Kwenu mastaa wa tasnia mbalimbali Bongo, habari zenu bwana. Poleni na majukumu ya kila siku ya kulijenga taifa.
Mkitaka kujua afya yangu, mimi ni mzima, namshukuru Mungu naendelea kutimiza majukumu yangu, likiwemo hili la kuwaandikia barua.
Nimewakumbuka leo kupitia barua, nataka kuwaambia kwamba mimi pamoja na mashabiki wengine wa sanaa yenu tumewachoka. Tumechoka kuona na kusikia kila siku mkifanya maigizo kwenye maisha yenu halisi.
Hivi ni kwa nini kila kukicha tunasikia mnaachana? Kwa nini hamdumu kwenye uhusiano wa mapenzi? Kwa nini hamdumu kwenye ndoa kama mashabiki wenu wanavyowategemea?
Penzi linapoanza kushamiri, mnalinadi kwenye mitandao na vyombo vya habari. Mnawaaminisha mashabiki wenu kuwa mnapendana kwa kauli zenu motomoto lakini ndani ya miezi miwili mitatu penzi chali.Wengine mnaonesha kwamba mmedhamiria na kuamua kufunga ndoa kabisa, lakini kumbe moyoni bado mnakuwa mna lenu jambo. Mashabiki wenu wanafurahia kuona mmeoana lakini ndoa nayo haidumu, mnaachana
Comments