HOTUBA YA MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, AKIFUNGUA MKUTANO WA NNE WA MABALOZI WA TANZANIA TAREHE 25 MEI, 2015 KATIKA HOTELI YA RAMADA - DAR ES SALAAM
Rais
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa Nne wa Mabalozi wa Tanzania nje ya nchi. Mkutano huo umefanyika katika Hoteli ya Ramada Jijini Dar es Salaam ukiwa umebeba Kaulimbiu isemayo “Diplomasia ya Tanzania
Mhe.
Bernard Kamillius Membe (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa;
Mhe.
Mahadhi Juma Maalim (Mb), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa;
Balozi
Liberata Mulamula, Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa;
Balozi
Hassan Simba Yahya, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa;
Mabalozi wote;
Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya
Wizara;
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Shukran
na Pongezi
Nakushukuru wewe Mheshimiwa
Waziri na Viongozi wenzako wa Wizara kwa kunialika kushiriki ufunguzi wa Mkutano
wa Nne wa Mabalozi wa Tanzania. Mkutano huu ni wa pili katika awamu yangu na wa
nne baada ya ule wa tatu uliofanyika Zanzibar, mwaka 2008. Nafarijika kuona kuwa Wizara imeendelea na
utaratibu huu mzuri wa kuwakutanisha Mabalozi kujadili utekelezaji wa Sera ya
Mambo ya Nje ya nchi yetu. Utaratibu huu unatoa fursa ya kujitathmini, kupeana
mrejesho na kuweka malengo na mikakati mipya.
Ni matumaini yangu kuwa utaratibu huu mzuri utaendelezwa na Serikali
zinazofuatia.
Kauli
Mbiu
Mheshimiwa Waziri;
Nimeipenda kauli mbiu
ya Mkutano inayosema “Diplomasia ya
Tanzania kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025”. Imebeba ujumbe muafaka hasa
ukizingatia kuwa tuko katika hatua za mwisho za kukamilisha maandalizi ya
kuanza Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka 5. Kama mjuavyo Mpango huu ni
sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Muda Mrefu wa miaka 25 unaotekelezwa kwa
Mipango mitatu ya muda wa kati wa miaka mitano kila mmoja kwa Dira ya Maendeleo ya Taifa. Shabaha kuu ya
Dira hiyo ni kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.
Kama tunavyofahamu, Sera
ya Mambo ya Nje ni muendelezo wa sera ya ndani, hivyo ni jambo la busara kuitana
na kukumbushana nafasi na wajibu wa Wizara katika kuchangia jitihada za
Serikali kufikia lengo hilo. Nimefurahishwa na mada mlizochagua na watu
mliowaalika. Naamini mkutano huu utakuwa na mafanikio makubwa.
Hali
ya Dunia
Waheshimiwa Mabalozi;
Sote tunafahamu kuwa
tangu kuzinduliwa kwa Sera ya sasa ya Mambo ya Nje, mwaka 2004, mambo mengi yamebadilika.
Hii ni kweli kwa hapa nchini na hata duniani.
Mafanikio mengi yamepatikana na changamoto kubwa na ndogo zimejitokeza.
Kuyumba kwa uchumi wa dunia mwaka 2002 na 2009 kumekuja na athari nyingi
hususan kwa nchi maskini na zinazoendelea. Misaada ya maendeleo kutoka nchi tajiri
imepungua na masoko ya bidhaa zetu kama pamba, tumbaku na dhahabu yamekuwa yanayumba.
Mabadiliko ya tabianchi ni changamoto nyingine ambayo inatishia ustawi wa nchi
maskini. Bado majadiliano na nchi zilizoendelea yanaendelea ili watimize wajibu
wao wa kihistoria wa kutusaidia kujenga uwezo wetu wa kukabiliana na athari zake.
