Kundi
maarufu la muziki wa Kwaito la nchini Afrika kusini, Mafikizolo
linatarajia kutua mchana huu jijini Dar es Salaam kwa ajili ya onesho
moja tu linalotarajia kufanyika katika ukumbi wa Mlimani City, kesho,
Jumamosi Aprili 5 mwaka huu.
Mafikizolo
imekuwa na rekodi nzuri ya kushinda kwenye tuzo mbalimbali za muziki,
kutokana na kupiga muziki na kucheza kwa umahiri, hasa mtindo wao
maarufu wa Kwaito.
Kundi
hilo linaloundwa na wasanii wawili(Nhlanhla Nciza na Tebogo Madingoane
pichani juu), kwa sasa linalotamba na vibao kama "Khona" na "Happiness",
watawasili nchini kesho mchana kwa ndege ya Shirika la Ndege la Afrika
Kusini.
Akiongea
na gazeti hili, mratibu wa onyesho hilo Vinny Magere kutoka kampuni ya
Juegacassa, amesema Mafikizollo, wanatarajia kufanya onesho moja tu
maalum na la kihistoria litakalodumu kwa muda wa saa nne.
Hii
itakuwa ni mara ya kwanza kwa kundi hili kufika nchini, tangu kuachia
wimbo wao wa "Khona", wimbo ambao umesababisha kundi hilo kujizolea
umaarufu mkubwa kwenye kumbi za starehe, na hata katika vituo mbali
mbali vya redio.
Mafikizolo
kwa sasa wanashikilia taji la kundi bora la mwaka, kwa mujibu wa tuzo
za muziki za SAMA (South African Music Awards), huku wakiongozwa kwa
kutajwa mara nyingi kwenye tuzo za Ulaya kama kundi bora la muziki kutoka Afrika.
Kundi
hilo maarufu kuliko yote yaliyowahi kutokea kusini mwa Afrika liliwahi
kutamba pia miaka ya nyuma na nyimbo kama "Ndihamba Nawe", "Ndixolele",
"Sebenza", "Ndashata" na "Ndizolila".
Onesho
la hilo, linatarajiwa kuanza saa moja usiku ambapo kiingilio kitakuwa
shilingi 20,000 kwa watakaolipa kabla ya onyesho, huku mlangoni
watalipia shilingi 35,000 za kitanzania.
Kundi hilo mwaka huu, limeingia katika vipengele vinne kwenye kinyanga’anyiro kikubwa cha tuzo za SAMA.
Katika
kinyang’anyiro hicho chenye vipengele 28, kundi hilo limepata nafasi ya
kuwania vipengele vinne, ambavyo ni Kolabo Bora ya Mwaka, albam Bora ya
Pop ya Mwaka, albam ya Mwaka kupitia albam ya Reunited, na kundi bora la Mwaka.
Kwa mujibu wa tovuti ya destinyconnect, hafla ya ugawaji tuzo hizo itafanyika nchini humo Aprili 28 mwaka huu.
Kundi
hili lilianza shughuli za kimuziki tangu miaka ya 1990, albamu yao ya
kwanza walitoa mwaka 1996. Tangu hapo wameshatoa albamu sita, baada ya
kutoa albamu yao ya tano mwaka 2003 "Kwela".
Kundi
lilianza kutetereka na baadaye mwaka 2013 waliungana tena na kutoa
albamu ya sita iliyoitwa "Reunited" na kutoa singo yao ya kwanza "Khona"
wimbo ambao umewatambulisha upya.
Comments