WAZIRI KAGASHEKI NA WAZIRI WA MAREKANI HAYES KUZINDUA KITUO CHA WAGENI KATIKA WMA YA BURUNGE - MANYARA
Waziri wa Maliasili na
Utalii Balozi Khamis Kagasheki(Pichani) na Naibu
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Marekani Bwana David Hayes kwa pamoja watazindua
Kituo cha Wageni cha Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (Wildlife Management Area - WMA) cha Burunge Mkoani Manyara na
kukikabidhi kwa wananchi.
Uzinduzi huo ambao
utafanyika tarehe 5 Februari 2013 ni sehemu ya maadhimisho ya jumuiya za WMA
ambazo zilianzishwa nchini mwaka 1998 kwa mujibu wa Sheria ya Wanyamapori.
Pia,
ni kuonyesha mafanikio ya Programu ya kuendeleza WMA ambayo inafadhiliwa na
Serikali ya Marekani. Vilevile ni ishara kuwa Serikali ya Marekeni itaendelea
kuunga mkono shughuli za uhifadhi nchini Tanzania, hususan mapambano dhidi ya
ujangili.
Kituo cha Wageni cha
Burunge ni sehemu tu ya misaada inayotolewa na Serikali ya Marekani katika
Programu ya Kuendeleza WMA nchini kote. Kwa WMA ya Burunge misaada mingine ni
ujenzi wa barabara za kufanikisha uhifadhi, kujenga kituo cha askari wa
Wanyamapori na kujenga lango kuu la kuingilia kwenye eneo la WMA hiyo.
Jumuiya za Hifadhi za
Wanyamapori ni maeneo ya wanyamapori yanayohifadhiwa na kulindwa na Wananchi
kwa manufaa yao na taifa. Tangu zianzishwe mwaka 1998 kuna jumla ya WMA 17
nchini ambazo zimesajiliwa rasmi na wahusika kuruhusiwa kufanya matumizi
endelevu katika maeneo hayo. Aidha, kuna maeneo 21 ambayo yako katika hatua
mbalimbali za kuanzishwa WMA.
[MWISHO]
George Matiko
MSEMAJI
WIZARA YA
MALIASILI NA UTALII
4
Februari 2013
Comments