Dawa ya Katiba Mpya kura ya maoni-Membe

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe 
-----
 Kama ilivyo kwa makada wengine wa CCM, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe anaona kuwa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilifanya kosa moja; iliamua kuwateulia Watanzania idadi ya serikali za Muungano.
Membe anaona dawa pekee ya kumaliza mgogoro huo unaotishia kupatikana kwa Katiba Mpya, ni kuitisha kura ya maoni ili wananchi waamue kwanza wanataka Muungano wa serikali ngapi ndipo mchakato uendelee.

Katika mahojiano na Mwananchi wiki iliyopita, Waziri Membe alisema kama ni kuepuka gharama, basi kura ya maoni ifanyike sambamba na Uchaguzi Mkuu mwishoni mwa mwaka 2015.

“Kwa maoni yangu, utengenezaji wa katiba uko sawa na safari inayoanzia Dar es Salaam kwenda Kigoma,” alisema Membe ambaye pia ni Mjumbe wa Bunge la Katiba kutokana na kuwa Mbunge wa Mtama na kuongeza, “Kwa hiyo mnapotaka kusafiri, ni lazima mkubaliane aina ya usafiri kabla ya kuanza safari. Mkishaamua kusafiri kwa treni, mnajua safari itakuwaje.”


Alisema sura ya kwanza kwenye katiba yoyote ni muhimu kwa kuwa ndiyo inayoamua mambo mengine yanayofuata. Kwa maana hiyo, Waziri Membe anasema ingekuwa busara kwanza kuamua muundo wa Muungano kwa kuwa sura nyingine zinazofuata zinarejea kwenye sura ya kwanza, jambo ambalo halikufanyika.

“Sura hii ndiyo itakayoleta mwanga wa nini kijadiliwe kwenye sura nyingine zote. Sasa kama hatukubaliani hapo, tutajadilije vifungu vingine ndani ya katiba hiyo?” alihoji.

Akizungumzia kazi ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba, alisema ilifanya kosa moja tu la kuandika rasimu moja tu na kuwateulia Watanzania idadi ya serikali na kuiwasilisha kwenye Bunge la Katiba.

Alisema wakati Tume ya Warioba ilizunguka nchi nzima kutafuta maoni ya wananchi na kwamba wapo waliosema wanataka serikali mbili, wapo pia waliotaka serikali moja na vilevile wapo waliotaka tatu.

“Ilipaswa kurekodi maoni hayo kama yalivyo na kuyapeleka bungeni ili Bunge liyapitie na kufanyia uamuzi kulingana na mahitaji yaliyopo. Alipokosea Warioba na timu yake ni kupeleka bungeni rasimu moja yenye maoni ya pendekezo moja tu la serikali tatu,” alisema Membe ambaye alijinadi kuwa ana uzoefu mkubwa katika masuala hayo ya kuandika katiba kutokana na kushiriki kutatua migogoro sehemu nyingi duniani, ikiwamo Zimbabwe.

“Walitakiwa kuja na rasimu tatu; ya serikali tatu, mbili au moja. Duniani kote panapokea tofauti ya mawazo katika mambo ya msingi kama hilo, kunapelekwa rasimu nyingi bungeni ili Bunge lijadiliane kwanza na kufikia maafikiano, kabla ya kuendelea na kupitisha vifungu vingine.

“Hata kina Warioba walitakiwa waje na rasimu tatu bungeni; moja iwe ile ya watu wanaotaka serikali moja, nyingine iwe ya wale waliotaka serikali mbili na pia iletwe rasimu ya wale wanaotaka serikali tatu. Kisha wangesema (kina Warioba) maoni yetu sisi (tume) ni Serikali tatu. Sasa wao, mengine wameyamaliza wenyewe na bungeni wakaleta rasimu moja tu ya serikali tatu.”

Alisema pamoja na kosa hilo, bado Tanzania ina fursa ya kujisahihisha kwa kuitisha kura ya maoni... “Sasa, dawa yake ni moja tu. Twendeni kwa wananchi ili waamue kwa kupewa swali moja. Unataka serikali ngapi?” alisema.Kwa Habari zaidi

SHARE THIS STORY

0
Share


“Tunaweza kufanya kura ya maoni kwa njia mbili. Kwanza kuitisha kura ya maoni ili wananchi wajibu swali moja tu na pili, kama hiyo ni gharama, basi wakati wa uchaguzi mwakani, tupige kura nne. Moja ya Rais, nyingine ya mbunge, ya diwani na boksi jingine liwe la idadi ya serikali.”
Waziri Membe alisema suala la idadi ya Serikali ni moyo wa mchakato mzima wa Katiba, hivyo linapaswa kupatiwa ufumbuzi kwanza kabla mambo mengi hayajaendelea.
Kuhusu Ukawa
Alipotakiwa kuzungumzia hatua ya wajumbe wa Bunge la Katiba wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kususia vikao vya chombo hicho cha kuandika Katiba, alisema: “Jumuiya ya kimataifa inawashangaa. Wamekuwa wakiwaunga mkono kwa mambo mengi, lakini katika hili hawako pamoja nao.”
Alisema kitendo cha wachache kususia Bunge ni cha ajabu na hakijawahi kutokea katika nchi nyingine zaidi ya Tanzania.
“Ni ajabu wachache kujigeuza kuwa pressure group (wana harakati). Ukiachia watu wazuie Bunge (la Katiba) kwa sababu tu hawapo, unaua dhana ya demokrasia. Kama wachache wanatumia vibaya kutambuliwa kwao au mwaliko, tutaiharibu nchi. Nguvu ya wachache haiko kwenye kususia vikao, bali ndani ya Bunge la Katiba. Ninaamini baadhi yao wanajuta kwa kususia vikao.”
Alitetea kitendo cha Rais Jakaya Kikwete kutoa maoni yake wakati akizindua Bunge la Katiba kwa maelezo kuwa alifanya hivyo ili kuwapa changamoto.
“Ilikuwa ni food of thought (kitu cha kusaidia kutafakari). (Kikwete) Halazimishi. Hakwenda pale kama Kikwete, bali kama presidency (taasisi ya urais),” alisema.
Membe alisema hakuna mshindi katika mchakato wa Katiba Mpya, hivyo hakuna maana watu wakavutana kiasi cha kutaka kuuathiri mchakato huo ambao tayari umetumia mabilioni ya shilingi.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.