Sasa hivi tuondoe fikra hizo lakini tunaweza kujieleza kwa hoja za msingi na mambo ya msingi katika hoja hii hapo ndipo tutakapojenga utawala bora ndani ya muungano,” aliongeza Mwanasheria huyo.
Akitoa ufafanuzi zaidi kwa wajumbe hao kuhusu muungano Othman alisema hata suala la uraia limepewa kipaumbele katika katiba ya Uswizi ambapo mtu anapozaliwa ndipo anapopewa uraia wake.
“Pale unapozaliwa ndio panapokupa uraia, na kuna mengi ambayo nadhani tatizo liliopo kwa wenzetu ni kwamba hawajifunzi kwamba muungano ni kitu gani. Muungano ni suala ambalo nchi mbili mnapoungana, nchi zilizokuwa huru ni suala la makubaliano na mtakachokubaliana ndicho ambachi kitakuja katika katiba yenu,” alisema Othman.
Othman ambaye ni mwanasheria aliyewahi kuandika waraka (paper) aliyoipa jina ‘masuala ya yasiokuwa na majibu ndani ya muungano’ aliwaambia wawakilishi hao kwamba maelezo ya Tundu Lisu yamejaa hadaa na yamejaa upotoshaji tena upotoshaji ambao umepindukia mipaka ya kweli.
“Mimi nimepata kusoma na kuangalia hiyo hutuba ya Mhe Tundu Lisu… lakini pia nimeona majibu ambayo yalitolewa na mhehsimiwa Shamsi Vuai Nahodha aliyesema kuwa maeelzo ya Mbunge Lisu yamejaa hadaa na upotoshaji naungana naye,” alisisitiza huku makofi ya wajumbe yakitawala ndani ya baraza hilo.
Tokea kuanza kwa kikao cha baraza la wawakilishi kwa kiasi kikubwa mijadala wa bajeti umetawaliwa na suala la muungano ambapo wajumbe wengi wamekuwa wakiungana na wananchi kudai maslahi zaidi kwa zanzibar ikiwemo kurejesha kwa hadhi ya rais wa zanzibar na mamlaka kamili ndani na nje ya nchi.
Imeandaliwa na Salma Said, Zanzibar

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.