Mamlaka nchini Kenya imesema kuwa
walinda usalama wamekabiliana na washukiwa wa kundi la wapiganaji wa
kiislamu la Al- Shaabab, katika wilaya ya Ijara katika kaunti ya Garissa
Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo.
Mapema, wapiganaji hao
waliokisiwa kuwa zaidi ya 50 kutoka Somalia, wanasemekana kushambulia
kambi za polisi katika eneo la Yumbis, takriban kilomita 30 kutoka
Daadab.Wavamizi wa Al-Shabaab waliteka vijiji vitatu na kupeperusha bendera yao Kaskazini Mashariki mwa Kenya kwa muda kabla ya maafisa wa polisi nchini kenya kuwasili na kuwafurusha.
Vijiji vilivyovamiwa ni Ramu iliyoko Mandera, na vijiji vya Yumbis na Holugho vilivyoko Garissa.
Mwezi uliopita Al Shaabab walivamia chuo kikuu cha Garissa na kuwaua watu 150 wengi wao wanafunzi.
Kundi hilo kutoka Somalia linaaminika kuwa na wafuasi nchini Kenya ambapo limetekeleza mashambulizi kadha katika jitihada ya kuilazimisha serikali ya Kenya kuondoa majeshi yake nchini Somalia.
Majeshi ya Kenya ni miongoni mwa kikosi cha kulinda amani cha muungano wa Afrika Amisom ambao wanaisaidia serikali dhaifu ya Somalia kupigana na waasi wa Al Shabaab.
Comments