UNAPENDWA NA KUOGOPWA NA WATU WENGI
DUNIANI
UKO HATARINI KUPOTEZA ASILI YAKE
KABISA
Na Onesmo Ngowi
Masumbiwi au kwa majina mwengine ndondi au ngumi na
kwa majina ya mitaani ndogwa, mawe n.k. ni mchezo unapoendwa sana na watu wengi.
Aidha mchezo huu ni kati ya michezo inayoogopwa sana duniani. Mchezo wa ngumi
uko hatarini kupoteza maana yake ya asili yaani kucheza kama burudani,
kuwakilisha nchi na kujenga ushupavu wa mchezaji. Mamilioni ya watu wanaojazana
kuutazama wasingependa kabisa kujiingiza kuucheza mchezo wa ngumi.
Japokuwa katika maisha ya kawaida watu wengi
hupigana kwa sababu mbalimbali kama vile kuwa na hasira, kujilinda au kuwaonea
tu wengine kwa sababu mbalimbali lakini kwa kawaida ni watu wachache sana walio
tayari kujiingiza katika kuucheza mchezo huu.
Kama tulivyokwisha ona kwenye makala zilizotangulia,
ngumi ni mchezo ambao ulianza wakati wanadamu walipoanza tu kukunja ngumi na
kurushina kama mchezo. Mchezo wa ngumi upo wa aina mbalimbali.
Japokuwa kumbukumbu nyingi zinaonyesha kwamba
chimbuko haswa la mchezo huu linakubalika kuwa ni nchi za kusini mwa Ulaya
hususan Uyunani (leo Ugiriki) na Urumi (Italia ya leo) lakini kuna mataifa au
dola nyingine nyingi zilizokuwa na aina yao ya michezo iliyofanana na
ngumi. Wanazuoni wa maswala ya michezo wanaifananisha michezo yote
ya kupigana iwe ni kwa kutumia mikono na miguu au kutumia silaha za aina
mbalimbali na mchezo wa ngumi.
Aidha mchezo wa ngumi ni kati ya michezo inayojenga
ushupavu wa wachezaji na kuwafanya washujaa wa jamii. Wachezaji wa ngumi mara
nyingi ni watu wanaoonekana kama mashujaa kutokana na ujasiri wanaoonyesha
katika mchezo wenyewe.
Wakati wa utawala wa Marcus Aurelius, mtawala
shupavu wa iliyokuwa dola ya Roma (Italia ya leo) na aliyepata mafanikio makubwa
ya kuipanua dola ya Warumi (Italia) toka ukanda wa bahari ya Mediterania hadi
jangwa la barafu la Siberia huko Urusi, mashujaa wengi wa michezo walichuana
kwenye mashindano yaliyofanyika Coliseum (uwanja mkubwa uliokuwa umejengwa
katika jiji la Roma).
Mashujaa hawa ni pamoja na wapiganaji ngumi na
wengine walioshiriki kwenye michezo yenye hatari na kujijengea umaarufu mkubwa
kwenye jamii ya Warumi. Dola ya Warumi ilikuwa na nguvu sana katika bara la
Ulaya na ilienea hadi kaskazini mwa bara la Afrika. Hivyo utamaduni wao hususan
michezo iliyochezwa baada ya ushindi wa vita ulienea kwenye himaya yao yote.
Kwa mfano katika dola ya Manchuria (China ya leo)
iliyotawala kutoka Uchina na nchi nyingi za mashariki ya kusini mwa Asia ngumi
zilijulikana kama Kung-Fu ambazo japokuwa kuchezwa kwa ngumi hizi huchanganywa
na mateke.
Maaskari wengi walitakiwa wawe wamejifunza kupigana
Kung Fu na waujue mchezo wenyewe kwa kiwango kikubwa. Kwao Kung Fu ilikuwa ni
aina nyingine ya silaha na walizitumia ipasavyo kwenye kukabiliana na maadui
kwenye vita. Baada ya ushindi wa vita walikusanyika katika viwanja
vikubwa na kucheza michezo hii kama isahara ya kusheherekea ushindi wao.
Dola ya Kijapani iliyotawala nchi nyingi za Asia
ikiwa ni mpinzani mkubwa wa dola ya Manchuria katika karne ya 12 nayo ilikuwa na
mchezo wa ngumi uliojulikana kama Karate. Mashujaa wengi wa Kijapani walitakiwa
wawe na ujasiri wa hali ya juu wa kupigana Karate.
Kwao Karate ilikuwa sio mchezo tu bali ni ufundi wa
kumshinda adui kwenye vita. Ushindani mkubwa kati ya Wachina na Wajapani
uliifanya michezo ya Karate na Kung Fu kupata umaarufu mkubwa sana. Kila upande
uliuona mchezo wake kama bora kuliko mwingine.
Katika miaka ya karibuni watawa wengi katika ukanda
huu wanaojulikana kama Monks (monki) waiijifunza Karate na Kung Fu kwa kiwango
cha juu ili kujilinda na Maharamia waliokuwa wanawavamia na kuiba mali zao.
Mtawala Genghis Khan wa dola ya Mongolia (Mongol
Empire) ambayo ilitawala kuanzia Mongolia yenyewe hadi Persia (Irani), Babilon
(Iraki) na baadhi ya nchi za Balkan (Ulaya ya Kati) aliwachagua wapiganaji wake
kwa ustadi na uangalifu mkubwa. Kwa kutumia wapiganaji waliosheheni kila aina ya
ushupavu aliweza kushinda majeshi mengi na kuwa kati ya watawala walioogopewa
sana wakati wa enzi yake.
Dola ya Otoman ya Kituruki
iliyotawala katika karne ya 19 ilitumia mchezo ulioulikana sana na wengi kama
Mieleka ukichanganya na utumiaji wa farasi. Mara nyingi wachezaji wa mchezo huu
walifariki kutokana na ugumu wa mchezo wenyewe na watanzamaji walisisimka sana
kuona damu ikimwagika. Kwao huu ulikuwa ndio ushujaa tosha.
Nazo dola za Mafarao wa Misri zilikuwa na aina yao
ya michezo iliochezwa haswa na watumwa kwa minajili ya kuwafurahisha Mafarao na
familia zao hata katika kujitetea au kushambulia maaduni! Kwa dhati kabisa
mchezo wa ngumi ulivyojulikana na Wanafalsafa wa zamani katika ukanda wa
Mediterania katika dola nilizotaja hapo juu ulikuwa ni mojawapo ya vipimo vya
ujasiri wa mtu.
Sio vibaya watanzania
wakaelewa kuwa ngumi ni mchezo wa zamani sana kuchezwa hata kabla nchi yetu
haijatawaliwa na wakoloni katika karne ya 19. Michezo hii iliyochezwa katika
viwanja vikubwa vyenye mikusanyiko mikubwa ya watu (Coliseum) huko Roma na
(Arena) huko Athina, iliyokuwa katika hekalu kubwa la ufalme wa Wayunani
(Ugiriki) la Akropolis.
Viwanja hivi vilikuwa ndio
mwanzo wa ulingo wa kisasa kwani japokuwa ulingo wa kisasa ni wa mraba lakini
mwanzo wake ni Arena ya mduara.
Mwandishi wa makala haya ni: Rais wa
Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC), Shirkisho la Ngumi za Kulipwa
Afrika Mashariki na Kati (ECAPBF), Shirikisho la Ngumi la Kimataifa bara la
Afrika (IBF/AFRICA) na Mkurugenzi wa Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC).
E-mail: ibfafrica@yahoo.cm
Comments