HIZI NDIO DALILI ZA VVU KWA WATOTO WADOGO


Maambukizi haya kwa mtoto huweza kuambatana na magonjwa nyemelezi hatari kama vile nimonia kali, kifua kikuu, homa za
mara kwa mara, kuharisha sugu, fangasi, na pia saratani mbalimbali.




Desemba Mosi kila mwaka,  Nchi mbalimbali duniani ikiwemo
Tanzania ilijumuika na dunia nzima kufanya kumbukumbu ya Siku ya Ukimwi. Hiyo siku maalum iliyotengwa na Umoja wa Mataifa (UN) kwa ajili ya kuwakumbuka wale wote waliokufa kwa ugonjwa huo hatari wa kuambukiza.

Shirika la Afya Duniani (WHO) na wadau wengine wa afya sehemu mbalimbali duniani waliadhimisha siku hiyo kwa uhamasishaji , kaulimbiu pamoja na hamasa kama ya kupima kwa hiari, ushauri nasaha, namna ya kuzuia maambukizi mapya, namna ya kuishi na virusi vya Ukimwi.

Pia elimu kwa mjamzito anavyoweza kupata huduma na kuweza
kumkinga mtoto asipate maambukizi ya VVU.

Makala hii itaongelea namna ya kutambua dalili za mtoto mwenye
VVU. Kwa kawaida kwa mtu mzima mwenye VVU, dalili huweza kujitokeza baada ya miaka 10 na huweza kuishi kwa mda mrefu bila dalili zozote, kwa mtoto huwa ni tofauti kwani dalili hujitokeza haraka sana huchukua mda wa mwaka 1 mpaka miaka mi 3.

Dalili hujitokeza au pengine hata mtoto akazaliwa na kufariki pia kuumwa ndani ya mwaka mmoja kunaweza kujitokeza, na
mtoto anaweza kupoteza maisha haraka kama hatua madhubuti za matibabu hazitachukuliwa.

Maambukizi haya kwa mtoto huweza kuambatana na magonjwa nyemelezi hatari kama vile nimonia kali, kifua kikuu, homa za
mara kwa mara, kuharisha sugu, fangasi, na pia saratani mbalimbali. Magonjwa haya huweza kusababisha mtoto asiwe na ukuaji mzuri, uzito kutoongezeka na utapiamlo.

Mambo haya ndiyo yanayosababisha mtoto kufariki mapema kwa kuwa uwepo wa magonjwa nyemelezi ni uthibitisho kuwa kinga yake na mwili haiko imara kustahimili mashambulizi ya magonjwa haya. Na mtoto anakuwa na kinga dhaifu ambayo haijawa imara.

Dalili za VVU kwa watoto Mara nyingi watoto hawa hujulikana au
hudhaniwa kuwa na VVU kwa sababu ya mama zao hugundulika kuwa na VVU, na mara nyngi ni mpaka pale dalili zianze kujitokeza.

Dalili zipo nyingi, ila nitagusia zile dalili za mwazoni zinazojitokeza mara kwa mara.

Ukuaji kuwa chini pamoja na kutoongezeka uzito au urefu kufuatana na viwango maalum vilivyowekwa na wataalam wa afya,
kupata maambukizi ya koo, maambukizi ya mfumo wa upumuaji mara kwa mara kama vile kikohozi mafua, kuvimba tezi za mwilini
maeneo ya shingoni na makwapani, mwili kudhoofu na kukonda, utapiamlo, homa za mara kwa mara, kuharisha, vipele mwilini.


Dalili zingine zinazojitokeza baada ya ugonjwa kupiga hatua za mbeleni ni kama vile fangasi za mdomoni na kooni, kikohozi
cha zaidi ya wiki 2, uzito kupungua sana, nimonia kali, kuharisha kusikokoma zaidi ya mwezi mmoja, uti wa mgongo na ubongo kuathirika, kupata degedege lisiloisha, kutokwa na upele na ngozi kuwa kavu, kushindwa kunyonya au kula vizuri, kulia na kutokua mtulivu kwa mda mrefu, upungufu wa damu usio na sababu maalum, saratani za ngozi, satarani au uvimbe sehemu mbalimbali mwilini.

Upimaji wa VVU kwa mtoto Mara nyingi wazazi au walezi huwa
wagumu kupima na huwa wanaogopa kwenda katika huduma za upimaji na wakija kufanya maamuzi tayari mtoto huletwa katika huduma za afya akiwa na hali mbaya na amedhoofu kimwili.
Hakika Ukimwi ni ugonjwa hatari. Na inahuzunisha zaidi pale
unapomwona mtoto mdogo akiwa na maambukizi haya na akiteseka. Kwa kifupi watoto wadogo wanaweza kuambukizwa Ukimwi kwa njia nyingi kama tulivyoona katika makala zilizopita.


Ugunduzi wa mapema wa VVU ni muhimu sana katika mapambano dhidi ya VVU kwa mtoto aliyezaliwa, kwani pale
inapogundulika kuwa na maambukizi hatua za haraka huweza kuchukuliwa ili kupata ushauri maalumu, matibabu ya kumkinga na magonjwa nyemelezi na kuanza kutumia dawa za kufubaza virusi-ARV.


Imejengeka tabia baadhi ya wazazi huamua wenyewe kwenda kununua vipimo vya kujipima VVU ambavyo hutoa majibu ya haraka kitaalamu huitwa Rapid Diagnostic Test. Hawa, huamua kujipima wenyewe na mtoto ambaye amezaliwa pia huweza kwenda kupima vipimo hivyo katika baadhi ya vituo
visivyotambulika au visivyo na ufahamu juu ya upimaji wa VVU.
Labda hufanya hivyo ni kwa kuogopa kutengwa na kunyanyapaliwa na jamii. fahamike upimaji wa mtaani huwa
na matokeo yasiyo sahihi na hautaweza kupata huduma stahiki.

Upimaji wa VVU una utaratibu wake wenye mtiririko unaofuata
miongozo ya Shirika la Afya Duniani(WHO) na hapa nchini
kwetu tunaifuata chini ya usimamizi wa Wizara ya Afya.


Kama nilivyoeleza awali kuwa upimaji au huduma kwa watu
wenye VVU zipo katika vituo vya afya vya serikali, hospitali za rufaa, hospitali kubwa binafsi, baadhi ya vituo vya afya mashirika ya kimataifa na hospitali za misheni. Pia wapo wataalamu mbalimbali wenye ujuzi wa ziada wa mambo ya Ukimwi hawa wamepewa mafunzo maalumu kama vile washauri nasaha, upimaji, huduma za matibabu ya VVU, uhamasishaji.


Mara nyingi dalili za mtoto na historia ya mama kipindi cha ujauzito kama alipimwa wakati wa ujauzito huwa ni jambo la msingi sana katika hatua za ugunduzi wa tatizo.
Kwa mtoto aliyezaliwa akipimwa huonekana ni (HIV-positive) hata kama hana VVU hii ni kwasababu ya uwepo wa askari mwili (antibody) katika mwili wa mtoto ambao walipita katika kondo la nyuma akiwa tumboni kwa mwa mama, na huendelea kuwapo
anapozaliwa mpaka kipindi cha zaidi ya miezi 18 kuendelea.


Pale mjamzito anapokuwa na VVU mfumo wa kinga ya mwili hujibu mapigo kwa kutoa askari mwili maalumu kwa ajili ya kupambana na VVU. Askari mwili hawa wanakuwapo katika mwili wa mama mwenye VVU.

Vipimo vya majibu ya haraka-vya VVU vimetengenezwa kung’amua uwepo wa askari mwili (antibody) hawa, hivyo kama mtoto atapimwa kwa vipimo hivi kabla ya miezi 18 basi majibu huwa ni chanya (positive) hivyo basi majibu yanakuwa sio sahihi (False result). Katika huduma za afya wataalamu wa afya huweza kuthibitisha maambukizi ya VVU, kwa kuongea na mzazi au mlezi na kupata historia ya afya ya mtoto wako,


washauri nasaha wataongea na wewe, baada ya kuelimika na
kupata ushauri, ndipo wataalamu wa afya humchunguza kujua dalili alizonazo, uchunguzi wa kimaabara, na mwishowe majibu
yakitoka huweza kuainishwa ni kuwekwa katika madaraja ya ugonjwa wa Ukimwi.


Ukimwi umeainishwa katika madaraja manne na uanzishwaji
wa huduma za matibabu kwa mtoto hutegemeana ameainishwa
daraja gani, hivyo usishangae kutoanzishiwa dawa za kufubaza
makali ya virusi-ARV. http://www.manyandahealthy.blogspot.com

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA