NDEGE YA MADAKTARI YAPATA AJALI ARUSHA, SITA WANUSURIKA KIFO
NA LILIAN JOEL, ARUSHA
Watu
sita wamenusurika kifo baada ya ndege ndogo ya madaktari maalum (Flying
doctors), wanaotoa huduma katika vijiji vya jamii ya wafugaji wa
Kimaasai imeanguka leo katika eneo la kijiji cha Kipenjiro, wilayani
Ngorongoro.
Habari
zilizopatikana kutoka Ngorongoro na kuthibitishwa na Mbunge wa
Ngorongoro, Saning’o Telele zimeeleza kuwa ndege hiyo iliyokuwa na
abiria saba ilianguka kati ya Saa 9:00 na 10:00 alasiri.
“Ni
kweli ndege ndogo ya Flying doctors wa Kanisa Katoliki inayotoa huduma
za kitabibu katika vijiji kadhaa wilayani Ngorongoro imeanguka leo ila
ni bahati nzuri hakuna taarifa ya vifo hadi hivi sasa,”alisema Mbunge
Telele kwa njia ya simu.
Mbunge huyo alitaja baadhi ya vijiji ambavyo madaktari hao hutoa huduma kuwa ni Naiyobi, Ngarasero, Olitatiro na Endulen.
Kwa
mujibu wa Telele, majeruhi wote waliokuwepo ndani ya ndege hiyo
walikimbizwa hospitali ya Seliani Jijini Arusha kwa matibabu baada ya
shirika linalomiliki ndege hiyo kutuma ndege nyingine kuwachukua kutoka
eneo la ajali.
Taarifa
zilizopatikana kutoka hospitali ya Endulen inayomilikiwa na Kanisa
Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha zinasema ndege hiyo ilikuwa na daktari
mmoja na wauguzi wawili kutoka hospitali hiyo ambao majina yao
hayakupatikana mara moja.
Pamoja na daktari na wauguzi, ndege hiyo pia ilikuwa na marubani wawili na wagonjwa wawili ambao ni mama na mtoto wake.
Vijiji
ambavyo Flying doctors hufika kutoa huduma kwa ndege hiyo ni vile
visivyokuwa na huduma ya kitatbibu na hazifikiki kirahisi kwa njia ya
barabara.
Kamanda
wa polisi mkoa wa Arusha, Lebaratus Sabas alithibitisha kutokea kwa
ajali hiyo lakini hakuwa tayari kuizungumzia kwa undani kwa maelezo kuwa
hajapokea taarifa rasmi za kutosha kutoka kwa maafisa wake walioko
wilayani Ngorongoro kutokana na mazingira halisi ya jiografia ya wilaya
hiyo kimawasiliano.
Comments