- Get link
- Other Apps
CHAMA KIPYA CHA 21 CHA SIASA NCHINI TANZANIA CHAPATA USAJILI WA KUDUMU LEO KINAITWA CHAUMMA
Baadhi ya wanachama cha CHAUMMA pamoja na viongozi wao wakishangilia baada ya kupewa usajili.
Na Thehabari.com
MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa amekipa usajili wa kudumu
Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA) huku akivitaka vyama vya siasa
kufuata sheria na kuepuka kuwa vyanzo vya vurugu na uchochezi wa
migogoro.
Tendwa ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akiwakabidhi
cheti cha usajili wa kudumu viongozi wa chama kimpya cha kinachojulikana
kama Chama cha Ukombozi wa Umma.
Alivitaka vyama vya siasa kuhakikisha vinatimiza malengo yao ya kushika
dola na hata kama itashindikana kwao, basi kuhakikisha wanapata nafasi
za uwakilishi wa wananchi zikiwemo za udiwani, ubunge pamoja na uongozi
wa serikali za mitaa kwa mujibu wa taratibu za nafasi hizo.
Alisema kwa sasa vipo vyama vya siasa ambavyo licha ya kuwa na usajili
wa kudumu na uongozi mzuri usio na migogoro vimeshindwa kutimiza malengo
ya msingi ya chama kwa kushika nafasi za uwakilishi maeneo anuai kwa
mujibu wa utaratibu.
“…Vyama hivi unakuta hawana mbunge, hawana diwani, hawana viongozi
serikali za mitaa, kijiji na kwingineko lakini ukiangalia wana viongozi
wazuri hawana migogoro ndani ya chama, haya sio madhumuni ya chama cha
siasa,” alisema Tendwa.
Aidha aliwataka viongozi wa CHAUMMA kuhakikisha wanajipanga vizuri ili
waweze kutimiza malengo ya chama na kuwawakilisha wananchi maeneo
mbalimbali ya uongozi kisiasa. Alisema katika mapendekezo mapya ofisi
yake inafikiria kuanza kuvipunguza vyama ambavyo licha ya kuwa na
usajili havifanyi chochote kama ilivyo kwa madhumuni ya kuanzisha chama.
“Sheria inafanyiwa marekebisho, chama kikikaa ndani ya miaka mitano
hakijafanya chochote tunafikiria kukifuta, kiongozi wa chama akitukana
miezi sita unafungiwa kwa muda…maana hatuwezi kuruhusu matusi, vurungu
na masuala mengine yasiokuwa na msingi ndani ya vyama vya siasa,”
alisema Tendwa.
Hata hivyo amesema katika mapendekezo yao ya mabadiliko ya katiba
wamependekeza mambo mengi ikiwemo sasa kuruhusu vyama kujiunga na
kufanya shughuli za siasa kama ilivyo kwa nchi za Kenya, Afrika Kusini,
Lethoto na nchini Namibia.
Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa cheti cha usajili wa kudumu
Mwenyekiti wa muda wa CHAUMMA, Wallance Mayunga alisema wamejipanga
vizuri katika kuwatumikia wananchi na chama chake kinatambua changamoto
zilizopo nchini katika uongozi, utendaji na utawala hivyo kina nia ya
kuleta mabadiliko.
Nafasi ya Katibu Mkuu wa muda wa CHAUMMA inashikiliwa na Shaffii Abed
huku Hamad Tao akiwa ni miongoni mwa wanachama waanzilishi wa nchama
hicho.
Comments