Rais wa Zanzibar Dkt Shein Akutana na Ujumbe wa Mabalozi waUmoja wa Ulaya Ikulu Zanzibar


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                                                        31 Machi, 2014
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amefanya mazungumzo na ujumbe wa Umoja wa Ulaya-EU ambapo wamezungumzia masuala mbalimbali ya uhusiano na ushirikiano kati ya jumuiya hiyo na Zanzibar.
Katika mazungumzo hayo Dk. Shein ameishukuru Jumuiya ya Ulaya kwa misaada yake mingi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kueleza kuwa misaada hiyo imekuwa chachu katika kuongeza kasi ya kuleta maendeleo nchini.
Aliueleza ujumbe huo ulioongozwa na Mwakilishi wa Umoja huo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Balozi Filiberto Ceriani Sebregondi kuwa Serikali na wananchi wa Zanzibar wanathamini sana ushirikiano wake na Umoja wa Ulaya na wametiwa moyo kuona Umoja huo umekuwa wakati wote ukiziunga mkono jitihada zao za kuijenga Zanzibar.
Baadhi ya misaada inayotolewa na Umoja huo ni pamoja na msaada katika bajeti, sekta ya nishati hususan utafutaji wa nishati mbadala, marekebisho katika sekta ya sheria, uimarishaji wa taasisi zinazoshughulikia masuala ya demokrasia, utamaduni na pamoja na mradi wa kijamii katika kupiga vita ukatili dhidi ya watoto.
Dk. Shein ameuhakikishia ujumbe huo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Jumuiya hiyo na wanachama wake kwa kuwa Umoja huo na wanachama wake ni marafiki wa kweli wa Zanzibar na watu wake.   
Wakati huo huo Mwakilishi wa Umoja huo nchini, Balozi Filiberto Ceriani Sebregondi mbali ya kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kumpa fursa yeye na ujumbe wake kukutana nae alieleza kuwa  mazungumzo kama hayo yanatoa nafasi ya kubadilishana mawazo na viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kujifunza kutoka kila upande kuhusu namna bora ya kuimarisha na kuendeleza ushirikiano wao.
Alieleza kuwa wakiwa Unguja  wataonana na watu mbalimbali na ziara yao hiyo itawapeleka hadi kisiwani Pemba kujionea hali halisi ilivyo kisiwani huko.
Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Naibu Mwakilishi wa Umoja huo Bwana Tom Vens na mabalozi wa nchi wanachama wa Umoja huo nchini ambao ni Ubelgiji, Ufaransa, Ujarumani, Ireland, Italia, Uholanzi, Hispania, Sweden na Uingereza.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI