Mtuhumiwa wa Kesi ya Kuiba na Kughushi Benki
akiondoka Mahakamani
**********************
MTU mmoja aliyefahamika kwa jina la Deogratius Mpembe
amehukumiwa kutumikia kifungo cha Miaka 20 Jela kwa kosa la kughushi nyaraka za
kutolea fedha katika Benki ya CRDB Tawi la Mwanjelwa Jijini
Mbeya.
Hukumu hiyo imetolewa jana na Hakimu wa Mahakama ya
Wilaya ya Mbeya Gilbert Ndeuruo, baada ya kumtia hatiani Mshtakiwa kwa makosa 14
ambayo Mtuhumiwa alikubali kutenda baadhi ya makosa na mengine
kuyakanusha.
Mwendesha mashtaka wa Serikali Lugano Mwakilasa
aliiambia mahakama hiyo kuwa Mshtakiwa alitenda makosa hayo katika vipindi
tofauti kati ya Mwezi Juni, 2011 kinyume cha kifungu cha 235 Sura ya 20 ya Mwaka
2002 ya kanuni ya adhabu.
Mwakilasa alisema Mtuhumiwa alipatikana na Kosa la
kughushi nyaraka za kutolea fedha katika Benki ya CRDB katika akaunti mbili za
mteja wa benki hiyo ambaye ni marehemu Clemence Kihanga ambaye imedaiwa
mahakamani hapo kuwa na uhusiano na Mshtakiwa.
Mbali na kosa hilo Mtuhumiwa huyo pia anadaiwa
kuiibia Benki hiyo fedha za kigeni Dolla za Marekani 118,137.4 pamoja na fedha
za kitanzania Shilingi Milion 2,468,181.24 ambapo Mtuhumiwa huyo alitenda kosa
hilo akiwa ni karani wa Benki hiyo akiwa na kitambulisho cha kazi chenye namba
CK 4M.
Upande wa Mashtaka ulikuwa na mashahidi wanne ambao ni
Meneja wa benki hiyo tawi la Mwanjelwa Ephraim Luwila, Mtaalamu wa maandishi
kutoka Jeshi la Polisi namba E2912 Johanes, Mke wa Marehemu Niku Kihanga na
Kaimu Meneja wa Benki hiyo Alfred Basajile.
Katika maelezo yao Mashahidi hao walitoa Vielelezo
mbali mbali mahakamani hapo kama sehemu ya ushahidi ikiwemo Kitambulisho cha
kazi cha Mtuhumiwa, Hati ya Kifo cha marehemu aliyefariki Novemba 2010 na
Nyaraka za maandishi ambazo zote zilikuwa na miandiko inayofanana na Mtuhumiwa
kama vile Mkato na Sahihi zake.
Awali ilielezwa kuwa kugundulika kwa wizi wa fedha
hizo ni baada ya Mke wa Marehemu Niku Kihanga kufuatilia masalio ya akiba ya
Mume wake baada ya kuidhinishwa kuwa msimamizi wa mirathi na kuomba kupewa
masalio ya akiba zote na kukuta kuna upungufu wa Dola 5000 kwa akaunti ya fedha
za nje na akaunti ya ndani ikikutwa na Shilingi 36,000/= badala ya Shilingi
2,400,000/=.
Mke wa marehemu alisema kufuatia kuwepo kwa upungufu
mkubwa wa fedha hizo aliamua kupeleka malalamiko kwa Meneja wa benki hiyo ambaye
alianza kulifanyia kazi kwa kupeleka malalamiko
Polisi.
Kutokana na Ushahidi huo pamoja na maelezo ya kukiri
Polisi, Hakimu Gilbert Ndeuruo alimtia hatiani Mtuhumiwa kwa makosa yote 14 na
kumhukumu kila kosa kwa miaka Mitano ambapo alisema Mtuhumiwa atatumikia makosa
yote kwa pamoja kwa kwenda Jela Miaka 20.
Aidha kabla ya kutoa hukumu hiyo Mwendesha mashtaka
Lugano Mwakilasa aliiomba Mahakama hiyo kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa
watumishi wengine wasiokuwa waaminifu.
Hata hivyo Hakimu huyo kabla ya kutoa hukumu alimtaka
Mtuhumiwa huyo kujitetea ili apunguziwe adhabu ya kifungo cha maisha kutokana na
makosa aliyokutwa nayo, ambapo Mtuhumiwa huyo aliiomba mahakama kumpunguzia
adhabu kwa kile alichodai anasumbuliwa na ugonjwa wa Kansa, Mtoto mmoja, Mkewe
na Mdogo wake ambaye anamsomesha kuwa wanategemea msaada
wake.
Pamoja na utetezi huo ambao Hakimu aliridhika nao na
kumpunguzia adhabu kutoka Kifungo cha Maisha hadi kumfunga kutumikia Jela kwa
Miaka 20 na kuongeza kuwa anaruhusiwa kukata rufaa endapo hatakuwa ameridhika na
adhabu aliyopewa ndani ya Siku 30.
PICHA , HABARI NA MBEYA YETU BLOG
Comments