Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya
Viwanda na Biashara Maria Bilia akizungumza wakati wa uzinduzi wa
mafunzo ya wadadisi 200 wa Sensa ya Viwanda itayofanyika nchi nzima
mwezi huu. Mafunzo hayo yanafanyika chuo cha Takwimu Mashariki mwa
Afrika kilichopo eneo la Changanyikeni jijini Dar es salaam.
Mkuu wa chuo cha Takwimu Mashariki
mwa Afrika kilichopo eneo la Changanyikeni jijini Dar es salaam
Prof.Ngalinda Innocent akizungumza na wadadisi watakaokusanya takwimu za
Sensa ya Viwanda mwezi huu wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku 14.
Mkuu wa chuo cha Takwimu Mashariki
mwa Afrika Prof. Ngalinda Innocent akizungumza jambo na Naibu Katibu
Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bi. Maria Bilia (katikati) na
Kamishna wa Sensa ya Watu na Makzi Bi. Hajjat Amina Mrsiho Said leo
jijini Dar es salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa
ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa akizungumza na wadadisi 200 watakaokusanya
takwimu za viwanda wakati wa Sensa ya Viwanda itakayofanyika nchini
nzima mwezi huu leo eneo la Chuo cha Takwimu cha Mashariki mwa Afrika
jijini Dar es salaam.
Baadhi ya wadadisi wa Sensa ya
Viwanda wakifuatilia hafla ya ufunguzi wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa
kukusanya takwimu sahihi wakati wa Sensa ya Viwanda leo jijini Dar es
salaam.
Kaimu Mkurugenzi wa Shirikisho la
wenye Viwanda nchini Bw.Hussein Kamote akizungumza wakati wa ufunguzi wa
mafunzo ya wadadisi 200 watakaokusanya takwimu wakati wa Sensa ya
viwanda itakayofanyika nchini mwezi huu.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya
Viwanda na Biashara Maria Bilia akiwa katika picha ya pamoja na
menejimenti ya NBS na wadadisi wa Sensa ya Viwanda.
…………………………………………………………………………………………………………
Na. Aron Msigwa – MAELEZO.
SERIKALI imewataka wamiliki wa
viwanda kuwapa ushirikiano wadadisi wa Sensa ya Viwanda watakaopita
katika maeneo yao kwa lengo la kukusanya takwimu sahihi za viwanda
vilivyopo nchini na mchango vinaotoa katika maendeleo ya taifa.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini
Dar es salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara
Maria Bilia wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku 14 ya wadadisi wa
Sensa ya Viwanda yanayoendelea katika chuo cha Takwimu cha Mashariki mwa
Afrika kilichopo eneo la Changanyikeni jijini Dar es salaam.
Amesema kuwa mafanikio
ya Sensa hiyo yatatokana na wamiliki wa viwanda kuthamini na kutambua
umuhimu za Sensa hiyo kwa kutoa ushirikiano kwa wadadisi watakaopita
katika maeneo yao kupata taarifa zinazohusu masuala mbalimbali ikiwemo
uzalishaji wa bidhaa na masuala ya ajira;
Amesema upatikanaji wa takwimu
sahihi kuhusu Sekta ya Viwanda nchini Tanzania utaiwezesha Serikali
kuweka Sera na mipango endelevu ya maendeleo itakayoisaidia sekta hiyo
kupiga hatua kimaendeleo.
“Sensa hii ya viwanda ni muhimu
kwa maendeleo ya nchi yetu, na mafanikio yake yatatokana na wenye
viwanda kutupa ushirikiano maana bila wao kutoa takwimu sahihi mipango
ya maendeleo kuhusu viwanda haitatekelezeka kwa sababu ya kukosa takwimu
sahihi” Amesema Bilia.
Kuhusu sampuli ya viwanda
vitakayoguswa na Sensa hiyo amesema ni pamoja na maeneo ya viwanda
yaliyoajiri watu wengi na yanayohusisha uzalishaji mkubwa wa bidhaa za
viwandani ,maeneo ya uzalishaji wa bidhaa za kokoto, bidhaa za vyakula
na maeneo yaliyoajiri mtu zaidi ya mmoja.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu
wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Dt. Albina Chuwa akizungumza wakati wa
ufunguzi wa mafunzo hayo amesema kuwa Sensa hiyo ya viwanda
itakayohusisha viwanda vyote nchini inafanywa kwa ushirikiano wa Ofisi
ya Taifa ya Takwimu na Wizara ya Viwanda na Biashara.
Amesema kukamilika kwa Sensa
hiyo kutaliwezesha taifa kuwa na takwimu sahihi za viwanda na kutambua
mchango wa Sekta ya viwanda katika uchumi wa taifa na mchango wa ajira
kwa wananchi.
Kuhusu mafunzo hayo ya siku 14
kwa wadadisi 200 watakaoendesha zoezi hilo amesema Ofisi ya Taifa ya
Takwimu kupitia Chuo cha Takwimu cha Mashariki mwa Afrika inaendesha
mafunzo hayo kwa vitendo na nadharia ili kuwawezesha na kuwajengea uwezo
wadadisi hao kukusanya takwimu bora.
“Lengo la kuendesha Sensa hii
ni kuhakikisha kuwa nchi yetu inapiga hatua na kuwa nchi yenye
maendeleo ya kati kwa kuwa na matumizi sahihi ya takwimu
ztu”
Kaimu Mkurugenzi wa Shirikisho
la wenye Viwanda nchini Bw.Hussein Kamote akizungumza wakati wa ufunguzi
wa mafunzo hayo kwa niaba ya wamiliki wa Viwanda nchini amesema kuwa
Sensa ya viwanda itakayofanyika nchini mwezi huu italiwezesha taifa
kuwa na takwimu sahihi zinazohusu sekta ya viwanda.
“Sensa hii ya viwanda ni muhimu
sana kwa maendeleo ya taifa nawaomba wenye viwanda watoe ushirikiano wa
kutosha maana bila wao zoezi hili litakuwa gumu”
Ameongeza kuwa Sensa ya viwanda
ni muhimu kutokana na mchango wake katika nchi nyingi za Asia ambazo
zimefanikiwa na kupiga hatua kimaendeleo kwa sababu ya kuwa Sensa
endelevu na takwimu sahihi za sekta ya viwanda na mchango wake katika
pato la taifa.
Comments