KUMBUKUMBU YA MAREHEMU GEOFFRET NKURLU
Thursday, February 21, 2013
MAREHEMU NKURLU |
Kazi ya Mungu haina makosa, lakini kwetu ni majonzi makubwa.
Kama binadamu tungekuwa na uwezo wa kukata rufaa ya kifo, hakika nasi
tungekata rufaa mbele ya Mungu ili turudishiwe baba yetu kipenzi,
Geoffrey Nkurlu, na kuendelea kuishi pamoja nae hapa duniani.
Hakika, tunajikuta tukiandika barua hii kwa uchungu mkubwa, maana
familia yako inaadhimisha miaka 12 ya kukukosa kwako, tangu hapo tarehe
kama ya leo 17/2/2001 ulipotutoka na kuwa mbali na sisi.
Baba mpendwa, watoto wako wote bado tumeshikamana kwa pamoja kama jinsi
wewe ulivyotulea na kutusisitiza tuwe wamoja. Tuko pamoja katika dhiki
na faraja,hakika tunaendelea kukuwaza, kukukumbuka, kukuenzi na kuishi
katika maadili bora ambayo ulitufunza.Kwa kweli tunakulilia miaka yote,
maana mchango wako ni mkubwa katika kuilea familia yako, ambayo leo hii
imeweza kusimama imara kutokana na malezi mema na mapenzi yako.
Baba mpendwa, sisi watoto wako, wakati mwingine kila tunapokufikiria,
hakika mioyo yetu inashindwa kuamini kama ni kweli haupo pamoja nasi.
Tangu kuzaliwa kwetu, umeweza kutulea, kutusumbukia na kutusomesha kwa
kidogo chako ulichokuwa unakipata.
Kitendo kama hicho ni cha kipekee. Nani kama wewe? Maisha yetu bila
wewe, yangekuwaje katika kipindi cha maisha yetu, tangu kuzaliwa kwetu,
kukua na kufikia katika kila kipindi kigumu ambacho daima ni picha
kamili ya maisha yetu.
Ingawa tupo mbali na wewe, lakini umetutoka kimwili tu, kiroho tuko na
wewe. Bado tunakumbuka kauli zako, ushauri wako katika familia yako
uliyoiacha katika wasiwasi mkubwa. Tumelia sana. Tumeumia sana.Na
tuonapo baba wa wenzetu wakifurahia na kupata hata mawaidha, nasi huwa
tunaukumbuka uwepo wako.
Picha na mtiririko wa maisha yako ni ushahidi kuwa wewe ulikuwa baba
bora kwetu, huku tukiamini Mungu muweza na muumba wa yote ataitumia
fursa hiyo kama sehemu ya kukulaza mahali pema kwa unyenyekevu wako.
Suala zima la kifo, linaashiria kuwa ni sehemu ya mpito katika maisha ya
duniani. Vitabu vyote vya dini vimekitaja kifo kuwa hakuna kiumbe
ambaye anaweza kuvuka bila kupitia katika hatua hiyo, hivyo tunatumia
nafasi hii kukuombea mwanga wa milele ukuangazie.
Baba mpendwa, wakati tunaendelea kuyakumbuka mazuri yako katika familia
hii uliyoiacha hali ya kuwa bado inakuhitaji, macho yetu yanashindwa
kuhimili mtiririko wa machozi katika mboni zetu, yakiwa ni mapenzi
makubwa baina yako na yetu.
Kazi ya Mungu haina makosa, lakini kwa upande wako ni ngumu mno kukubali
matokeo na kujua kweli hatutakuwa wote katika kipindi cha maisha ya
duniani. Umetangulia baba. Jina la bwana libarikiwe,sisi tunaendelea
kukulilia miaka yote.
Tusingeweza na hatukuwa na sababu ya kuzuia hitaji la Mungu. Ingawa sisi
tulikupenda na kukuhitaji sana, lakini Mungu alikupenda zaidi na aliona
muda wako wa kuishi duniani umekoma na hakika ulistahili kwenda kwake
kwa mapenzi yake, kwa vile kifo ni njia yetu sote na kila nafsi itaonja
mauti. Dunia tunapita.
Sisi watoto wako, Masala, Matina, Nzigia, Amani, Angaza na Atuza.
Tunakulilia na kukuombea daima.
Comments