NAIBU WAZIRI WA AFYA NA USTAWI WA JAMII, DK SEIF RASHID AKIFUNGUA KONGAMANO LA 8 LA MFUKO WA TAIFA WA BIMA YA AFYA NA WANAHABARI MTWARA







HOTUBA YA MHE. DKT. SEIF S. RASHID (MB.),
NAIBU  WAZIRI WA AFYA NA USTAWI WA JAMII  KATIKA KONGAMANO LA NANE LA BIMA YA AFYA  LA WANAHABARI,  KATIKA UKUMBI WA CHUO CHA ELIMU MTWARA TAREHE 21 - 22 FEBRUARI, 2013







·       Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia,  Waziri - Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,

·       Mheshimiwa Aggrey Deaisile Mwamri - Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,

·       Mheshimiwa Abass Kandoro - Mwenyekiti wa Wakuu wa Mikoa,

·       Mheshimiwa Joseph Simbakalia - Mkuu wa Mkoa wa Mtwara,

·       Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Wakuu wa Wilaya

·       Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya za Mikoa ya Mtwara na Lindi,

·       Wakurugenzi wa Halmashauri za Mikoa ya Mtwara na Lindi,

·       Waganga Wakuu wa Mikoa  na Wilaya – Mikoa ya  Mtwara na Lindi,

·       Bwana Emanuel Humba, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya,

·       Waratibu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii wa mikoa ya Mtwara na Lindi,

·       Wanahabari kutoka vyombo mbalimbali,

·       Wageni Waalikwa,

·       Mabibi na Mabwana,


Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia Afya njema siku ya leo na kutuwezesha kukusanyika hapa. Vile vile, naushukuru Uongozi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kunialika kuwa mgeni rasmi katika Kongamano hili muhimu kwa Ustawi wa Sekta ya Afya. Kwa niaba ya Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, napenda niwakaribishe wote na kuwatakia heri ya mwaka mpya, 2013.  Pia niwashukuru wenyeji wetu kwa mapokezi na maandalizi mazuri ya kongamano hili ambalo nimeambiwa ni la nane.  Hongereni sana.

Ndugu Washiriki,
Kama ilivyoelezwa katika taarifa ya utangulizi na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Lengo Kuu la Kongamano hili ni kupata taarifa za utafiti uliofanywa na wanahabari katika halmashauri 26 mbalimbali hapa nchini,katika Utafiti huo kulikuwa na changamoto na mafanikio yaliyojitokeza, ni matarajio yangu kuwa mtajadili taarifa hiyo kwa umakini na kuupatia ufumbuzi wa pamoja wa changamoto zilizojitokeza. Aidha, ni matumaini yangu kuwa mafanikio yaliyopatikana katika uchangiaji ngazi za halmashauri mtayapa kipaumbele na kuyatangaza.  Katika kutoa habari za mafanikio kwa wananchi ni vema tuwafahamishe juu ya hali ya upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya, uimarishaji wa miundombinu, motisha zinazotolewa kwa watoa huduma ngazi ya Halmashauri,  haya ni mambo ambayo kwa ujumla wake yatawapa moyo zaidi wananchi na watendaji kwa kuona kuwa mambo haya yanawezekana.  Nawaombeni mjadiliane kwa uhuru na uwazi na ukizingatia kuwa watendaji wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya  ambao wapo pamoja nasi, watakuwa na jukumu la kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu uendeshaji wa Mfuko.  Masuala ya kisera yatatolewa ufafanuzi na Wawakilishi kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Ndugu Washiriki,
Ili kuhakikisha kuwa fedha zinazochangwa na wananchi kwa lengo la kuboresha huduma za afya nchini zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa, Serikali ilitoa muongozo wa matumizi ya fedha za uchangiaji mwaka 1997 ambao ulielekeza kipaumbele cha fedha za uchangia kiwe ununuzi wa dawa hasa katika ngazi ya Halmashauri.  Katika kusisitiza umuhimu wa suala hili serikali iliagiza kuwa fedha zitokanazo na Mfuko wa Afya ya jamii (CHF), Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Fedha za Papo kwa Papo, Fedha za Tele kwa Tele, ilielekezwa kuwa asilimia 67 ya fedha hizo zitumike kwa ajili ya kununulia dawa. 

Wizara yangu na Serikali kwa ujumla tunatarajia kuwa utafiti wenu utatoa picha halisi ya hali ilivyo katika Halmashauri zetu. Hususan, matumizi ya fedha zitokanazo na michango ya mifuko ya jamii. Vile vile, matokeo ya utafiti huu yatatusaidia sana kubaini kasoro na mapungufu na hata ushauri wa wananchi kuhusu namna bora zaidi ya kuimarisha utendaji wa sekta ya afya.  Vile vile, nauagiza uongozi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuwasilisha taarifa ya utafiti na majumuisho ya kongamano Wizarani kwa utekelezaji.

Ndugu Washiriki,
Kongamano hili leo linatimiza miaka nane ambacho ni kielelezo tosha cha umuhimu wa kuwashirikisha wanahabari katika masuala yanayohusu sekta ya afya pamoja na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.  Kauli Mbiu ya Kongamano ya mwaka huu inasema “Matumizi Sahihi ya Fedha za Uchangiaji Katika Halmashauri ili kuboresha huduma katika vituo vya matibabu”. Binafsi napenda kuupongeza Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kuona umuhimu wa kuwashirikisha wana hahari katika kufuatilia changamoto za utoaji wa huduma zenu ili baada ya Kongamano wapate taarifa za kina kuhusu hali ilivyo kwenye Halmashauri zetu ambapo kuna wanachama wa Mfuko wa Afya ya Jamii.

Ndugu Washiriki,
Naomba niwakumbushe wanahabari kupitia vyombo vyenu vya habari kuwa, mnao wajibu mkubwa kutoa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF), kitu ambacho kitawasaidia wao kupata matibabu ya uhakika na kupitia michango yao itatuwezesha kununua dawa za ziada. Naomba wanahabari msisubiri kongamano kama hili, lakini kila mnapoona inawezekana tumieni kalamu zenu na ujuzi wenu wa kufuatilia mambo ili muisaidie Serikali kubaini changamoto zinazowakwaza wananchi katika kujiunga na Mifuko ya Afya ya Jamii na mifumo mingine ya uchangiaji wa huduma.

Ndugu Washiriki,
Baada ya kusema hayo machache, naomba niwashukuru tena kwa kunikaribisha kushiriki nanyi katika kongamano hili. Hivyo natamka kuwa Kongamano la Nane la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Wanahabari limefunguliwa rasmi.

Ahsanteni kwa Kunisikiliza

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.