Wazazi mkoani Lindi watakiwa kusimamia maendeleo ya elimu ya watoto wao

Mama Salma Kikwete akihutubia mamia ya wananchi wa mkoa wa Lindi waliohudhuria sharehe za kutimiza miaka 36 ya Chama cha Mapinduzi zilizofanyika kimkoa katika kijiji cha Rondo kata ya Chiponda mkoani Lindi tarehe 5.2.2013. PICHA/JOHN LUKUWI   
***************************
Na Anna Nkinda – Maelezo , Lindi

Wazazi mkoani Lindi wametakiwa kusimamia elimu ya watoto wao kwa kuhakikisha kuwa wanaenda shule, wanakagua madaftari yao na kuwarekebisha  pale ambapo wamekosea kwa kufanya hivyo  watafaulu  vizuri katika masomo  na kufanikiwa kimaisha kwani elimu ni msingi wa maendeleo.

Wito huo umetolewa jana na mke wa Rais Mama Salma Kikwete kwenye kilele cha sherehe za maadhimisho ya miaka 36 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) zilizofanyika kimkoa katika kata ya Rondo wilaya ya Lindi  vijijini.

Mama Kikwete ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri kuu ya CCM taifa toka wilaya ya Lindi mjini alisema kuwa maendeleo ya elimu si mazuri katika mkoa huo hivyo basi kina baba washirikiane na wake zao kuhakikisha kuwa watoto wanahudhuria shule na kufanya vizuri katika masomo yao.

“Ninyi watoto nawasihi msome kwa bidii mkumbuke kuwa huu si wakati wa mtoto kukatisha masomo kwa ajili ya kupata ujauzito  kwani mkiwa na elimu kutakuwa  na uhakika wa kupatikana kwa wataalamu mbalimbali katika mkoa huu na kutatua tatizo la kutokuwa na  wataalamu ambalo limedumu kwa muda mrefu”, alisema Mama Kikwete.

Aidha Mjumbe huyo wa Halmashauri kuu ya CCM taifa aliwataka wanawake kutosubiri nafasi za upendeleo za viti maalum bali wagombee nafasi mbalimbali za uongozi ndani na nje ya chama  ili wafike katika ngazi ya maamuzi na kuachana na fikira kuwa wao hawawezi kumwaga sera wakati wa uchaguzi.

Alimalizia kwa kuwataka  wakazi wa mkoa  huo kudumisha amani, upendo na utulivu, kufanya  kazi kwa bidiii, maarifa na kujituma, wakulima walime kilimo cha kisasa ambacho kitawafanya wavune mazao mengi zaidi pia wafanyakazi  watumie muda wa kazi kufanya kazi na kuwahudumia wananchi.

Mama Kikwete pia alifungua jengo la ofisi ya CCM lenye thamani ya shilingi milioni 35 ambalo limejengwa na Mbunge wa jimbo la Mtama ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Benard Membe.

Waziri Membe alisema kuwa jengo hilo lina vyumba sita ambavyo ni  ofisi za jumuia zote za chama hicho ambazo ni Vijana, Wanawake, Wazazi, pia kuna ofisi za Mbunge, Mjumbe wa NEC na chumba cha mikutano.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM wa mkoa huo  Ally Mtupa aliwataka wanachama wa chama hicho  kuwa na  mahusiano mazuri baina yao na  viongozi wanaowaongoza. Wakisikia jambo wasiwe na papara ya kukimbilia kuandamana bali wafanye upelelezi kwanza na wakishabaini ukweli ndipo wachukue hatua.

Mtupa alisema, “Hivi sasa kuna watu wanapita mitaani na kupotosha ukweli kuwa Serikali yetu haijaleta maendeleo, wamesahau kuwa wanatembea katika barabara na kutibiwa   katika Hospitali zilizojenga na CCM, tunawaomba watu hawa wawaheshimu viongozi wanaotawala kwani hata vitabu vya dini  vinasisitiza umuhimu wa kuwatii viongozi waliopewa mamlaka ya kutawala”.

Sherehe hizo zilienda sambamba na mchango wa matembezi ya mshikamono ambapo zaidi ya shilingi milioni mbili zilipatikana, ufunguzi wa ofisi za CCM, ufanyaji wa usafi wa mazingira , kuwatembelea wagonjwa mahospitalini, utoaji wa kadi kwa wanachama wapya ambapo wanachama wa kawaida 286 , jumuia ya wazazi 63 na kutoka vyama vya upinzani 23 walipewa kadi.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.