UFAFANUZI KUHUSU KUPITIWA UPYA KWA MATOKEO YA MTIHANI WA KIDATO CHA NNE MWAKA 2012
Mnamo tarehe 03 Mei, 2013 Serikali
kupitia Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Wiliam Lukuvi
(Mb) ilitoa Kauli ya Serikali Bungeni Kuhusu Taarifa ya Awali ya Tume ya
Taifa ya Kuchunguza Sababu za kushuka kwa ufaulu wa Mtihani wa Kidato
cha Nne Mwaka 2012. Kauli ya Serikali ilielekeza kuwa matokeo ya Mtihani
wa Taifa wa Kidato cha Nne mwaka 2012 yafutwe na yaandaliwe upya kwa
kutumia utaratibu uliotumika mwaka 2011 ili Wanafunzi hao wawe katika
mazingira yanayofanana na ya wenzao wa miaka iliyopita kwa kuwa mfumo
uliotumika mwaka 2012 katika kupanga matokeo na madaraja ni tofauti na
ule uliotumika mwaka 2011 na miaka iliyotangulia.
Kwa kuzingatia mapendekezo ya Tume
na Maelekezo ya Baraza la Mawaziri, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Ufundi, kwa mamlaka aliyonayo chini ya Sheria ya Baraza la Mitihani
Tanzania, kifungu cha 20, sura 107 ameliagiza Baraza la Mitihani la
Taifa kupitia upya Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne mwaka 2012.
Aidha, imeagizwa kwamba matokeo hayo yaandaliwe kwa kutumia utaratibu
uliotumika mwaka 2011. Serikali haikuagiza kufanyika upya kwa mitihani
hiyo na wala haikuagiza kusahihishwa upya.
Hivyo, Serikali inapenda
kuwahakikishia wananchi kwamba hapatakuwa na zoezi la kurudia
usahihishaji wa mtihani huo kwa sababu hakuna dosari zilizobainishwa
kwenye usahihishaji wa mitihani hiyo. Alama za watahiniwa ambazo
zimehakikiwa zipo tayari, kitakachofanyika ni kwa Baraza la Mitihani
kutumia alama hizo kuchakata matokeo upya kwa kutumia viwango vya ufaulu
vilivyotumika mwaka 2011. Utaratibu ambao umekuwa ukitumika tangu mwaka
1973 wakati Baraza lilipoanzishwa, ni wa kuweka viwango vya ufaulu kila
mwaka kwa kuzingatia ufaulu wa somo husika na ufaulu katika mwaka
uliotangulia.
Kutokana na maelezo hayo, ni
dhahiri kuwa zoezi la kupitia upya matokeo ya Kidato cha Nne 2012
litachukua muda mfupi na matokeo yatatangazwa hivi karibuni.
Selestine Gesimba
KAIMU KATIBU MKUU
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI
10/05/2013
Comments