Na Willy Sumia, Katavi
KATIKA
hali isiyo ya kawaida basi la kampuni ya Sumry limetumbukia mtoni na
kuuwa watu tisa na kujeruhi abiria wapatao hamsini na tatu katika mto
Iku uliopo katika kijiji cha Sitalike wilaya ya Mlele mkoani Katavi.
Tukio hilo la
kusikitisha lilitokea saa sita usiku kuamkia Julai 5, 2013 basi hilo
lilipokuwa likitokea mjini Sumbawanga kuelekea Mpanda mkoani Katavi
likiwa na abiri waliokuwa wametoka Mbeya.
Kaimu
Kamanda wa Polisi mkoani Katavi Emanuely Nnley alisema jana kuwa ajali
hiyo ilihusisha basi aina ya Nissan Diesel lenye namba T909 AZT mali ya
kampuni ya Sumry lililokuwa likiendesha na dereva aliyetajwa kwa jina na
Stephano Chimane maarufu kwa jina la Ntungu.
Alisema basi hilo
lilipofika katika daraja hilo lenye kona kali na mteremko dereva wake
alishindwa kulimudu na kulenga daraja hali iliyosababisha tairi za nyuma
kupanda juu ya ukingo na kudumbukia mtoni ambapo dereva wa basi hilo
aliweza kutoka na kukimbilia kusikojulikana.
Alifafanua kuwa juhudi
za uokoaji zilianza kufanyika usiku huo huo ambapo majeruhi 53
waliokolewa na maiti tisa za wanaume watatu na wanawake watano na motto
mmoja wa kike ziliopolewa katika maji.
Alisema hali ya
majeruhi inaendelea vizuri isipokuwa majeruhi watatu walikimbizwa katika
hospitali ya mkoa wa Rukwa kwa matibabu zaidi na kufafanua kuwa chanzo
cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva kushindwa kuliongoza gari, ubovu wa
gari na wembamba wa daraja
Akizungumza na gazeti
hili Afisa Mwandamizi wa SUMATRA mikoa ya Rukwa na Katavi, David Chiragi
alisema basi hilo lilikuwa limeiba njia kwani leseni yake inaliruhusu
basi hilo kufanya safari za Sumbawanga Kirando na siyo Sumbawanga Mpanda
kwa mujibu wa leseni iliyotolewa mwezi Juni mwaka huu.
Alisema hata upana wa
daraja ilipotkea ajali hiyo ni mdogo sana ambapo vipimo vinaonesha
daraja hilo lina upana wa mita 3.5 (tatu na nusu) tu wakati basi lina
upana wa mita nne na nusu hivyo kujenga mazingira ya ugumu wa dereva
kulenga daraja inapotokea msukosuko wa aina yoyote hasa wakati wa usiku
na hivyo kuwataka wakala wa barabara mkoani Katavi kuangalia namna ya
kupanua daraja hilo na kuboresha eneo hilo.
Alisema katika kipindi
cha Januari hadi July 2013 zaidi ya ajali tisa zimetokea katika daraja
hilo zikihusisha magari makubwa saba na madogo mawili kutokana na
madereva kushindwa kumudu magari yao na kulenga daraja hilo.
Alisema pia basi hilo
lina makosa ya kutembea nje ya ratiba, kuiba njia na kuzidisha abiria
hivyo ofisi yake imechukua hatua ya kuvunja safari za mabasi ya kampuni
ya Sumry za mchana na badala yake mabasi yote yataondoka Sumbawanga na
Mpanda majira ya asubuhi pekee.
Baadhi ya majeruhi wa
ajali hiyo wakiongea kwa tabu katika hospitali ya wilaya ya Mpanda jana
walisema kuwa dereva wa basi hilo alikuwa akiendesha kwa mwendo wa
taratibu sana tangu mwanzo wa safari hali iliyowapa shaka kuwa huenda
alikuwa hajui kueondesha magari au basi hilo lilikuwa na hitilafu kwani
waliondoka mjini sumbawanga majira ya saa kumi na moja jioni na kufika
eneo hilo saa saba na nusu usiku tofauti na mwendo wa kawaida ambapo
walitakiwa kufika saa nne usiku eneo hilo.
Kondakta wa basi
lililopata ajali alisema kuwa dereva huyo alikuwa mgeni wa njia pia
alikuwa hajazoea kuendesha mabasi aina ya Nissan Diesel hali
iliyomlazimu kumuelekeza njia wakati wote wa safari lakini ilipofika
eneo la mteremko wa mto Sitalike Iku alimueleza kuwa mbele kuna daraja
jembamba na kona kali dereva huyo alibadili gia ikagoma na kuanza
kuporomoka hadi mtoni.
Mkuu wa mkoa wa Katavi
Dr Rajabu Rutengwe alitoa rambi rambi kwa wafiwa wote na kuwapa pole
wahanga wa ajali hiyo mbaya kutokea tangu mkoa huo uanze.
Comments