JESHI LA SIMBA LIPO KAMILI KUTAFUNA LIBOLO JUMAPILI

Simba SC

Na Prince Akbar
WAWAKILISHI wa Tanzania katika Ligi ya Mabingwa Afrika, wanaendelea vizuri na kambi yao ya kujiandaa na mchezo wa kwanza wa Raundi ya Kwanza dhidi ya Recreativo de Libolo ya Angola mwishoni mwa wiki. 
Ofisa Habari wa Simba SC, Ezekiel Kamwaga amesema kikosi hakina majeruhi mpya na wachezaji wote wanaendelea na mazoezi vizuri kwenye Uwanja wa Kisasa wa Tanzania Game Trackers Safaris (TGT), Arusha. 
Amesema timu inafanya mazoezi mara mbili kwa siku na kesho inatarajiwa kurejea jijini Dar es Salaam na kwamba uongozi wa Simba SC unavishukuru vyombo vya habari hapa nchini ambavyo vinazidi kuarifu jamii kuhusiana na mechi hiyo itakayochezwa Jumapili Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
"Hata hivyo, uongozi wa Simba ungeomba sapoti zaidi katika namna ya kuripoti mechi hizi za kimataifa. Kwa mfano, leo hii kuna gazeti limeandika kuhusu umafia (unyama) ambao Libolo wamefanyiwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) la kutopewa uwanja wa kufanyia mazoezi.".
"Pamoja na maelezo mazuri ya Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, kwamba kilichofanyika kipo ndani ya kanuni za CAF, bado gazeti hilo limeandika kwamba huo ni unyama. Tunaomba kueleza machache kwa vyombo vyetu vya habari hapa nchini."alisema. 
Alisema mwishoni mwa mwaka jana, wachezaji na baadhi ya  wanaounda jopo la ufundi la Timu ya Taifa la Vijana (Ngorongoro Heroes) walipigwa na askari nchini Kongo kwenye mechi za kuwania kufuzu michuano ya CAF kwa Vijana.
"Hakuna gazeti hata moja la Kongo lililoripoti kuhusu vipigo na mateso waliyopata Watanzania nchini humo na timu yao ikashinda. Msimu uliopita, Simba ilinyimwa kufanya mazoezi kwa siku tatu katika mji wa Shandi nchini Sudan kwa sababu zisizo na kichwa wala miguu,". 
"Hakuna chombo chochote cha Sudan kilichoripoti kuhusu tukio hilo ingawa hiyo ilikuwa ni miongoni mwa sababu zilizosababisha Simba itolewe kwenye michuano hiyo. Msimu huo huo uliopita, wachezaji wa Simba waliachwa wakipigwa na baridi ya nyuzi joto 4C nje ya uwanja wa mazoezi kwa zaidi ya saa nzima mjini Setif, Algeria kwenye mechi ya CAF Orange Cup... Hakuna chombo chochote cha habari cha Algeria kilichoripoti kuhusu hili,".
"Hivyo ndivyo vilikuwa vitendo vya kinyama. Lakini Simba SC inaamini TFF ilifanya ilichofanya kwa mujibu wa kanuni. Ujumbe ambao Simba SC inataka kuufikisha kwa wadau wetu wa vyombo vya habari ni kufahamu kwamba vyombo vyetu haviko kwa ajili ya kutetea wageni. Vyombo hivi vinatakiwa kusaidia vilabu vya Tanzania viliwakilishe taifa vizuri katika mashindano,"alisema.
Kamwaga alisema si nia ya Simba SC kutaka vyombo vya habari vya Tanzania vitetee unyama, bali ni kuona vyombo vya habari vinakua chachu ya kusaidia timu zetu zifanye vizuri na si kusaidia timu za kigeni kwa vile timu zetu zikienda ugenini huwa hazisaidiwi na yeyote.
"Ombi letu kubwa kwenu ni kwamba uzalendo utangulie kwenye kuripoti matukio makubwa ya kimichezo hapa kwetu,"alisema Kamwaga na kuongeza kwamba kesho kutakuwa na mkutano na waandishi wa habari katika Ofisi za Makao Makuu ya Simba Mtaa wa Msimbazi jijini Dar es Salaam.
Katika Mkutano Huo, Simba inatarajiwa kutangaza habari kubwa kuhusu mustakabali wake katika siku zijazo na kwamba itakuwa hebari njema kwa wote wenye mapenzi mema na klabu na taifa letu kwa ujumla

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.