Serikali yajipanga kutumia nguzo za zege kusambaza umeme



Na Veronica Simba
Serikali inaendeleza jitihada za kuachana na matumizi ya nguzo za umeme za miti na badala yake kutumia nguzo za zege ikiwa ni hatua mojawapo ya kuboresha huduma ya usambazaji na upatikanaji wa umeme nchini.

Hayo yalibainika mwishoni mwa wiki katika kikao baina ya uongozi wa Kampuni ya Sunshine Group Ltd na wataalam wa sekta ya umeme kutoka Wizara ya Nishati na Madini pamoja na Shirika la Umeme nchini (Tanesco).

Katika kikao hicho, Kampuni ya Sunshine iliwasilisha mapendekezo (proposal) ya kuanzisha kiwanda cha kutengeneza nguzo za umeme za zege kwa ajili ya matumizi ya hapa nchini.

Akieleza msimamo wa Serikali kuhusu mapendekezo hayo, Kamishna Msaidizi wa Umeme, Mhandisi Innocent Luoga alisema Serikali ina dhamira ya kutumia nguzo za umeme zilizotengenezwa kwa zege na kuachana na za miti zinazotumika sasa kutokana na manufaa yake.

Mhandisi Luoga aliyataja manufaa ya kutumia nguzo za zege kuwa ni pamoja na uimara wa nguzo husika. “Huwezi kulinganisha uimara wa nguzo za zege na hizi za miti tunazotumia hivi sasa. Nguzo za zege ni madhubuti na imara zaidi,” alisema.

Akifafanua zaidi, Mhandisi Luoga alisema, kutokana na uimara wa nguzo za zege, uhai wake ni wa muda mrefu kulinganisha na nguzo za miti.

“Uhai wa nguzo za zege ni kati ya miaka 70 hadi 100, wakati uhai wa nguzo za miti ni miaka 50,” alisema Luoga na kusisitiza kuwa sifa hiyo ya uhai mrefu wa nguzo za zege inazalisha manufaa mengine kwa Serikali na wananchi kwa ujumla endapo nguzo hizo zitatumika.

Akielezea manufaa yanayotokana na uhai mrefu wa nguzo za zege, Mhandisi Luoga alisema Serikali itatumia fedha kidogo kutokana na nguzo za zege kudumu kwa muda mrefu, tofauti na nguzo za miti ambazo uhai wake ni mdogo.

Aidha, faida nyingine za kutumia nguzo za zege, zilizotajwa na wataalam katika kikao hicho ni pamoja na kuwa rafiki wa mazingira ambapo huepusha ukataji wa miti.

Nyingine ni uwezo wake wa kutopitisha maji na kutoshika moto kwa urahisi (water and fire proof).

Akihitimisha mazungumzo husika, Kamishna Luoga alisema Serikali itaendelea kufanya mazungumzo na Kampuni hiyo pamoja na wawekezaji wengine wenye nia ya kutengeneza nguzo za umeme za zege ili kufikia makubaliano yatakayowezesha pande zote mbili kunufaika.

“Mkakati wetu ni kwa Tanesco kutengeneza nguzo za zege kwa matumizi ya ndani ya nchi lakini ni vema tukapata wawekezaji wengine watakaosaidia kutengeneza nguzo hizo kwani mahitaji ni makubwa sana,” alisema.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA