Macho ya dunia kwa Nelson Mandela
Maisha ya Rais wa zamani wa Afrika Kusini yamebaki kuwa kama mshumaa unaokaribia kuzimika kutokana na upepo mkali. Macho na masikio ya dunia yameelekezwa kwake kutokana na ugonjwa wa mapafu unaomsumbua.
Hivi sasa amelazwa katika hospitali isiyofahamika mjini Pretoria kutokana na tatizo hilo.
“Mzee Mandela yuko hospitalini na hali yake bado haijabadilika,” amekaririwa mmoja wa wanafamilia.
Maombi yamekuwa yakifanywa makanisani kote nchini Afrika Kusini kumwombea Mandela ambaye anatibiwa kwa ugonjwa wa mapafu.
Mandela, mwenye umri wa miaka 94, alipelekwa hospitalini Jumamosi , ikiwa ni mara ya tatu kulazwa hospitalini mwaka huu.
Inaelezwa kuwa Mandela amekuwa akiugua kwa muda mjini Johannesburg, baada ya kukumbwa tena na ugonjwa wa mapafu.
Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini, amerejea wito wake kwa watu wa Afrika Kusini kumuombea Mandela, maarufu kama Madiba.
Hata hivyo inaelezwa kuwepo kwa wasiwasi wa hali
yake. Wengi walipata matumani baada ya bintiye Mandela Zindzi, kusema
kuwa babake yuko salama na anaendelea kupata nafuu.
Mkewe Mandela, Graca Machel, alifutilia mbali, ziara yake mjini London Jumamosi ili kuwa karibu na mumewe.
Maisha ya Mandela
Nelson Rolihlahla Mandela ni mwanasiasa mkongwe na
mwanaharakati aliyepambana na sera za ubaguzi za makaburu wa Afrika
Kusini na hatimaye kuwa Rais wa kwanza Mwafrika nchini humo. Ni mshindi
wa Tuzo ya Amani ya Nobel. Mbali na tuzo hiyo, ameshatunukiwa zaidi ya
tuzo 250 katika miongo minne iliyopita.
Alizaliwa Julai 18 mwaka 1918. Ni rais wa kwanza
aliyechaguliwa kidemokrasia nchini Afrika Kusini. Alikuwa mwanasheria na
mwanachama wa Chama cha African National Congress (ANC) aliyepinga
siasa ya ubaguzi nchini Afrika Kusini.
Comments