Jaji mkuu wa mahakama ya
kikatiba nchini Misri Adli Mansour anatarajiwa kuapishwa kama rais wa
mpito wa nchi hiyo baada ya jeshi kumng'oa madarakani rais Mohammed
Morsi, ambaye ni kiongozi wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia nchini
humo.
Mkuu wa jeshi Generali Abdul Fattah al-Sisi
alitoa tangaza hilo kupitia televisheini Jumatano jioni, katika kile
Morsi, alisema ni mapinduzi ya kijeshi.Hatua hiyo inakuja baada ya siku nyingi ya maandamano, dhidi ya rais Morsi wa chama cha Musolim Brotherhood.
Waandamanaji walimtuhumu yeye na chama chake kwa kusukuma ajenda ya kiisilamu kwa taifa hilo na kukosa kusuluhisha matatizo ya kiuchumi yanayokumba taifa hilo.
Chama cha Muslim Brotherhood kimesema kuwa bwana Morsi pamoja na washauri wake wako chini ya kifungo cha nyumbani na hawana mawasiliano ya nje.
Hapo awali mkuu wa majeshi alisema kuwa katiba ya nchi hiyo imeahirishwa na kwamba jaji mkuu wa taifa hilo atachukuwa mamlaka ya rais.
Maelfu ya waandamanaji wanaompinga bwana Morsi mjini Cairo walisherehekea kwa shangwe na vifijo kufuatia taarifa hiyo ya jeshi lakini wale wanaomuunga bwana Morsi wanasemekana kubaki kimya huku wakisubiri matukio yatakayofwata.
Rais Obama amesema kuwa ana wasiwasi mkubwa kuhusiana na matukio yaliyopo nchini Misri huku katibu mkuu wa umoja wa mataifa Banki Moon akitaka kuwe na utulivu.
Comments