Mkuu
wa mkoa wa Njombe Kapteni mstaafu Aseri Msangi akihutubia mamia ya
wananchi waliofurika viwanja vya mabehewani wilayani Makete mkoani
Njombe katika maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa.(Picha/habari na Edwin
Moshi, Makete)
Licha ya
serikali kuendelea kutatua changamoto lukuki katika sekta ya elimu
nchini, wadau wa elimu mkoani Njombe wametakiwa kuwajibika kila mmoja
kwa nafasi yake, ili kuinua kiwango cha elimu mkoani humo kwa kuwa ni
agizo la serikali hasa katika mkakati wa matokeo makubwa sasa (BRN)
Mkuu wa
mkoa wa Njombe Kapteni Mstaafu Aseri Msangi ameyasema hayo wilayani
Makete mkoani hapa katika maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa na kusema
kwamba ushirikiano wa pamoja kila mtu kwa nafasi yake kutasaidia kuzidi
kuinua kiwango cha elimu kwa mkoa wake
Mh.
Msangi amesema suala la kuongeza kiwango cha ufaulu ni la kila mmoja
hivyo kuagiza maafisa elimu wilaya zote za mkoa huo kupita kwenye kila
shule za sekondari na msingi kubaini changamoto zinazopelekea wanafunzi
kufanya vibaya kwenye mitihani yao, na kuwashirikisha wazazi kwa kufanya
nao kikao na baada ya hapo watagundua changamoto nyingi ambazo wataweza
kuzitatua na zile zilizozidi uwezo wao watazipeleka sehemu husika ili
zitatuliwe
"Nyie
maafisa elimu wa wilaya zote, nawaagiza tembeleeni shule zenu hasa zile
zinazofanya vibaya, mtagundua changamoto nyingi sana, pia muwashirikishe
wazazi kwa kufanya nao kikao na muandike kwenye muhtasari maana mwisho
wa mwezi huu nitaihitaji ili nione kama mmetekeleza, nawahakikishieni
mtagundua mambo mengi sana huko" amesema Msangi
Amesema
kwa sasa wanafunzi 538 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza
mwaka huu bado hawajaripoti hivyo kutoa agizo kuwa wanafunzi hao
watafutwe popote walipo ili waripoti shuleni tayari kwa masomo
Awali
akisoma risala kwa niaba ya wanafunzi wenzake mkoani Njombe, Noela
Msinangila amesema wanaipongeza serikali kwa kuongeza idadi ya waalimu
kila mwaka, kuongeza vitabu, kujenga mabweni pamoja na nyumba za waalimu
huku wakiomba serikali kuendelea kutatua changamoto zinazowakabili
ikiwemo uhaba wa vyumba vya madarasa, kuongeza idadi ya waalimu wa
sayansi na hisabati, pamoja na kuwasaidia wanafunzi yatima na wanaoishi
katika mazingira hatarishi.
Naye
afisa elimu mkoa wa Njombe Bw. Said Nyasiro amesema mkoa wa Njombe
umejipanga vilivyo katika kuinua kiwango cha elimu siku hadi siku
kulingana na mipango iliyowekwa ikiwemo kuhskikisha wanafunzi wanasomea
katika mazingira mazuri
Afisa elimu mkoa wa Njombe Bw. Said Nyasiro akisoma taarifa ya elimu kimkoa.
Bw.
Nyasiro amesema kwa sasa watahakikisha shule zote katika mkoa huo
zitatoa chakula kwa wanafunzi wake kwa kuwa itasaidia wanafunzi hao
kuzingatia masomo ipasavyo wawapo darasani, pamoja na kutoa zawadi kwa
shule 10 za sekondari na msingi zinazofanya vizuri kimkoa kama motisha
katika kuinua elimu
Katika
maadhimisho pamoja na mambo mengine zimetolewa zawadi kwa shule 10 za
sekondari na msingi zilizofanya vizuri pamoja na halmashauri 3
zilizoongoza kielimu
Comments