YANGA KUIBUKIA KWA MAAFANDE WA JKT RUVU LEO?
Kikosi cha
Mabingwa wa Kombe la Kagame Yanga, ambacho kesho kinashuka Uwanja wa
Taifa kuivaa JKT Ruvu katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
DAR ES SALAAM, Tanzania
BAADA ya kuyumba katika mechi mbili za kwanza
za Ligi Kuu ya Bara, Yanga, leo Jumamosi wanashuka dimbani kwa mara ya tatu kuwakabili JKT Ruvu ya Pwani kwenye
Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
Yanga iliyokuwa ikipewa nafasi kubwa ya
kufanya vema kutokana na usajili mzuri, iliianza ligi kwa sare ya 0-0 dhidi ya
Prisons kabla ya kufungwa 3-0 na Mtibwa Sugar.
Matokeo
hayo yanaifanya Yanga leo kukutana na JKT Ruvu ikiwa nafasi ya pili kutoka
mkiani, ikiwa na ponti moja, haijafunga bao huku nyavu zake zikitikiswa mara
tatu.
Wapenzi
na mashabiki wa timu hiyo wameshikwa na butwaa wakihoji yako wapi mashuti ya
akina Saidi Bahanunzi, Didier Kavumbagu, Hamisi Kiiza na vipi ukuta imara wa
timu hiyo, uruhusu mabao matatu.
Licha
ya ukuta wake kusukwa na Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani, Mbuyu Twite
na viungo Athumani Idd ‘Chuji’, Haruna Niyonzima, waliruhusu nyota wa Mtibwa
kufunga mara tatu.
Akizungumzia
mechi ya leo, Kocha Mkuu wa timu hiyo, Tom
Saintfiet, amewataka nyota wake kusahau kipigo hicho, wapambane kuhakikisha
wanashinda kuanza safari upya.
Alisema
ni matumaini yake kushinda mechi ya leo licha ya ubora wa wapinzani wao, ambao
nao watakuwa wakitaka ushindi kusawazisha makosa ya kufungwa mabao 2-0 na Simba.
Hata
hivyo, Saintfiet alisema kwa kuitambua vizuri taaluma yake, hata ikitokea
akapoteza mechi ya leo, hatajuta akitambua kuwa ni sehemu ya mchezo.
Pia,
amewasihi wapenzi na mashabiki wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi kuipa sapoti
timu yao kwa
kuishangilia, akitambua kuwa hamasa ina nafasi yake katika kupigania ushindi.
Kuhusu
kikosi chake, Tom amesema Bahanunzi, Salum Telela na Juma Seif ‘Kijiko’ ndio
majeruhi, wengine wote wako fiti kuipigania timu yao.
Vita
nyingine ya ligi hiyo iliyoanza Septemba 15, itakuwa kwenye Uwanja wa Chamazi
kwa wenyeji Azam kuwakaribisha wababe wa Yanga, Mtibwa Sugar.
Mechi
nyingine itakuwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha kwa JKT Oljoro
kuwakabili Polisi Moro huku
Coastal Union ikiwaalika Toto African ya Mwanza Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Comments