CAF YABADILI MWAMUZI MECHI YA STARS
Shirikisho
la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limefanya mabadiliko ya mwamuzi wa mechi
ya mchujo kusaka tiketi ya Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ligi ya
Ndani (CHAN) kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes)
itakayochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mwamuzi
aliyeondolewa kutokana na sababu za kiufundi ni Jean Claude Birumushahu
aliyekuwa mwamuzi msaidizi namba moja. Nafasi yake sasa inachukuliwa na
Herve Kakunze pia kutoka Burundi.
CAF
imemuondoa mwamuzi huyo baada ya kufeli katika mtihani wa waamuzi
(Cooper Test) kwa waamuzi wa Burundi wanaotambuliwa na Shirikisho la
Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) uliofanyika nchini humo siku tatu
zilizopita.
Waamuzi hao na Kamishna wa mechi hiyo
Gebreyesus Tesfaye kutoka Eritrea wanatarajiwa kuwasili nchini kesho
(Julai 11 mwaka huu) kwa ndege za Kenya Airways na EgyptAir kwa muda
tofauti.
Nayo Uganda Cranes inatarajiwa kuwasili
nchini kesho (Julai 11 mwaka huu) na itafikia hoteli ya Sapphire.
Shirikisho la Mpira wa Miguu Uganda (FUFA) bado halijatuma taarifa rasmi
juu ya ujio wa timu hiyo.
Wakati huo huo, makocha wa Taifa Stars,
Kim Poulsen na wa Uganda, Milutin Micho pamoja na manahodha wao watakuwa
na mkutano na Waandishi wa Habari utakaofanyika keshokutwa (Julai 12
mwaka huu) saa 5 asubuhi kwenye ofisi za TFF kuzungumzia mechi ya
Jumamosi.
FRIENDS, POLISI KUCHEZA MECHI YA RCL JUMAPILI
Mechi ya marudiano ya Ligi ya Mabingwa wa
Mikoa (RCL) kati ya Friends Rangers ya Dar es Salaam na Polisi Jamii ya
Mara iliyokuwa ichezwe Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) imesogezwa mbele
kwa siku moja.
Timu hizo sasa zitacheza Jumapili (Julai
14 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi. Polisi Jamii
ilishinda bao 1-0 mechi ya kwanza iliyochezwa Julai 6 mwaka huu Uwanja
wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.
Refa Hans Mabena kutoka Tanga ndiye
atakayechezesha mechi akisaidiwa na E. Mkumbukwa na Hajj Mwalukuta wote
kutoka Tanga. Mwamuzi wa akiba (fourth official) ni Kessy Ngao wa Dar es
Salaam.
Mechi kati ya Stand United FC ya
Shinyanga na Kimondo SC ya Mbeya itachezwa Jumamosi (Julai 13 mwaka huu)
kwenye Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga. Mwamuzi atakuwa Daniel
Warioba kutoka Mwanza. Kimondo SC ilishinda mechi ya kwanza bao 1-0.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Comments