MASHINDANO ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii
inayowahusisha waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari (NSSF
Media Cup) yameanza kutimua vumbi katika uwanja wa TCC, Chang'ombe jijini Dar
es Salaam.
Akifungua mashindano hayo, Waziri wa Kazi na Ajira,
Gaudencia Kabaka, amewataka wanahabari nchini kuhakikisha wanajiunga na Shirika
la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), ili kujihakikishia maisha ya amani na
utulivu baada ya kustaafu.
Alisema kuwa, wanahabari wanapaswa kwenda mbali zaidi katika
kulitumia shirika hilo, ili kunufaika na mafao mbalimbali yanayotolewa kwa
wanachama.
Katika ufunguzi huo, timu ya soka ya New Habari (2006) Ltd
iliumana na Habari Zanzibar katika Soka, ambako hadi filimbi ya mwisho Habari Zanzibar iliibuka
kidedea kwa magoli 4-1, magoli ya Zanzibar yaliwekwa wavuni na Amoor Suleiman aliyeweka
wavuni goli moja na Yusuph Juma magoli matatu huku goli la New Habari likiwekwa
wavuni na Florian Mwasinde.
Kwa upande wa netiboli, timu ya Jambo Leo iliichapa timu ya
Wizara ya Habari Bara kwa jumla ya magoli 59-8, katika pambano la upande mmoja
lilipoigwa kwenye viwanja hivyo.
Katika mechi ya pili ya netiboli, Azam Media iliumana na
Tanzania Standards Newspaper (TSN), ambako Azam waliibuka washindi kwa magoli
18-13.
Kabaka aliwataka washiriki wa mashindano hayo ya 11
yanayoshirikisha wafanyakazi wa vyombo vya habari kuonesha ushindani, ufundi na
nidhamu ili kuongeza hamasa ya michuani hiyo.
Alivitaka vyombo vya habari kuepuka kuingiza wachezaji wasio
wanahabari (mamluki), kudumisha lengo la umoja na ushirikiano baina ya shirika
hilo kongwe na vyombo vya habari, ikiwamo kuwapa mazoezi wafanyakazi wa vyombo
hivyo.
Waziri wa
Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka akizungumza wakati wa uzinduzi wa
mashindano hayo. Wa pili kushoto ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Taifa
la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Chiku Matesa.
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia
Kabaka (wa pili kulia), akipata maelezo kutoka kwa Ofisa Uhusiano wa Shirika la
Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Carolyne Newa wakati alipotemberlea banda la
NSSF wakati wa uzinduzi wa mashindano ya NSSF Media Cup 2014 kwenye uwanja
wa TCC Chang’ombe jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka
akisalimiana na mshambuliaji wa timu ya New Habari 2006, Joh Dande wakati wa
uzinduzi wa michuano ya NSSF Media Cup 2014 kwenye uwanja wa TCC Chang'ombe Dar
es Salaam.
Comments