MWAKALEBELA AWASHAURI TFF MAMBO YA RUSHWA MICHEZONI!
Siku moja baada ya Shirikisho la Mpira
wa Miguu Tanzania (TFF) kumtaka mshambuliaji ,Nsa Job Mahinya ,wa
Coastal Union kuwasilisha maelezo yake juu ya madai kuwa alipewa rushwa
ya sh. milioni mbili ili asiifunge moja ya timu vigogo vya soka nchini, katibu mkuu wa zamani wa shirikisho hilo, Fredrick Mwakalabela, amesema suala hilo limechukuliwa kwa uharaka sana.
Mwakalabela amesema kauli ya kumwambia
kuwa, TFF itachukua hatua kali dhidi ya yake iwapo hatawasilisha maelezo
yake kuhusiana na suala hilo ingelenga kumtumia nyota huyo kama chanzo
cha taarifa zaidi zinazohusu masuala ya Rushwa michezoni kwani tatizo
hilo lipo hususani mwishoni mwa ligi.
“Kuna mambo mengi yalijitokeza miaka ya
nyuma, unakumbuaka suala la Ulimboka Mwakingwe na akina Shabaan Kado
wakati simba ilikwenda Morogoro, sidhani kama lilichukuliwa hatua
sutahiki,na ndio maana mambo haya yanaendelea kujitokeza chini kwa
chini”. Alisema Mwakalabela.
Mwakalebela alisema kuwa , kuna watu
wachache wanaotia doa soka letu kutokana na mazoea ya kucheza mchezo
mchafu na kupanga matokeo katika mechi muhimu.
Katibu huyo mkuu wa zamani wa TFF
alisema kuna wakati Fulani wachezaji hucheza chini ya kiwango wakidaiwa
kuwa na mapenzi na timu Fulani wakitarajia kusajiliwa, lakini mambo haya
hupuuzwa.
Mwakalebela aliongeza kuwa ,wachezaji
wanafahamiana nani kachukua rushwa katika mchezo fulani, cha msingi ni
kusimama kidete kupiga vita mchezo huu mchafu unaomaliza kiwango cha
soka letu.
Katibu huyo wa zamani wa TFF alisema pia waamzi mara kwa mara wanatuhumiwa kupokea hongo ili kuzisaidia timu fulani.
“Sauala la waamuzi pia linatakiwa
lichukuliwe kwa uzito wa juu, kuna mambo fulani yanajitokeza katika
michezo, hakika yanatia hofu kubwa, ukifuatilia ripoti za waamuzi huwa
zinafanana sana, lakini ukishihudia mchezo unaweza kugundua kuwa kuna
uhuni umefanyika”. Aliongeza Mwakalebela.
Mwakalabela alisisitiza kuwa wakati
akiwa kiongozi waamuzi na makamisaa wa mechi walikuwa wanaandika ripoti
inayofanana hata kama kulikuwa na matatizo, suluhisho ni kuwepo
mwangalizi maalumu wa waamuzi na hali ya mchezo husika ili kama kuna
mambo yasiyoeleweka wahusika wachukuliwe hatua zinazostahiki.
Katibu mkuu huyo wa zamani wa TFF
alishauri kuwa mambo haya yaangaliwe kwa jicho la tatu, na kama
yatapuuzwa timu zinazojihusishwa na uozo huu zitaendelea kuumbuka
kimataifa, pia timu ya taifa itakosa wachezaji wazuri.
Taarifa kutoka TFF hapo jana zilieleza
kuwa Job alikaririwa Aprili 3 mwaka huu na kituo cha redio cha Clouds FM
katika kipindi cha Amplifier kuwa alipewa kiasi hicho cha fedha na
kiongozi wa timu husika ili asiifunge katika mechi ya Ligi Kuu ya
Vodacom, lakini alipokea fedha hizo na kuifunga timu hiyo.
Baadaye kiongozi huyo alikuwa akimtaka
arejeshe fedha hizo. Pia TFF imekiandikia kituo hicho cha redio kutaka
nakala ya kipindi hicho ili pamoja na maelezo ya mshambuliaji huyo
vipelekwe katika Kamati ya Nidhamu kwa ajili ya hatua za kinidhamu.
Comments