Hivi sasa sote tumeweka matumaini yetu kwenye mkutano wa Paris, Desemba 2015
kupata mkataba ulio bora. Tusipofanikiwa itakuwa hatari kubwa. Tanzania iendelee
na jitihada zake kama tulivyofanya wakati wa kuongoza Kamati ya Marais wa Umoja
wa Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabia Nchi (CAHOSCC).
Ndugu Mabalozi;
Vitendo vya uhalifu wa
kimataifa na ugaidi navyo vinazidi kushamiri duniani na kutuathiri hata sisi. Zamani
tulikuwa tunasikia mambo hayo yakitokea nchi za mbali, lakini, hivi sasa nasi
ni wahanga wa uhalifu huo. Mitandao ya kimataifa ya biashara ya dawa za kulevya
inaangamiza vijana wetu. Hivyo basi lazima tushiriki katika mapambano dhidi ya
biashara na matumizi ya dawa za kulevya.
Ndovu wetu wanatishiwa kumalizwa na
majangili na washirika wa mitandao ya kimataifa; na matishio ya ugaidi
yanaviweka vyombo vya ulinzi na usalama kuwa katika hali ya tahadhari wakati
wote. Majawabu ya changomoto hizi hayawezi kupatikana kwa juhudi za nchi moja
peke yake, yanahitaji ushirikiano na jumuiya ya kimataifa. Mabalozi mnao wajibu
wa kuendelea kutafuta wabiya wa kushirikiana nasi katika mpambano haya.
Utandawazi
unaostawishwa na maendeleo ya sayansi na teknolojia umeleta fursa na una
changamoto zake nyingi pia. Ukweli huo ndiyo iliyotufanya kutunga Sheria ya
Kudhibiti Uhalifu wa Mitandaoni (Cyber Crime Act) hivi karibuni. Vilevile, Jumuiya za Kikanda zinazidi
kuimarika katika kila kona ya dunia. Tanzania ni mwanachama wa EAC na SADC.
Ushiriki wetu umekuwa na tija na kuleta maslahi ya kiuchumi na kibiashara. Hata
hivyo hatuna budi kujituma na kujipanga vizuri zaidi ili tuweze kunufaika
zaidi.
Mafanikio
ya Diplomasia ya Tanzania
Waheshimiwa Mabalozi;
Pamoja na mabadiliko
hayo na changamoto zake, inatia moyo kuona diplomasia ya nchi yetu imeendelea
kustawi. Tanzania ina jina kubwa kikanda na kimataifa kuliko nguvu zetu za kiuchumi
na kijeshi. Kwa ajili hiyo tumekuwa tunaaminiwa na kushirikishwa katika
shughuli na mambo mbalimbali. Tumeendelea
kuwa sauti ya watu wasio na sauti na wanyonge na kuwa kimbilio lao. Ni kwa ajili hiyo tumeaminiwa katika majukumu
muhimu na Jumuiya za kikanda na kimataifa hususan AU, SADC na UN.
Jambo lingine la
kujivunia sote kuhusu diplomasia yetu ni kuwa na uhusiano mzuri na nchi jirani na
mashirika ya kimataifa. Nimeingia madarakani Tanzania ikiwa haina adui, na naondoka bila
adui. Kwa jumla tumefanikiwa kuimarisha udugu, urafiki na ushirikiano na
majirani zetu wote. Pale palipotokea
upepo mbaya, tumetumia njia za kidiplomasia kuondoa tofauti zetu tukiongozwa na
hekima ya wahenga kuwa: “unaweza
kuchagua rafiki lakini huwezi kuchagua jirani”.
Hali kadhalika,
tumepokea wageni wengi waliofanya ziara nchini ikiwemo marais wa mataifa
makubwa duniani yakiwemo Marekani na China.
Ziara hizo ziliitangaza nchi yetu na kufungua milango ya fursa kwa nchi
yetu ya kunufaika kwa misaada ya maendeleo, biashara na vitega uchumi.
