KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, askari polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia
(FFU) wilayani Ngorongoro, mkoani Arusha, kwa agizo la Mkuu wa Wilaya (DC) hiyo,
wamevamia kijiji usiku wa manane, kupiga mabomu na kupora mali.
Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia juzi kuanzia saa nane hadi saa kumi
katika Kijiji cha Kisangiro, kwa kile kilichodaiwa kuwa walikuwa wakisaka silaha
za moto zinazodaiwa kumilikiwa na wakazi wa jamii ya Kisonjo, maarufu kama
Watemi.
Uvamizi huo umefanyika ikiwa ni siku chache tangu DC huyo, Elias Wawa Lali,
kufanya mkutano na viongozi wa kimila wa jamii hiyo kijijini hapo siku ya
Jumamosi wiki iliyopita.
Katika mkutano huo, aliwatisha watu wa jamii hiyo akiwataka wasalimishe
silaha hizo za kivita aina ya SMG na SAR pamoja na mifugo aliyodai
waliwanyang’anya wafugaji wa Kimasai hivi karibuni wakati wa vurugu za
kugombania ardhi.
Wawa Lali alijigamba mbele ya wazee hao kuwa amekwisha kuanza kufunga mizigo
kwa ajili ya kuondoka pamoja na familia yake, hivyo akatoa siku tatu agizo lake
hilo liwe limetekelezeka, vinginevyo angewaamuru FFU wavamie kijiji hicho kwa
nguvu kusaka silaha hizo na mifugo.
Wakizungumza na gazeti hili kwa hofu jana, baadhi ya wakazi hao wakiwemo
wazee, walisema kuwa walivamiwa usiku wa manane na askari hao waliofika eneo
hilo wakiwa na magari mawili na kuanza kupiga mabomu, kuvunja nyumba na kupora
mali mbalimbali.
Walisema kuwa hadi jana waliweza kubaini nyumba 31 zilizobomolewa, yakiwemo
maduka na mali mbalimbali zikiwa zimeporwa, huku vijana watano wakikamatwa na
askari hao na kushikiliwa katika Kituo cha Polisi Loliondo.
“Kwenye mkutano wetu na mkuu wa wilaya, tulikubaliana atupe siku zaidi ili
tufanye uchunguzi dhidi ya madai yake kuwa baadhi yetu wanamiliki silaha za moto
na kama zitapatikana tutazisalimisha, lakini tumeshangazwa kuona tunavamiwa
usiku na askari wakipiga vijana wetu na kupora mali,” alisema mmoja wa wazee
hao.
Wazee hao ambao wanamlalamikia mkuu wa wilaya hiyo wakidai anaegemea upande
wa Wamasai katika mgogoro huo, walisema kuwa tukio hilo la juzi limesambaratisha
kijiji, kwani vijana na watoto wamekimbilia kusikojulikana wakihofia mabomu ya
polisi.
“Mpaka sasa hakuna silaha waliyoipata wala mifugo, zaidi wameleta hofu
kijijini kwetu, watoto wamekimbia hawaendi shule, hatujui wako wapi. Askari
wamekuja kuvunja nyumba zetu na kupora, serikali ipo wapi na huu ni utawala bora
upi?” alihoji mmoja wa wazee hao kwa hasira.
Kwa muda mrefu sasa jamii hizi mbili za Wasonjo na Wamasai wa ukoo wa Loita,
zimekuwa kwenye mgogoro mkubwa wa ardhi kiasi cha kusababisha vurugu
zilizopoteza maisha ya watu, kujeruhi na mifugo kadhaa kupotea.
Agosti 24 na Septemba mosi mwaka huu, jamii hizo ziliingia tena kwenye
mapigano katika kijiji hicho eneo la Naan zikigombea ardhi, ambapo kila upande
unadai ni sehemu yake.
Mapigano hayo yalisababisha watu saba kujeruhiwa na mifugo zaidi ya 800
kupotea.
Hata hivyo, baada ya msako mkali wa polisi wa Tanzania kwa kushirikiana na
maofisa wa Kenya kwa kutumia helikopta, mifugo zaidi ya 700 ilipatikana na
silaha kadhaa zilikamatwa kutoka pande zote.
Lakini mkuu wa wilaya hiyo, amekuwa akiwaandama Wasonjo kuwa walisalimisha
silaha mbili tu wakati wenzao Wamasai wamesalimisha zote, jambo linalopingwa na
Wasonjo hao wakidai anakumbatia jamii hiyo ya Loita ambayo inatokea Kenya.
Kwa mujibu wa wazee hao, Loita ni wavamizi kutoka Kenya kwani jamii nyingine
ya Wamasai asili ya Tanzania za Laitayok, Salei na Kisongo wanaishi nazo bila
migogoro yoyote.
Madai hayo yaliungwa mkono na mkuu wa wilaya alipozungumza na gazeti hili kwa
njia ya siku Ijumaa iliyopita, akisema hali hiyo ilijidhihirisha wakati wa
mapigano ya karibuni kwani baada ya mifugo ya Wamasai hao kutekwa na Wasonjo,
maofisa wa Kenya waliingilia kati kusaidia kuitafuta.
Alisema kuwa
Wamasai wa Tanzania wamekuwa wakiwaalika wenzao kutoka Kenya na
kuishi nao pamoja na kuwapatia malisho, na kwamba serikali kupitia Idara ya
Uhamiaji inaendelea kuwachunguza.
Katika kushughulikia mgogoro huo, Julai mwaka 2005, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa
Arusha, Mohamed Babu, aliandika barua ya kuzuia matumizi ya ardhi husika baada
ya juhudi za usuluhishi kushindikana.
Katika zuio hilo, pia Mkuu wa Wilaya wa wakati huo, Kapteni mstaafu Msengi na
Katibu Tawala waliandika barua kusisitiza eneo hilo lisitumike kwa matumizi
yoyote kama kulima, kutundika mizinga, kulisha mifugo na kukata majani hadi hapo
ufumbuzi utakapopatikana.
Lakini katika hatua ya kushangaza Wamasai wameachwa wakiendelea kulikalia
eneo husika na kufanya shughuli zao wakati wenzao wa jamii ya Wasonjo kila
wanapojaribu kufanya shughuli zao katika eneo hilo, serikali ya wilaya
inawakamata na kuwafungulia mashitaka kwa uvamizi.
Alipoulizwa juu ya uwepo za zuio hilo, mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, alikiri
lakini akasema ofisi yake haina barua hizo hadi sasa. Na kuhusu hatua ya FFU
kuingia kijijini hapo usiku juzi na kufanya uharibifu na uporaji, alidai hizo
habari anazisikia kwa mwandishi.
“Hizo habari nazisikia kwako, mimi bado nasubiri majibu kutoka kwa wazee,”
alijibu Wawa Lali kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu yake ya
kiganjani. Chanzo;Tanzania Daima
|
Comments