Huduma za dharura kwa wazazi Kibiti zaokoa maisha ya mama na mtoto
Mratibu
wa Mtandao wa Utepe Mweupe Kitaifa (The White Ribbon Alliance), Rose
Mlay akimjulia hali mmoja wa akinamama aliyejifungua katika wodi ya
wazazi katika Kituo cha Afya Kibiti leo.
Mratibu wa Mtandao wa Utepe Mweupe Kitaifa (The White Ribbon Alliance),
Rose Mlay akitambulishwa kwa baadhi ya wahudumu katika wodi ya wazazi
kwenye Kituo cha Afya Kibiti leo alipotembelea kuangalia mwenendo wa
utoaji huduma za dharura katika kituo hicho. Jengo ambalo ni chumba cha upasuaji linalotoa huduma za dharura kwa wajawazito katika Kituo cha Afya Kibiti
Mmoja
wa akinamama aliyepatiwa huduma za uzazi katika Kituo cha Afya Kibiti
kinachotoa huduma za dharura kwa akinamama wajawazito akizungumzia
msaada wa huduma hiyo kwa wajawazito
Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kibiti, Chagi Jonas Lymo akizungumza
na mwandishi wa habari wa Kituo cha ITV alipotembelea kituo hicho pamoja
na Mtandao wa Utepe Mweupe Kitaifa (The White Ribbon Alliance). Baadhi ya akinamama wakipatiwa huduma katika kituo cha afya Kibiti leo.
Mratibu wa Mtandao wa Utepe Mweupe Kitaifa (The White Ribbon Alliance),
Rose Mlay (kulia) akizungumza na Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya
Kibiti, Chagi Jonas Lymo katika kituo hicho leo Kibiti.
MGANGA
Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kibiti, Chagi Jonas Lymo amesema uwepo wa
huduma za dharura kwa wajawazito katika kituo hicho cha afya umesaidia
kiasi kikubwa katika uokoaji wa maisha ya mamamjamzito pamoja na vifo
vya watoto eneo hilo.
Lymo
ametoa kauli hiyo leo mjini Kibiti alipokuwa akizungumza na Mratibu wa
Mtandao wa Utepe Mweupe Kitaifa (The White Ribbon Alliance), Rose Mlay
pamoja na Mkurugenzi wa World Lung Foundation walipotembelea kituo hicho
kuangalia namna kinavyotoa huduma kwa wananchi na changamoto zake.
Akizungumza
zaidi, Lymo alisema tangu Kituo cha Afya cha Kibiti kuanza kutoa huduma
za dharura kimekuwa msaada mkubwa kwa akinamama wajawazito eneo hilo na
kwa sasa idadi ya akinamama wanaojifungulia eneo hilo imeongezeka mara
tatu zaidi tofauti na ilivyo kuwa awali jambo ambalo unaonesha
wamevutiwa na huduma hiyo muhimu kwa wajawazito.
Alisema
kwa sasa kituo hicho kinafanya upasuaji kwa matatizo yote ya uzazi kwa
wajawazito, ikiwemo kutoa huduma za kuongezewa damu kwa wajawazito wenye
mahitaji jambo ambalo limesaidia kwa kiasi kikubwa kuokoa maisha ya
mama mjamzito pamoja na mtoto mtarajiwa.
"...Awali
tulikuwa hatutoi huduma za upasuaji kwa akinamama wajawazito...tulikuwa
hatuna chumba cha upasuaji hivyo tulitoa huduma za uzazi za kawaida, na
ilipotokea matatizo kwa mjamzito tulimshauri kwenda ama kwenye
hospitali ya Mchukwi (ya kulipia) ambayo ipo umbali wa takribani
kilometa 15 au kwenda kwenye Hospitali ya Wilaya Utete ambayo ni
kilometa 84 kutoka hapa," alisema.
"...Baada
ya kuanzisha huduma za upasuaji kwa akinamama wajawazito, akinamama
waliokuja kujifungulia hapa waliongezeka..., mwezi wa kwanza tu wa
kuanza kutoa huduma hizi wakinamama waliongezeka kutoka idadi ya
wagonjwa 35 kwa mwezi waliongezeka hadi kufikia zaidi ya akinamama 100
kwa mwezi," alisema Lymo.
Alisema
kwa mwezi uliopita (Machi) jumla ya wajawazito 135 walifika kupata
huduma za uzazi kiasi ambacho kwa sasa ni kikubwa na kinazidi uwezo wa
kituo, jambo ambalo alishauri ipo haja ya kituo hicho kuongezewa
mahitaji anuai ili kwenda sambamba na ongezeko la wateja wake kwa sasa.
Kwa
upande wake Mratibu wa Mtandao wa Utepe Mweupe nchini, Bi. Rose Mlay
alisema serikali ikiamua kwa kushirikiana na wadau wengine inaweza
kumaliza matatizo ya vifo kwa wajawazito pamoja na watoto kwa kusogeza
huduma za dharura katika vituo vya afya ambavyo vingi vipo karibu na
wananchi.
"...Inawezekana
kabisa kupambana na vifo vya akinamama wajawazito pamoja na watoto
endapo Serikali ikijipanga na kuamua vituo vya afya viwekewe bajeti ya
kutosha na hatimaye kuweza kutoa huduma za dharura kwa akinamama
wajawazito na watoto," alisema Bi. Mlay.
World
Lung Foundation ndiyo taasisi iliyokiwezesha kituo cha Afya cha Kibiti
kuweza kutoa huduma za dharura kwa akinamama wajawazito. Akizungumzia
hatua hiyo, Mkurugenzi wa World Lung Foundation, Dk. Nguke Mwakatundu
alisema taasisi hiyo imevisaidia jumla ya vituo 10 vya afya kutoa huduma
za dharura pamoja na kuziwezesha hospitali nyingine tano katika nyanja
tofauti kwenye utoaji huduma za afya.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com
Comments