Vilevile, tumepanua
wigo wa mahusiano kwa kuongeza marafiki na wabia wengine wa maendeleo. Katika
kipindi cha miaka 10 nchi 6 za Brazil, Oman, Uturuki, Qatar, Umoja wa
Falme za Kiarabu (UAE) na Namibia zimefungua ubalozi nchini Tanzania. Aidha, nchi 16 za Morocco, Malta, Equador, Montenegro, Azerbaijan, Bosnia na
Herzegovina, Moldova, Saint Vincent na Grenadies, Fiji, Paraguay, Kosovo,
Geogia, Kyrgyzstan, Visiwa vya Marshall, Visiwa vya Solomon, na Kazakhstan
zimeanzisha uhusiano wa kidiplomasia na nchi yetu. Nchi yetu pia imefungua
Ofisi za Ubalozi katika nchi 7 za Brazil, Uholanzi, Malaysia, Oman, Kuwait,
UAE na Comoro. Kama hali itaruhusu tunatarajia
kufungua Ubalozi nchini Uturuki na Algeria kabla ya kumaliza kipindi changu cha
uongozi.
Mahusiano haya mapya na yale ya zamani ambayo tumeendelea kuyapalilia
yamefungua fursa nyingi kwa nchi yetu na watu wetu. Mahusiano haya yametuwezesha kupata mikopo na
misaada ya kimaendeleo ambayo imeziongezea Serikali zetu mbili: Serikali ya
Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar uwezo wa kutekeleza
miradi ya maendeleo. Tunapojisifu leo
hii kwa hatua kubwa katika kujenga miundombinu msingi ya mawasiliano, uchukuzi
na nishati na upanuzi na uboreshaji mkubwa wa huduma za jamii kuna michango muhimu
ya wadau wa nje. Haya ni matokeo chanya kazi yenu nzuri ya kuyajenga na
kuyastawisha mahusiano mazuri na mataifa.
Miradi mikubwa ya uzalishaji wa umeme, barabara, bomba la gesi, viwanja
vya ndege, mkongo wa taifa ni matokeo ya mahusiano hayo. Nawashukuru sana kwa mchango wenu huo.
Maeneo mawili mapya katika Sera yetu
ya Mambo ya Nje katika kipindi cha miaka 10 iliyopita ni ushirikishwaji wa
Watanzania waishio ughaibuni (Diaspora) na ushiriki wa Ulinzi wa Amani
(Peace-keeping Operation). Ni katika
kipindi hiki tumetunga Sera ya Diaspora na kuamsha hamasa ya kuwatambua na
kuwashirikisha Watanzania wenzetu waishio nje katika gurudunu la maendeleo.
Hatukuweza kukidhi haya yao ya uraia pacha lakini tumefanikiwa kuwapa haki
mahsusi kwenye Katiba Pendekezwa.
Tumeshiriki katika shughuli za ulinzi wa amani kule Darfur Sudan, Lebanon
na DRC chini ya operesheni za Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika. Aidha, tumeshiriki katika utatuzi wa migogoro katika bara la
Afrika ukiwemo ule wa Comoro na kurejesha umoja wa nchi hiyo.
Mpango wa Taifa 2015 – 2020
Waheshimiwa Mabalozi,
Mafanikio niliyoyataja ni sehemu tu ya mafanikio mengi tuliyoyapata
katika kutekeleza Sera yetu ya Nje. Nchi yetu iko salama na haina maadui bali
marafiki duniani kote. Tumefanikisha kuvutia misaada ya maendeleo, vitega
uchumi na biashara, mambo ambayo yamechangia katika jitihada za nchi yetu kukuza uchumi na
kupunguza umaskini. Jukumu kubwa lililo
mbele yetu ni kutumia fursa zetu kuwa na mahusiano mazuri na mataifa na
mashirika ya kimataifa pamoja na ya kijiografia na maliasili yetu kujenga uwezo
wetu wa kiushindani kikanda na duniani.
Mheshimiwa
Waziri;
Mtakumbuka kuwa, malengo makuu ya Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa
Miaka Mitano tunaomalizia ulilenga kuondoa vikwazo vya ukuaji wa uchumi.
Shabaha yake ni:
(a)
kujenga
uwezo wa nchi yetu kukuza uchumi na kuondoa umaskini haraka;
(b)
kujizatiti
kutumia fursa zilizopo nchini kukuza mahusiano ya kiuchumi baina ya nchi yetu na
nyingine katika Jumuiya za Kikanda na Kimataifa;
(c)
Kukuza ajira ili kupunguza tatizo la
ajira linalowakabili vijana.
Siwezi kusema
tumefanikiwa kila kitu, lakini tumepiga hatua ya kuridhisha na tumeonyesha
muelekeo mzuri. Hali ya uchumi kwa maana
ya viashiria vya uchumi jumla, tupo mahali pazuri. Pato la Taifa limekuwa kwa wastani wa asilimia 7 na kuongezeka kutoka Dola za
Kimarekani bilioni 14.4 mwaka 2005
hadi Dola za Kimarekani bilioni 43 mwaka
2015. Hivyo hivyo, pato la wastani la Watanzania nalo limeongezeka kutoka Dola za Kimarekani 375 mwaka 2005 hadi Dola za Kimarekani 944 mwaka 2014.
Katika kipindi cha
muongo mzima sasa, makusanyo ya kodi yameongezeka kutoka shilingi billion 177.1 mwaka 2005 hadi shilingi bilioni 800 mwaka 2015. Tumefanikiwa
kudhibiti mfumuko wa bei kutoka asilimia
18 mwaka 2011 hadi asilimia 4.5 mwaka
huu. Hivi karibuni thamani ya sarafu yetu imekua inapungua dhidi ya dola ya
Marekani. Hatuko peke yetu thamani ya dola ya Marekani imepanda dhidi ya sarafu
zote duniani.
Katika kipindi hiki
pia tumefanikiwa kuboresha miundombinu ya usafirishaji yaani upanuzi na
uboreshaji wa bandari, ujenzi wa barabara na uimarishaji wa reli na uzalishaji na
usambazaji wa umeme nchini. Aidha, tumerekebisha baadhi ya sheria zilizokuwa
zinatukwamisha ili kuboresha mazingira ya uwekezaji. Nimefurahi kuwa katika mkutano huu wahusika
watapata fursa ya kuzungumza na Mabalozi kuhusu maeneo hayo. Kwa ujumla, tumeweka
msingi mzuri wa ukuaji wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kuelekea mwaka 2025.
Mpango wa Pili wa
Maendeleo wa Miaka 5 ambao tunauanza katika mwaka wa fedha ujao, unalenga
katika kuhamasisha mapinduzi ya viwanda kwa lengo la kuongeza thamani ya
maliasili zetu na bidhaa za kilimo, kujenga uwezo wetu wa biashara ndani na nje
ya eneo la Jumuiya ya Afrika Mashariki na kukuza ajira.
Mpango huu unalenga
kujenga juu ya mafanikio ya mpango wa kwanza. Hivyo, utekelezaji wa mpango huu
unahitaji sana tuvutie vitega uchumi na teknolojia za kisasa nchini kwa lengo
la kuchochea mapinduzi ya viwanda vidogo, vya kati na vikubwa. Tukifanikiwa katika haya tutaweza kuitumia
vizuri fursa tulizonazo na ile ya kijiografia ya kuzungukwa na soko kubwa.
Ndugu Waziri na Ndugu Mabalozi;
Nchi inawategemea
ninyi kutumia nafasi mlizonazo kuvutia wawekezaji zaidi, teknolojia za kisasa na
kutafuta masoko ya bidhaa zetu. Hili ni
jukumu lenu la msingi katika utekelezaji wa diplomasia ya uchumi. Nawataka muwe
wabunifu na makini katika kuwaunganisha wafanyabiashara wa nchini na wenzao wa
nje mnakowakilisha nchi yetu.
