Novemba 9,
2012
UCHAGUZI TAREFA, TAFCA SASA DESEMBA
22
Uchaguzi wa
viongozi wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tabora (TAREFA) na Chama cha
Makocha wa Mpira wa Miguu Tanzania (TAFCA) sasa utafanyika Desemba 22 mwaka
huu.
Kwa mujibu wa
ratiba za uchaguzi za vyama hivyo, Kamati zao za uchaguzi zitatangaza kuanza
mchakato wa uchaguzi Novemba 10 mwaka huu wakati fomu kwa wanaotaka kugombea
uongozi zitaanza kutolewa Novemba 12 mwaka huu. Mwisho wa kuchukua na kurudisha
fomu ni Novemba 16 mwaka huu.
Kamati ya
Uchaguzi ya Shirkisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imetoa mwongozo huo kwa
Kamati ya Uchaguzi ya TAFCA baada ya kuomba hivyo kutokana na wagombea sita tu
kujitokeza kuomba nafasi tatu za uongozi katika mchakato wa awali.
Kwa waombaji
ambao awali walichukua na kulipia ada ya fomu za kugombea uongozi TAFCA na
TAREFA, hawatatakiwa kulipia tena ada kwa nafasi zile zile walizoomba, isipokuwa
watatakiwa kujaza fomu upya.
PONGEZI KWA
UONGOZI MPYA FA MWANZA
Shirikisho la
Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha
Mpira wa Miguu Mkoa wa Mwanza (MZFA) uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika
Novemba 8 mwaka huu.
Ushindi
waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza chama hicho unaonesha jinsi wajumbe
wa Mkutano Mkuu wa MZFA walivyo na imani kubwa kwao katika kusimamia mchezo huo
katika Mkoa wa Mwanza.
TFF inaahidi
kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Kamati za Utendaji ya MZFA iliyochaguliwa chini
ya uenyekiti wa Patrick Songora aliyechaguliwa kwa kipindi cha pili
mfululizo.
Uongozi huo
mpya wa MZFA una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha
shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba ya chama chao pamoja na vyombo
vya mpira wa miguu vilivyo juu yao.
Pia tunatoa
pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya MZFA na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa
kuhakikisha uchaguzi unaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama
wa TFF.
Viongozi
waliochaguliwa kuongoza MZFA ni Patrick Songora (Mwenyekiti), Nassoro Mabrouk
(Katibu) na Richard Kadutu (Mwakilishi wa Klabu TFF).
Boniface
Wambura
Ofisa
Habari
Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Comments