Habari za kimichezo kutoka shirikisho la mpira wa miguu TFF
MECHI SITA KUONEKANA SUPERSPORT ‘LIVE’ SUPER WEEK
Kituo cha televisheni cha
SuperSport cha Afrika Kusini kitaonesha moja kwa moja mechi sita za Ligi
Kuu ya Vodacom katika Super Week kati ya Aprili 11 na Mei 18 mwaka huu.
Mechi hizo ni kati Azam
na African Lyon itakayochezwa Aprili 11 mwaka huu badala ya Aprili 10
mwaka huu kwenye Uwanja wa Azam Complex uliokoChamazi, Dar es
Salaam. Yanga na Oljoro JKT ambayo sasa itachezwa Aprili 13 mwaka huu
badala ya Aprili 10 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Azam na Simba itakayochezwa
Aprili 14 mwaka huu badala ya Aprili 13 mwaka huu Uwanja wa Taifa, na
mechi kati ya Coastal Union na JKT Ruvu itakayochezwa Aprili 16 mwaka
huu badala ya Aprili 10 mwaka huu.
Mechi nyingine ya Super Week
itakayochezwa Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga ni kati ya Mgambo
Shooting na Yanga itakayofanyika Aprili 17 mwaka huu badala ya Aprili 13
mwaka huu.
Pia mechi nyingine itakayooneshwa
live na SuperSport ni kati ya Yanga na Simba itakayofanyika Mei 18
mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kutokana na mechi za Super Week,
mechi kati ya Mtibwa Sugar na Oljoro JKT iliyokuwa ichezwe Aprili 13
mwaka huu sasa itachezwa Aprili 17 mwaka huu Uwanja wa Manungu, Turiani
mkoani Morogoro.
TFF YATAKA MAELEZO YA MCHEZAJI KUHUSU RUSHWA
Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) limemtaka mshambuliaji Nsa Job wa Coastal Union
kuwasilisha maelezo yake juu ya madai kuwa alipewa rushwa ya sh. milioni
mbili ili asiifunge moja ya timu vigogo vya soka nchini.
Job alikaririwa Aprili 3 mwaka
huu na kituo cha redio cha Clouds FM katika kipindi cha Amplifier kuwa
alipewa kiasi hicho cha fedha na kiongozi wa timu husika ili asiifunge
katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom, lakini alipokea fedha hizo na
kuifunga timu hiyo.
Baadaye kiongozi huyo alikuwa
akimtaka arejeshe fedha hizo. Pia TFF imekiandikia kituo hicho cha redio
kutaka nakala ya kipindi hicho ili pamoja na maelezo ya mshambuliaji
huyo vipelekwe katika Kamati ya Nidhamu kwa ajili ya hatua za kinidhamu.
TFF itachukua hatua kali dhidi ya
Job iwapo hatawasilisha maelezo yake kuhusiana na suala hilo, na
imetaka wadau kutoa ushirikiano ili iweze kupambana kikamilifu na
vitendo vya rushwa kwenye mpira wa miguu.
Comments