Katika dunia ya sasa na
huko tuendako, usalama na ustawi wetu utategemea zaidi uwekezaji na biashara na
si misaada ya maendeleo ambayo imeendelea kuwa isiyotabirika na isiyotosha. Hamna budi sasa kuongeza msukumo kwenye kuvutia
watalii, wawekezaji, kutafuta masoko na kusaidia wafanyabiashara wa Tanzania
kufanya biashara nje. Ningefarijika sana
kama mtajipima na kujisifu kwa uchangiaji wenu kwa uchumi na kuwawezesha wafanyabiashara
wetu kujitanua kimataifa.
Zama za sasa haitoshi
kujisifu kwa uhodari wa kuandika ripoti na kuhudhuria mikutano. Tujisifu pia kwa
kuchangia kukuza uchumi wa nchi. Ni vizuri kujiuliza mtachangia vipi kuwezesha
uchumi wetu kukua na hivyo uwezo wa Serikali kuongezeka kipato ili bajeti za balozi
ziweze kuongezeka. Kila mtu ajiulize
ubalozi wake umechangia nini na kiasi gani? Je, nini kifanyike ili ubalozi huo
uweze kuchangia zaidi. Ni matumaini
yangu kuwa mkutano huu utatafuta majawabu na maswali haya. Huo ndio mtazamo chanya wa kuelekea nchi ya
uchumi wa kati mwaka 2015.
Waheshimiwa Mabalozi;
Mnatakiwa pia kutafuta
wabia wapya wa maendeleo na kuimarisha ushirikiano nao. Hawa siyo wengine bali
ni mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) na Watanzania wenzetu waishio nje (Diaspora).
Nchi zinazotoa misaada ya maendeleo hupitishia kiasi kikubwa mikononi mwa NGOs.
Aidha, mifuko ya misaada ya watu binafsi Bill
and Melinda Gates Foundation zinatoa michango muhimu kwa maendeleo ya
kiuchumi na kijamii wakati mwingi inazidi hata ile tunayopata kutoka nchi
wahisani. Bado ipo nafasi ya kuongeza ushiriki wa taasisi za namna hii kwa
maendeleo yetu. Isitoshe taasisi nyingine zina ushawishi mkubwa kwa mashirika
ya kimataifa, Serikali na sekta binafsi. Hivyo basi, tukiweza kuimarisha uhusiano
na taasisi hizi tutafaidika katika jitihada zetu za kujiletea maendeleo.
Watanzania wanaoishi
nje ya nchi nao wanaweza kutoa mchango
muhimu. Mazungumzo yangu nao yanaendelea kuzaa matunda. Wengi wameonesha
hamasa kubwa ya kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo nyumbani.
Zipo nchi duniani zinazonufaika na diaspora zao na sisi inaweza kuwa hivyo. Tumeanza
lakini bado tunahitaji kuongeza juhudi. Mkutano huu uje na mawazo mazuri juu ya
nini kifanyike kuwafanya Watanzania walio nje wachangie zaidi ya wafanyavyo
sasa. Tuangalie wenzetu hao wanafanya
vipi na kuiga yale mazuri tuyafanye.
Uboreshaji wa
Maslahi na Mazingira ya Kazi ya Watumishi wa Nje
Mheshimiwa Waziri;
Waheshimiwa Mabalozi,
Katika
kipindi cha Awamu ya Nne tumeendelea kuboresha mazingira ya kazi ya Balozi zetu
na maslahi ya watumishi wake. Nasema
tumejitahidi kwa kuwa tofauti na watumishi wa kada nyingine serikalini, kada ya
utumishi wa nje mahitaji yake ya kifedha ni makubwa sana. Hii ni kutokana na
kuzingatia mazingira yao ya kufanyia kazi nje ya nchi yetu. Tumeendelea kuiboresha hali kadri uwezo wetu
wa fedha uliporuhusu. Ninyi ni mashuhuda
wa maboresho ya msingi tuliyoyafanya katika Kanuni za Watumishi wa Nje (Foreign
Service Regulations). Tumerekebisha viwango vya posho ya nje (Foreign Service
Allowance), posho ya wenza na ya elimu kwa watoto wa watumishi wakiwa ubalozini. Aidha, tumewapatia balozi vitendea kazi
ikiwemo magari ya uwakilishi yenye hadhi na heshima inayolingana na Balozi.
Kutokana na kuanza
kutengwa fedha za maendeleo, Wizara imeweza kununua na kujenga majengo ya
ubalozi ambayo pia ni vitega uchumi. Tumefanya hivyo New York, Washington DC na
Paris. Tunatarajia kujenga majengo ya namna
hiyo Nairobi na Oman. Pamoja na ununuzi,
tumeendelea na ukarabati wa majengo mengi ya Balozi zetu katika kuboresha taswira
ya nchi yetu nje. Lengo letu ni siku
nyingine tuachane na kupangisha majengo ya ofisi na kuishi katika Balozi zetu bali
yawe mali yetu. Kwa kuwa ni vitega uchumi pia vitega uchumi na hivyo kutaziongezea
Balozi mapato na uwezo wa kujiendesha bila kutegemea sana fedha kutoka
nyumbani.
Vilevile, kuna haja
kwa Wizara kujenga uwezo wa maafisa waliopo na watakaoajiriwa kupitia mafunzo
na kupata uzoefu kwa kutenda. Ninachozungumzia hapa ni kuwa na maafisa wenye uelewa mtambuka na uwezo
wa kuchambua mambo na kushiriki ipasavyo kwenye majadiliano ya kimataifa. Wasiwe
wasikilizaji tu bali wawe washiriki makini wanaofahamu maslahi ya nchi na
kuyalinda. Chuo cha Diplomasia
kiendelezwe kwa ajili ya kuandaa wanadiplomasia wetu. Pia tuwapeleke watumishi wetu kuongeza elimu
katika vyuo mbalimbali duniani. Aidha, mnapaswa sana kupanua wigo wa ujuzi wa
maafisa wetu. Muwe na mchanganyiko wa taalama
nje zaidi ya uhusiano wa kimataifa. Mnahitaji
wataalamu wa elimu ya fani za uchumi, biashara ya kimataifa, nishati na
nyinginezo.
Mheshimiwa Waziri na viongozi
wenzako;
Mabalozi;
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Nashiriki Mkutano huu
kwa mara ya mwisho nikiwa Rais wa Nchi yetu. Hivyo, napenda kutumia nafasi hii
kuwaaga rasmi. Naondoka nikiwa na kumbukumbu nzuri kwenu kwani tumefanikiwa
mengi pamoja. Nakushukuru sana
Mheshimiwa Waziri Bernard Membe kwa ushirikiano na msaada wako mkubwa na
wenzako katika kunisaidia katika eneo langu hili kwa miaka tisa. Naelewa ugumu na uzito wa jukumu lenyewe
maana name niliwahi kuwa Waziri wa Mambo
ya Nje kwa miaka 10. Nakupongeza kwa
jinsi ulivyoongoza vizuri Wizara hii nyeti na mafanikio mliyoweza kupata. Hii
ni Wizara ambayo haikuwahi kuninyima usingizi katika kipindi cha uongozi wangu.
Naondoka nikiwa na faraja kuwa Diplomasia yetu iko katika hali nzuri. Nina imani kuwa wanadiplomasia wetu watafanya
Watanzania tuendelee kutembea kifua mbele.
Daima mkumbuke ule msemo wetu, “Better than yesterday, Less than Tomorrow”
yaani tuhakikishe tunafanya vizuri kuliko jana, ingawaje ni pungufu kuliko kile
tutakachofanya kesho.
Inawezekana, timiza
wajibu wako.
Asanteni sana kwa
kunisikiliza
Comments