MAADHIMISHO YA WIKI YA ELIMU MKOA WA NJOMBE YAFANA, MKUU WA MKOA ATILIA MKAZO SUALA LA ELIMU

 Mkuu wa mkoa wa Njombe Kapteni mstaafu Aseri Msangi akihutubia mamia ya wananchi waliofurika viwanja vya mabehewani wilayani Makete mkoani Njombe katika maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa.(Picha/habari na Edwin Moshi, Makete)
Licha ya serikali kuendelea kutatua changamoto lukuki katika sekta ya elimu nchini, wadau wa elimu mkoani Njombe wametakiwa kuwajibika kila mmoja kwa nafasi yake, ili kuinua kiwango cha elimu mkoani humo kwa kuwa ni agizo la serikali hasa katika mkakati wa matokeo makubwa sasa (BRN)

Mkuu wa mkoa wa Njombe Kapteni Mstaafu Aseri Msangi ameyasema hayo wilayani Makete mkoani hapa katika maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa na kusema kwamba ushirikiano wa pamoja kila mtu kwa nafasi yake kutasaidia kuzidi kuinua kiwango cha elimu kwa mkoa wake

Mh. Msangi amesema suala la kuongeza kiwango cha ufaulu ni la kila mmoja hivyo kuagiza maafisa elimu wilaya zote za mkoa huo kupita kwenye kila shule za sekondari na msingi kubaini changamoto zinazopelekea wanafunzi kufanya vibaya kwenye mitihani yao, na kuwashirikisha wazazi kwa kufanya nao kikao na baada ya hapo watagundua changamoto nyingi ambazo wataweza kuzitatua na zile zilizozidi uwezo wao watazipeleka sehemu husika ili zitatuliwe

"Nyie maafisa elimu wa wilaya zote, nawaagiza tembeleeni shule zenu hasa zile zinazofanya vibaya, mtagundua changamoto nyingi sana, pia muwashirikishe wazazi kwa kufanya nao kikao na muandike kwenye muhtasari maana mwisho wa mwezi huu nitaihitaji ili nione kama mmetekeleza, nawahakikishieni mtagundua mambo mengi sana huko" amesema Msangi

Amesema kwa sasa wanafunzi 538 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu bado hawajaripoti hivyo kutoa agizo kuwa wanafunzi hao watafutwe popote walipo ili waripoti shuleni tayari kwa masomo
 Mwanafunzi Noela Msinangila akisoma risala.

Awali akisoma risala kwa niaba ya wanafunzi wenzake mkoani Njombe, Noela Msinangila amesema wanaipongeza serikali kwa kuongeza idadi ya waalimu kila mwaka, kuongeza vitabu, kujenga mabweni pamoja na nyumba za waalimu huku wakiomba serikali kuendelea kutatua changamoto zinazowakabili ikiwemo uhaba wa vyumba vya madarasa, kuongeza idadi ya waalimu wa sayansi na hisabati, pamoja na kuwasaidia wanafunzi yatima na wanaoishi katika mazingira hatarishi.

Naye afisa elimu mkoa wa Njombe Bw. Said Nyasiro amesema mkoa wa Njombe umejipanga vilivyo katika kuinua kiwango cha elimu siku hadi siku kulingana na mipango iliyowekwa ikiwemo kuhskikisha wanafunzi wanasomea katika mazingira mazuri
 Afisa elimu mkoa wa Njombe Bw. Said Nyasiro akisoma taarifa ya elimu kimkoa.

Bw. Nyasiro amesema kwa sasa watahakikisha shule zote katika mkoa huo zitatoa chakula kwa wanafunzi wake kwa kuwa itasaidia wanafunzi hao kuzingatia masomo ipasavyo wawapo darasani, pamoja na kutoa zawadi kwa shule 10 za sekondari na msingi zinazofanya vizuri kimkoa kama motisha katika kuinua elimu

Katika maadhimisho pamoja na mambo mengine zimetolewa zawadi kwa shule 10 za sekondari na msingi zilizofanya vizuri pamoja na halmashauri 3 zilizoongoza kielimu

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI