Rose Muhando Kutikisa Tamasha la Shangwe Kagera


MWIMBAJI maarufu wa muziki wa Injili nchini, Rose Muhando pichani na mwenzake Enock Jonas (Zunguka) wanatarajiwa kutia chachandu katika tamasha la kwanza kubwa kufanyika Mkoani Kagera.Tamasha hilo la Shangwe Kagera lina lengo la kuielimisha jamii na kuamsha mwamko wa kusaidia watoto yatima na wanaoishi katika maisha magumu. Mkurugenzi wa Kampuni ya Beula Communications Ltd, ambao ni waandaji wa tamasha hilo, Melkizedeck Mutta, anasema kuwa matayarisho ya tamasha hilo yanaendelea vizuri kutokana na mwitikio mkubwa wa watu mbalimbali waliojitokeza kushiriki.
Pia, Mutta alisema bendi ya muziki ya wazawa mkoa huo, Kakau Band pamoja na vikundi vingine vya wanakwaya wa makanisa mbalimbali, kikundi cha watoto yatima wanatarajia pia kutumbuiza. Mutta anasema tamasha hilo la aina yake linatarajiwa kufanyika Uwanja wa Kaitaba na pia kwenye ukumbi wa Lina’s mjini Bukoba, siku ya Uhuru, Desemba 9.
“Mpaka sasa tumekamilisha sehemu kubwa ya matayarisho hayo ikiwamo kulipia uwanja pamoja sehemu ya malipo kwa wasanii ambao watashiriki,” alisema.
Pia, mkurugenzi huyo aliwaomba wadhamini zaidi na wadau wengine wa maendeleo ya watoto kujitokeza kushiriki ili kuwasaidia jamii hasa watoto yatima na wengine wanaoishi katika mazingira magumu. Muta alisema malengo ya tamasha hilo ni kuhamasisha jamii kuishi kwa amani, kupendana na kusaidia watu wengine hasa wasiojiweza kimaisha ili na wao wajione ni sehemu yao.
Katika kutambua hilo kampuni yetu iliamua kufanya utafiti mdogo nakugundua changamoto nyingi katika Mkoa wa Kagera, mojawapo ni kuwa na watoto wengi wanaoishi katika mazingira magumu. Baada ya kuliona hili, tulitembelea vituo mbalimbali vya kulelea watoto hao, mojawapo ni Tumaini Children’s Centre kinachomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Ki lutheri Tanzania (KKKT).
Kituo hiki kinalea watoto wote bila kujali kabila,jinsia wala dini zao, kwa sasa kituo hiki kinahudumia watoto zaidi ya 800, kwa kuwapatia elimu,chakula, malazi n.k ambapo kwa muda mrefu kimekuwa kikipata msaada toka Sweden ambao kwa sasa wametangaza kuusitisha kwa maelezo kuwa jamii ya Watanzania inapaswa kujifunza na kuanza kuhudumia watu wao wenyewe.
Kutokana na hilo ndiyo maana tumeonelea tuwe na tamasha la kuamasisha jamii ili ianze kuona umuhimu wa kusaidia wenzao wanaohitaji msaada.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI

KOCHA WA AL.AHLY ASEMA YANGA NI TIMU BORA NA NGUMU