MBIO ZA URAIS 2015 ZAANZA


Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais, Dk Jakaya Kikwete akisikiliza jambo kwa makini
CCM CHAPULIZA KIPENGA, WILAYA ZA IRINGA, SONGEA ZATANGULIA, DK NCHIMBI KIDEDEA UJUMBE WA NEC, LEO NI SUMAYE NA NAGU

Na Waandishi Wetu
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza rasmi chaguzi mbalimbali za uongozi kuanzia ngazi za wilaya ambazo zitatoa safu za uongozi wa chama hicho watakaokiongoza kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015, ambao utatanguliwa na ule wa Serikali za Mitaa wa 2014.

Chaguzi hizo zilianza jana kwa baadhi ya wilaya kuchagua wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec), wenyeviti wa wilaya na safu nyingine za uongozi huku leo idadi ya wilaya zikitarajiwa kuongezeka.
Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete akifungua kikao cha Nec, mjini Dodoma Jumanne iliyopita, alisema chama hicho kimepitisha majina ya vijana wengi kugombea nafasi mbalimbali ili kutengeneza timu ya ushindi katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu ujao.
Alisema katika uteuzi huo, vijana watapewa nafasi zaidi kutokana na ukweli kuwa, chama bila ya vijana hakiwezi kuwa imara kwa sababu ndiyo nguvu ya ushindi.
Wilaya ambazo jana zilifanya uchaguzi ni Iringa Mjini, Songea Mjini, Songea Vijijini, Mbinga na Namtumbo.
Katika uchaguzi wa Songea Mjini, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi aliibuka kidedea katika nafasi ya ujumbe wa Nec.
Habari kutoka ndani ya mkutano huo zinasema kwamba waziri huyo alishinda baada ya kupata kura 722 huku mpinzani wake Yusuf Mwambola akiambulia kura 54.
Uchaguzi huo unafanyika huku baadhi ya wanaCCM ambao waligombea na majina yao kukatwa na Nec wakilalamika kuwa kilichowaponza ni kushiriki katika mchakato wa kutaka kumwondoa madarakani Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wakati wa Bunge la Aprili, mwaka huu.
Baadhi ya vigogo walioondolewa majina yao kugombea nafasi mbalimbali ndani ya chama hicho ni pamoja na Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe, Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono, Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla na Mbunge wa Kahama, James Lembeli.

Mchuano mkali Hanang’
Wilaya za Babati Mjini, Mbulu na Hanang’ zinatarajiwa kufanya uchaguzi leo ambako macho na masikio yataelekezwa Hanang’ ambako Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye anachuana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk Mary Nagu katika nafasi ya ujumbe wa Nec.
Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara inatarajiwa kufanya uchaguzi wake Jumatatu na mchuano mkali unatarajiwa kuwa katika nafasi ya Mjumbe wa Nec ambayo inagombewa na Mbunge wa Jimbo hilo, Christopher Ole Sendeka na mfanyabiashara maarufu na Diwani wa Kata ya Mirerani, Justine Nyari.

Katika Mkoa wa Pwani, uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika leo katika wilaya tatu. Katibu wa CCM mkoa huo, Sauda Mpambalioto alizitaja wilaya hizo kuwa ni Kibaha, Mafia na Rufiji.
Alisema Wilaya za Bagamoyo, Kisarawe na Mkuranga zitafanya uchaguzi huo kesho.
Katibu wa CCM Wilaya ya Mbarali, Paul Mwita alisema uchaguzi wilayani hapo unatarajiwa kufanyika leo.
“Wagombea wa nafasi mbalimbali wameshapewa taarifa kamili na mkutano huo utafanyika katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Mount Fort,” alisema Mwita.
Mkoani Tabora, Wilaya za Urambo na Uyui zinatarajiwa kufanya uchaguzi leo. Kwa upande wa Wilaya ya Nzega uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika leo na kesho.
Wilayani Igunga, Katibu wa chama hicho, Mery Maziku alisema kuwa uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika Oktoba Mosi. Tabora Mjini uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika kesho katika ukumbi wa Utumishi wa Umma.

Vijana wachaguana
Uchaguzi wa Jumuiya ya Vijana wa CCM, UVCCM wilayani Kishapu, Shinyanga umefanyika na Luhende Luhende aliyekuwa akitetea kiti chake kuibuka kidedea.
Uchaguzi huo umerudiwa baada ya mara ya kwanza kufanyika Agosti 28, mwaka huu. Katika uchaguzi huo, Luhende aliibuka mshindi kwa kupata kura 223 huku mpinzani wake, Paul Kimali akipata kura 216.
Hata hivyo, Luhende hakutangazwa mshindi kwa kuwa hakupata zaidi ya nusu ya kura hivyo uchaguzi huo kurudiwa jana.
Katika uchaguzi wa jana, Luhende alipata kura 243 na mpinzani wake, Kimali alipata kura 190.
Akizungumzia ushindi wake, Luhende aliahidi kufanya kazi ya kujenga umoja miongoni mwa vijana wa wilaya hiyo katika kipindi cha miaka mitano bila kuwabagua.
Kimali alisema uchaguzi huo ulikuwa mkali na kuahidi kutoa ushirikiano kwa mpinzani wake katika kipindi chote cha uongozi wake.
Imeandikwa na Suzy Butondo, Kishapu; Joseph Lyimo, Manyara; Julieth Ngarabali, Pwani; Godfrey Kahango, Mbarali na Mustapha Kapalata, Tabora.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*