RAIS KIKWETE ASISITIZA USHIRIKANO SIPO II.
Na Zawadi Msalla
- MAELEZO
Arusha.
Rais Jakaya Kikwete ameiasa Jumuiya ya Maendeleo ya
Nchi Kusini mwa Afrika (SADC) kuimarisha ushirikiano kati yake na nchi wanachama
wa Jumuiya hiyo ili kufanikisha utekelezaji wa Mkakati wa pili wa
kushughulikia masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Jumuiya hiyo.
Rais Kikwete ameeleza hayo wakati akizindua Mkakati wa
kushughulikia masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama wa Jumuiya hiyo (SIPO II)
jijini Arusha wakati wa mkutano uliowahusisha wawakilishi mbalimbali kutoka
katika Jumuiya wanachama wa SADC.
Amesema ili malengo ya Mkakati huo yaweze kufanikiwa ni
lazima ushirikiano wa ndani na nje wa nchi hizo wanachama uimarishwe na
kuongeza kuwa SADC haiwezi Kutegemea mikakati ya ndani ya ulinzi na Usalama ya
nchi fulani kutaka kutekeleza mkakati wake.
"SADC haitakiwi kuiingilia kwa kutaka kuibadili
mikakati ya ndani ya Nchi wanachama ya ulinzi na usalama badala yake
washirikiane kwa karibu kuangalia nini cha kufanya" Amesema Rais.
Kuhusu umuhimu wa mkakati huo Rais Kikwete amesema
utakuwa muongozo wa SADC katika masuala yote ya ulinzi, usalama na siasa, na
umejikita katika kutatua vikwazo mbalimbali vya kiulinzi
vilivyopo.
Amefafanua kuwa Utekelezaji wa SIPO na maazimio yake
utapelekea hali ya amani na utawala bora kwa Nchi nyingi za Afrika na kuongeza
kuwa katika awamu ya pili ya SIPO mabadiliko mengi yamefanyika yakiwemo
uongezaji wa vipaumbele katika mfumo wa utekelezaji na ufuatiliaji wa masuala ya
ulinzi na usalama.
Uzinduzi wa SIPO II utaangalia ushirikiano kati ya Nchi
wanachama, ushirikiano katika masuala ya kibiashara, uhakika wa kushughulikia
masuala ya upatikanaji wa Amani na ushirikiano katika nyanja ya
habari.
Akieleza historia ya chombo cha Usalama cha SADC alisema
kabla ya kuanzishwa kwa chombo hicho kulikuwa na ushirikiano wa nchi katika
masuala ya ulinzi na usalama na kubainisha kuwa kuanzishwa kwa SIPO kunatokana
na nchi wanachama kuona umuhimu wa kuwa na chombo kinacho waongoza katika
masuala hayo yote.
Awali akizungumza na wajumbe wa mkutano huo Waziri wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Benard Membe amesema kuwa SIPO imekuwa
ni nyenzo muhimu nay a kutegemewa na nchi za SADC katika masuala yote ya
usalama.
Amesema SIPO ilizinduliwa rasmi mwaka 2004 na baadae
kufanyiwa marekebisho ya kimsingi mwaka 2007 na kueleza kuwa kutokana na
marekebisho hayo ya Mwaka 2007 ilikubaliwa kuwa mikakati na vapaumbele vya SIPO
iwe inapitiwa kila baada ya miaka mitano.
Aidha uzinduzi huo utafuatiwa na mafunzo mbalimbali
yatakayoendeshwa na wataalamu kwa muda wa siku nne
Comments