PANYA ROAD KWISHA KAZI! KOVA ALALA NJE SAA 120

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova. ya kuwakosesha amani wakazi wa Jiji la Dar es Salaam usiku wa Ijumaa iliyopita, lile kundi la vijana wahalifu linalojulikana kwa jina la Panya Road limefikia ukingoni baada ya kudhibitiwa kwa kasi kubwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Amani linakupa ‘full stori’.
Kundi hilo liliibuka majira ya saa moja jioni ya Ijumaa iliyopita na kufanya vurugu katika maeneo ya Magomeni-Kagera, Dar ikidaiwa kuwa walikuwa wakilipa kisasi baada ya mwenzao aliyefahamika kwa jina la Ayubu Mohamed  ‘Diamond’ kuuawa na wananchi wenye hasira kali.
TUJIUNGE NA KOVA
Akizungumza na wanahabari wetu ofisini kwake jijini Dar juzi, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema tangu siku ya tukio hadi Jumatano (jana) ameendelea na msako maalum wa kuwadaka Panya Road hao ambao ndiyo janga la mjini kwa sasa.

WANAE WAMMISI
“Nimeamua haswa kuwafungia kazi, silali, wanangu wananimisi kwa muda, naingia mzigoni usiku kucha kuhakikisha tunawakamata wahusika wote ambao wanasadikika ni wafuasi wa Panya Road. Hata leo (Jumanne) na kesho (Jumatano) msako upo palepale,” alisema Kova.

ALALA NJE SAA 120
Kutokana na msisitizo huo wa Kova, hesabu za harakaharaka zinaonesha kuwa, tangu Ijumaa iliyopita hadi Jumatano (jana), Kova atakuwa amelala nje kwa siku 5 sawa na saa 120 ambapo muda wa asubuhi anakuwa ofisini kama kawaida, jioni anaendelea na msako  akisimamia vijana wake.

Kundi linalodaiwa ni Panya Road.
WALIOKAMATWA
Kwa mujibu wa Kamanda Kova, hadi juzi Jumanne, idadi ya vijana 510 wanaotuhumiwa kuhusika na kundi hilo walikamatwa sanjari na viongozi wao watatu.
“Ukiachilia mbali wadogowadogo, vinara ambao tumewakamata ni Halfan Nurdini (24), mkazi wa Tandale-Sokoni, Said Mohamed (22), mkazi wa Tandale-Sokoni na Mohamed Ndangula mkazi wa Mburahati jijini Dar,” alisema Kova.

AMA ZAO AMA ZAKE
Akizidi kutilia msisitizo kuhusu kundi hilo ambalo ni maarufu kwa kupora mali za watu katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar, Kova alisema msako unaendelea kwa wale wachache ambao bado hawajatiwa nguvuni basi ama zao ama zake.
“Haiwezekani vijana kama hawa watishie amani, niwaambie tu wale ambao bado hatujawakamata, tutawafikia na wote tutawafikisha kwenye mikono ya sheria,” alisema.

JK APELEKEWA TAARIFA
Imeelezwa kuwa, kutokana na unyeti wa tukio hilo lililotikisa jiji kwa takriban saa nne (Ijumaa), taarifa ya namna ambavyo linashughulikiwa zimepelekwa Ikulu ya Magogoni kwa Rais Jakaya Kikwete ‘JK’ ambapo ametoa maagizo mazito juu ya wahusika.
“JK amepelekewa taarifa, ameelekeza cha kufanyika. Hili tukio halikuwa la kufumbia macho,” kilisema chanzo kilichopo ndani ya jeshi la polisi.

POLISI WAPONGEZWA
Wakizungumza na wanahabari wetu kwa nyakati tofauti, wananchi walilipongeza jeshi la polisi  chini ya Kamanda Kova kwa jinsi walivyolidhibiti kundi hilo.

Abdallah Juma, mkazi wa Tandale alisema kuwa nguvu ya polisi inapaswa kuungwa mkono ikiwa ni pamoja na raia kutoa taarifa zinazohusiana na vikundi kama hivyo.
”Wananchi tunapaswa kuunga mkono jitihada za jeshi la polisi, tukiungana kwa pamoja hakika hakutakuwa na wahalifu mitaani na tutaishi kwa raha mustarehe kuliko siku ile ya Ijumaa usiku,” alisema Abdallah.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
WANASIASA WATAJWA
Chanzo kilicho ndani ya jeshi la polisi kimewaonya baadhi ya wanasiasa ambao wanatajwa kuwashinikiza vijana hao kufanya vurugu katika harakati zao za kisiasa.“Vijana hawahawa wa Panya Road ndiyo wanaotumiwa na baadhi ya wanasiasa katika mipango yao. Huwa wanawapa fedha na kuwatuma kwenda kumzomea mgombea fulani, waache mara moja kwani wanachangia kuwapa nguvu,” kilisema chanzo hicho.

WAJUMBE WA MTAA KUKIONA
Chanzo kingine kimesema kuwa, mkakati umewekwa kuwataka wajumbe wa serikali za mitaa jijini Dar kuhakikisha hakuna Panya Road kwenye maeneo yao na mitaa itakayobainika kuwa na vibaka wengi, wajumbe watawajibishwa.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA