WANAOTAKA URAIS KUPITIA CCM, WAPAMBE WAO KUADHIBIWA KWA KUENEZA TAARIFA ZA UONGO;NAPE

 Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye akizungumza na waandishi wa habari, Katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibara asubuhi hii, kuhusu moja ya maamuzi ya Kamati Kuu ya CCM, ya kuwataka wanaotaka kuwania urais kupitia CCM na wapambe wao kuacha kueneza taarifa za uongo kwenye vyombo vya habari na kwamba atakayebainika kufanya hivyo atachukulia hatua kali za kinidhamu.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye akisisitiza jambo katika mkutano huo na waandishi uliofanyika katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui Znzibar asubuhi hiii.
……………………………………………………………………
Mwaka huu 2015 ni mwaka wa uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Rais wa Jamhuri ya Muungano. Hii ni kwa mujibu wa katiba ya nchi. Ratiba ya mchakato wa kuwapata wagombea wa CCM kwa nafasi hizo haijatolewa bado.

Itakumbukwa Kamati Kuu iliyopita ya tarehe 13/01/2015, iliyoketi Kisiwandui Zanzibar ilipitisha ratiba ya shughuli za kawaida za Chama kwa mwaka 2015 na kupanga kushughulikia ratiba ya mchakato wa uteuzi wa wagombea wa CCM vikao vijavyo.

Pamoja na kutotolewa kwa ratiba hiyo, bado zimekuwepo harakati nyingi za wanaotaka kuteuliwa na CCM kugombea nafasi mbalimbali hasa ya urais wa Jamhuri ya Muungano. Harakati hizo baadhi halali, nyingi haramu.

Pamoja na kutaadharishwa mara nyingi juu ya madhara ya harakati hizo kwa umoja na mshikamano wa Chama bado baadhi yao wamekuwa wakiendelea na harakati hizo.

Kwa muda sasa kumekuwepo na uzushi mwingi juu ya baadhi ya wanaotaka kuwania nafasi hizo kujadiliwa na hata kuchukuliwa hatua na vikao vya chama. Maneno haya kwa sehemu kubwa yamekuwa yakisambazwa na wagombea wenyewe au wapambe wao.

Uzushi huu, hauna nia njema kwa CCM, unalengo la kukigawa Chama na kuonyesha kama vile Chama hakina kazi nyingine ila kujadili na kushughulika na watu hao. Kwa mara nyingine CCM inapenda kuwataadharisha wagombea hao na wapambe wao kujiepusha na kusambaza taarifa zisizokuwa za kweli. Kwa kuwa vitendo hivi vinakigawa Chama chetu.

CCM haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya wote wanaosambaza taarifa hizi. Ni vyema wagombea wakawadhibiti wapambe wao na wakajichunga wenyewe dhidi ya hujuma hizi kwa Chama kwani zitawapotezea sifa ya kugombea.

Wengi wa wanaosambaza taarifa hizi ni wagombea au wapambe wasiojiamini kutokana na matendo yao, ambayo hata wao wana mashaka na uadilifu wao. Hatuoni sababu ya mgombea anayefuata sheria, kanuni na taratibu za Chama kuhofia kuchukuliwa hatua kila vikao vya Chama vinapofanyika.

Ukitenda kwa haki huna haja ya kuogopa vikao na kuzusha uongo na uzushi usio na ukweli. CCM inaamini matendo haya hayatajirudia.

Aidha Chama Cha Mapinduzi kinawaomba wanachama na wananchi kuzipuuza taarifa zinazosambazwa kwa kuvinukuu vyanzo visivyo rasmi, kama kuna hatua au taarifa kwa umma juu ya hatua yoyote katika mchakato huu basi itatolewa na wasemaji halali wa Chama na si kutoka vyanzo vya barabarani.

Itakumbukwa pia baada ya Kamati Kuu iliyopita kukutana tulitangaza kufanyika kwa kikao cha Kamati Ndogo ya Maadili kwa ajili ya kushughulikia masuala ya kimaadili kwenye sakata la Escrow kwa viongozi wa Chama walioko kwenye vikao vya Chama vya maamuzi.

Jana kumekuwepo na harakati nyingi za vyombo vya habari na watu binafsi kujaribu kupata taarifa ya nini kimetokea kwenye kikao hicho cha Maadili.

Tunapenda kuwakumbusha kuwa kwa mujibu wa taratibu taarifa za kilichotokea kwenye kikao cha Kamati Ndogo ya Maadili huwa hazitolewi kwa umma mpaka baada ya kufikishwa kwenye Kamati Kuu. Hivyo basi tunawaomba kutulia na kusubiri taarifa rasmi baada ya kufikishwa kwenye Kamati Kuu kuliko kuhangaika sasa hivi, jambo linaloweza kusababisha kuokotwa kwa habari za barabarani ambazo nyingi si za kweli. Tulieni subirini taarifa rasmi. KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI

Imetolewa na;- Nape Moses Nnauye Katibu wa Itikadi na Uenezi. 20/01/2015

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*