Membe akalia kuti kavu Nec

Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe akiteta jambo na Zitto Kabwe wa Chadema

Dodoma
KAMPENI za kuegemea makundi ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), zinazidi kukitafuna chama hicho baada ya kundi la makada wa chama hicho kumpigia kampeni chafu, mmoja wa wagombea wa Ujumbe wa Halmashauri Kuu Nec, kupitia Kapu, Bernad Membe.

Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa kundi hilo la makada linapiga kampeni ya kutaka Membe asichaguliwe katika nafasi hiyo,ili kumharibia harakati zake za kutaka kuwani urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kupitia chama hicho.

“Unajua wanachotaka kikifanya ni kumfanya ashindwe kuwa mjumbe wa Nec ili wawe na hoja ya kusema kwamba kama ameshindwa kupata hata ujumbe wa Nec atafaa kuwa rais,” alisema mmoja wa makada wa CCM waliopo mjini Dodoma kuhudhuria mkutano mkuu wa uchaguzi wa chama hicho unaoanza Novemba 10.

Kampeni zinazofanywa na kundi hilo dhidi ya Membe na watu wengine ambao hawakubaliki katika kundi hilo kwa njia ya kutoa taarifa kupitia ujumbe wa simu na mdomo kufahamishana msimamo wao.

Membe
Hata hivyo,Membe ambaye ni pia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, alipotakiwa kuzungumzia suala hilo jana alisema kuwa, amepata taarifa kundi hilo kufanya kampeni chafu dhidi yake na akatangaza kiama dhidi ya wabaya wake kuwa watarajie kuona anapata ushindi wa kimbunga katika uchaguzi huo.

''Nakubaliana kabisa kwamba ziko njama za kunihujumu ambazo hata mimi nazijua, lakini wabaya wangu hao wanafanya jambo ambalo hawalijui, kwani kama wangejua wasingepoteza muda huo,'' alisema Membe.

Hata hivyo, alikataa kumtaja mtu ambaye anamhujumu, lakini akasema kuwa lipo kundi ambalo linapoteza muda wao na kuwaza habari za yeye bila ya kujua wanashindana na nguvu ya aina gani.

Waziri huyo alisema kuwa maajabu atakayoyaonyesha siku ya Novemba 13 yatakuwa ni makubwa kiasi ambacho hao waanaotaka kumhujumu watajua.

Alijifananisha na mti wa muembe ambao hutupiwa mawe wakati wote kuliko mchongoma wenye miiba ambao alisema hauwezi kutupiwa mawe kwani hauna kitu cha kuchukua juu yake.

''Kwa mfano ningeshangaa sana kama ningepita bila ya kupata misukosuko, kweli ningeshangaa sana maana nimezoea kupambana na misukosuko, lakini kitendo cha kutokea misukosuko kwangu kinadhihirisha kabisa mimi ni nani juu yao,'' alisema Membe huku akikunja ngumi kuonyesha yuko tayari kwa mpambanao huo.

Alipotakiwa kueleza kama njama hizo zinaendana na makundi ya urais alisema '' hilo mimi sijui, lakini nasisitiza kuwa njama mbaya dhidi yangu zipo na kwa vyovyote nitashinda ushindi mkubwa.''

Aliwafananisha wapinzani wake kuwa ni watu wasiokumbuka kwani walifanya hivyo hata katika uchaguzi uliopita, lakini alishinda na hata katika kipindi hiki wataaibika tena.

''Mimi niliwachapa katika kipindi kilichopita na waliaibika ndivyo ninavyowatangazia hata katika kipindi hiki kuwa ni vita takatifu, lazima nitawachapa tena kwa kichapo cha hali ya juu.'' alisema huku akionyesha kujiamini zaidi.

Kundi hilo mbali ya kupigia kampeni mbaya, Membe limetoa orodha ya wagombea ambao litawapigia kura katika nafasi ya ujumbe wa Nec.

Katika orodha hiyo yumo, Naibu waziri wa Mawasiliano, Januari Makamba ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya nje ya CCM, Katibu Mkuu wa Chama hicho, Wilson Mukama, Mweka Hazina wa chama hicho, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Nchi ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Steven Wasira na Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa chama hichjo UVCCM taifa, Martine Shigela.

Wengine ni Mbunge wa Nkenge,Asumpta Mshama, Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), William Lukuvi, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, David Mathayo, Jackson Msome na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na michezo, Fenella Mukangara.

Vita kubwa inaonekana kuwa katika nafasi 10 za ujumbe wa Nec kwani mawaziri sita ni miongoini mwa wanachama 31 wa Bara watakaopamba vikali kupata nafasi hizo.

Hali ni hiyo pia kwa upande wa Zanzibar kwani katika wanachama 28 wanaowania nafasi 10 za Nec Zanzibar, wapo mawaziri wanne.

Mbali na mawaziri sita nafasi 10 za Tanzania Bara pia kuna wabunge watatu, mkuu wa wilaya mmoja na vigogo wawili wa Kamati Kuu ya chama hicho.

wa upande wa Zanzibar wamo mawaziri wanne akiwamo Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi.

Wajumbe waanza kuingia
Mji wa Dodoma na vitongoji vyake umeaanza kufurika baada ya wajumbe wa mkutano mkuu kuanza kuwasili.

Tangu jana makao makuu ya CCM, kumeonekana watu wengi wakiingia na kutoka huku wakiwa wamevaa nguo zenye rangi ya chama hicho.

Mwananchi ilishuhudia Wauza nguo pamoja na makada wengine wa chama hicho baadhi yao wakiwa na vipeperushi vya wagombea walikuwa wakipishana katika milango ya jengo hilo la CCM wakitafuta kupata vitambulisho vya kuingilia katika Ukumbi wa Kizota utakapofanyikia mkutano huo.

Taarifa kutoka ndani ya CCM katika kamati ndogo ya mapokezi zinasema kuwa ,siku maalumu ya kuwasili kwa wageni ilikuwa ni jana, lakini wengi wanatarajia kuingia leo.

“Sisi tuliweka vyumba maalumu kwa ajili yao kuanzia jana (leo), lakini taarifa tulizonazo wengi wataanza kuingia leo na tayari walishapiga simu kuulizia vyumba vyao,” alisema mtoa taarifa.
Kiongozi huyo wa CCM ambaye alikataa kutajwa jina lake kwa sababu sio msemaji wa chama, alisema wale watakaoingia kuanzia jana watatakiwa kujilipia gharama kwa siku moja kutokana na ukweli kuwa CCM kililipa gharama hizo kuanzia leo.

Alibainisha kuwa wengi wa wageni wanaoingia kuanzia leo ni ambao kwa namna ama nyingine wanaonekana licha ya kuwa ni wajumbe, lakini wanakuja kwa kazi maalumu ya kuwapigia debe baadhi ya wagombea.

Akizungumzia ujio huo alisema kuwa ,hadi jana walishakamilisha maandalizi ya nyumba kwa sehemu kubwa na leo wanatarajia kuwasilisha
taarifa yao kwa kamati kuu ya maandalizi ambayo iko chini ya Ofisi ya Katibu Mkuu wa CCM.

Katika nyumba mbalimbali za mji wa Dodoma, vyumba vimechukuliwa na CCM kwa ajili ya wajumbe wake wa mkutano mkuu.

“Hii nyumba imechukuliwa vyumba vyote na Chama Cha Mapinduzi, hivyo kama mtu anakuja hapa anatakiwa kulala usiku wa kuamkia kesho tu kisha anatakiwa kuhama,” alisema Pendo ambaye ni mhudumu wa moja ya nyumba za kulala wageni eneo la Mji mpya.

Mhudumu huyo alikiri taarifa za kupandisha bei katika kipindi cha mkutano na kusema ni kweli wanafanya hivyo kutokana na hali halisi inavyobidi.

Katika eneo la CCM Makao makuu, wafanyakazi wa ngazi za chini wameeleza kuwa upepo wa kisiasa unamwendea vizuri Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia bunge Willian Lukuvi kuliko wengine.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*