Kikosi cha kwanza cha Taifa Stars kilichoshuka dimbani juzi
Thomas Ulimwengu akichuana na beki wa Morocco.
--
Taifa Stars imepoteza mechi ya
ugenini baada ya kufungwa mabao 2-1. Mechi hiyo ya kundi C ya mchujo
kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia mwakani nchini
Brazil dhidi ya Morocco imechezwa usiku wa kumakia jana kwenye uga wa
Grand Stade de Marrakech, jijini Marrakech.
Licha ya kufungwa, Stars ndiyo
iliyokuwa ya kwanza kumjaribu kipa wa Morocco, Nadir Lamyaghri aliyeokoa
shuti la mpira wa adhabu la Aggrey Morris katika sekunde ya 40 tu tangu
refa Daniel Frazier Bennett kutoka Afrika Kusini apulize filimbi ya
kuanzisha pambano hilo.
Refa alitoa faulo hiyo baada ya
mshambuliaji Thomas Ulimwengu kukwatuliwa na Ahmed Kantari baada ya
kumtambuka beki mwingine wa Simba hao wa milima ya Atlas.
Stars walicheza pungufu kwa dakika 58
baada ya Morris kutolewa nje kwa kadi nyekundu kwa kumkwatua ndani ya
eneo la hatari Abdelaziz Barrada huku akiwa amebaki yeye na mshambuliaji
huyo. Adhabu hiyo iliandamana na penati ambayo Morocco waliitumia
kupata bao la kuongoza dakika ya 37 mfungaji akiwa Abderazzak Hamed
Allah.
Kabla, Stars wanaodhaminiwa na
Kilimanjaro Premium Lager walitengeneza nafasi nzuri ya kufunga dakika
ya 25 baada ya Ulimwengu kufanikiwa kuwatoka mabeki wawili wa Morocco na
kuingia eneo la hatari lakini shuti lake hafifu lilidakwa na kipa
Lamyaghri.
Morocco waliongeza bao lingine dakika
ya 50 na Youssef El Arabi baada ya mabeki wa Stars kujichanganya katika
kudhibiti pasi ya mwisho ya wachezaji wa timu hiyo, na mshambuliaji
huyo kumfunga kirahisi kipa Juma Kaseja.
Kiungo mshambuliaji Amri Kiemba
aliifungia Stars bao maridadi dakika ya 61 kwa mkwaju wa mbali
uliomshinda kipa Lamyaghri. Kabla ya kuachia shuti hilo, Kiemba
aliwatoka wachezaji wa timu ya Morocco ambayo ndiyo imepeta ushindi wake
wa kwanza katika mechi hizo za mchujo za Kombe la Dunia.
Dakika sita kabla ya filimbi ya
mwisho Mbwana Samata angeweza kuisawazishia Stars, lakini licha ya
kuwatoka mabeki wawili wa Morocco baada ya kupokea pasi ya John Bocco
mpira aliopiga ulitoka nje.
Stars ambayo bado inashika nafasi ya
pili katika kundi hilo ikiwa na pointi sita inaondoka hapa kesho (Juni 9
mwaka huu) mchana kwa ndege ya EgyptAir kupitia Cairo, Misri na
itawasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 11
alifajiri (Juni 10 mwaka huu).
Mechi ilishuhudiwa na watanzania takriban 500 waliotoka Dar, waishio
Morocco na nchi jirani wakiongozwa na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni
na Michezo, Amos Makala.
Kamati ya Ushindi ya Taifa Stars pia iliwakilishwa na wajumbe kadhaa akiwemo Kaimu Mwenyekiti Ramadhan Dau, Mohamed Dewji na Zitto Kabwe.
Katika mechi hiyo Stars iliwakilishwa
na; Juma Kaseja, Erasto Nyoni, Shomari Kapombe, Aggrey Morris, Kelvin
Yondani, Frank Domayo, Mrisho Ngasa/Nadir Haroub, Salum Abubakar, Thomas
Ulimwengu/Khamis Mcha/John Bocco, Amri Kiemba na Mbwana Samata.
Taifa Stars inatarajiwa kurejea nyumbani leo Jumatatu saa kumi na moja na nusu alfajiri kwa ndege ya Shirika la Egypt Air.
Comments