CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimemwandikia rasmi barua Rais
Jakaya Kikwete, kikimtaka achukue hatua, kwa mujibu wa mamlaka yake kikatiba
kuhusu mauaji ya kisiasa.
Katika barua hiyo ya Septemba 10, mwaka huu, iliyoandikwa na Mwenyekiti wa
Taifa, Freeman Mbowe, pamoja na hatua nyingine CHADEMA imetaka Rais Kikwete
achukue hatua ya kuwafukuza kazi baadhi ya viongozi.
Wanaotakiwa kufukuzwa ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel
Nchimbi, IGP Said Mwema, Kamishna wa Operesheni wa Jeshi la Polisi, Paul
Chagonja, RPC wa Mkoa wa Morogoro, Faustine Shigolile na RPC wa Iringa, Michael
Kamuhanda, kwa kutowajibika kufuatia mauaji yaliyotokea katika mikoa ya Morogoro
na Iringa.
Aidha, CHADEMA kimetaka Rais Kikwete aunde tume ya kijaji/kimahakama ya
uchunguzi wa vifo vilivyotokea katika mikusanyiko, mikutano, maandamano au
mazingira ya kisiasa yaliyohusisha chama hicho.
Vifo hivi ni vile vilivyotokea Arusha Januari 5, mwaka jana, Igunga Novemba
mwaka huo huo, Arumeru Mashariki Aprili mwaka huu, Iramba Julai 14, Morogoro
Agosti 27 na Iringa Septemba 2, mwaka huu.
Kwamba wakati wakisubiri hatua za rais pamoja na majibu ya barua hiyo,
wanawaagiza viongozi na wanachama wake kutokutoa ushirikiano kwa kamati
iliyoundwa na Waziri Nchimbi na timu zilizoundwa na Jeshi la Polisi kuchunguza
mauaji yaliyofanywa na askari katika mikoa ya Iringa na Morogoro.
Mbowe alisema itakumbukwa kuwa katika maandamano yaliyoitishwa na CHADEMA
Januari 5, mwaka jana jijini Arusha, watu watatu walipoteza maisha baada ya
polisi kutumia nguvu na risasi za moto kutawanya waandamanaji.
“Katika uchaguzi mdogo wa Igunga pamoja na matukio mengine yaliyojitokeza na
yaliyohusisha vurugu kinyume cha sheria, Mbwana Masoud, mwanachama wa CHADEMA
alitekwa, kuteswa na kunyongwa katika mazingira ya kutatanisha. Mpaka sasa
hakuna hatua stahiki zilizochukuliwa kufanya uchunguzi kuhusu kifo hicho,”
alisema Mbowe.
Alisema kuwa mara baada ya uchaguzi mdogo wa Arumeru Mashariki, kiongozi wa
kata wa CHADEMA, Msafiri Mbwambo, alichinjwa na chanzo chake kudaiwa
kusababishwa na masuala ya kisiasa.
Aliongeza kuwa hivi karibuni yalitokea mauaji katika Kijiji cha Ndago, Wilaya
ya Iramba mkoani Singida ambapo kikundi cha watu kilivamia na kushambulia
mkutano wa CHADEMA kwa mawe, huku polisi wakiwepo bila kuchukua hatua.
“Baada ya mkutano kumalizika na viongozi wa CHADEMA kuondoka eneo la mkutano,
kijana mmoja anayedaiwa kuwa kiongozi wa kata wa UVCCM alikutwa amepoteza maisha
katika kijiji hicho, jirani na eneo ulipofanyika mkutano wa hadhara,” alisema
Mbowe.
Kwamba hivi karibuni tena katika maandamano ya mapokezi ya viongozi wa
CHADEMA mkoani Morogoro, polisi walimshambulia Ally Zona na kupoteza maisha, na
baadaye wakatoa taarifa kuwa aligongwa na kitu kizito.
Katika barua hiyo, Mbowe aliongeza kuwa hivi karibuni mkoani Iringa wakati wa
kufungua matawi ya chama chake kwenye Kata ya Nyololo, polisi walimlipua kwa
bomu mwandishi wa habari wa kituo cha Televisheni cha Channel Ten, Daudi
Mwangosi.
Alisema kuwa pamoja na polisi kuhusika na mauaji hayo, bado Waziri Nchimbi,
IGP Mwema, Kamanda Chagonja, makamanda Shigolile na Kamuhanda hawakuchukua hatua
yoyote ya kuwajibika kwa kuhusika moja kwa moja na matukio haya au kiutendaji
katika jeshi hilo kwa ujumla.
“Ili kupata ukweli wa sababu za vifo hivyo, mauaji yote haya hayajafanyiwa
uchunguzi wowote wa kimahakama/kijaji kwa mujibu wa sheria za nchi yetu kinyume
na ahadi ya waziri mkuu bungeni wakati akihitimisha hoja yake katika Bunge la
Bajeti la mwaka 2011/2012. Hakuna uchunguzi wa kifo ‘inquest’ uliofanyika na
hakuna Mahakama ya Korona ‘Coroner’s Court’ iliyoanzishwa ili kuchunguza vifo
hivi,” alisema Mbowe.
Kwamba Kamati Kuu ya CHADEMA katika kikao maalumu hivi k
aribuni, mojawapo ya
mambo yaliyoazimiwa ni kumwandikia barua rais kwa lengo la kumtaka achukue hatua
za utekelezaji kwa mujibu wa mamlaka yake na kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
“Iwapo serikali haitazingatia, CHADEMA kitawaongoza wananchi kwa njia za
kidemokrasia, ikiwemo maandamano ya amani kushinikiza hatua za haraka
kuchukuliwa kwa masilahi ya taifa,” alisema Mbowe.
Aliongeza kuwa katika majadiliano ya kina kabla ya kufikia maazimio na
maamuzi hayo, kamati kuu ilizingatia kuwa hali ya siasa nchini ni tete, serikali
inayoongozwa na CCM imeshindwa kusimamia vizuri rasilimali za nchi ikiwamo
kudhibiti mfumuko na ongezeko la bei, hivyo kuchangia ugumu wa maisha kwa
wananchi na migogoro ya kijamii na ufisadi nchini.
|
Comments