HOTUBA YA RAIS KIKWETE MAADHIMISHO YA WIKI YA ELIMU



HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE KATIKA KILELE CHA MAADHIMISHO YA PILI YA KITAIFA YA WIKI YA ELIMU TANZANIA UWANJA WA JAMHURI, DODOMA - TAREHE 15 MEI, 2015

Mheshimiwa Dkt. Shukuru Jumanne Kawambwa (Mb), Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi;
Mheshimiwa Hawa Ghasia (Mb), Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa;
Waheshimiwa Manaibu Waziri;
Mheshimiwa Chiku Galawa; Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Magreth Sitta (Mb), Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii;
Waheshimiwa Wabunge;
Balozi Ombeni Sefue, Katibu Mkuu Kiongozi;
Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu;
Washirika wa Maendeleo;
Wadau wa Maendeleo ya Elimu;
Viongozi wa Serikali na Mashirika ya Dini;
Walimu na Wanafunzi;
Ndugu Wanahabari;
Ndugu Wananchi;
Mabibi na Mabwana.

Shukrani

Ninayo furaha kubwa ya kuungana nanyi leo katika kuhitimisha maadhimisho haya ya pili ya kitaifa ya wiki ya elimu. Nakushukuru wewe, Mheshimiwa Waziri na viongozi wenzako wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa kunipa heshima hii kubwa ya kushiriki  maadhimisho haya.
Pia, nawashukuru na kuwapongeza kwa dhati viongozi na wananchi wa Mkoa wa Dodoma wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Chiku Galawa kwa kukubali kuwa wenyeji wa maadhimisho haya kwa mara ya pili mfululizo. Vile vile, napenda  kuipongeza Kamati ya Maandalizi ya Kilele cha Maadhimisho ya Pili ya Kitaifa ya Wiki ya Elimu Tanzania kwa kazi nzuri waliyofanya ya kufanikisha shughuli hii. Kwenu wote nasema hongereni sana!

Kauli Mbiu
Ndugu Waziri;
Ndugu wananchi;
          Nimefurahishwa na kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu isemayo “Elimu Bora ni Haki ya Kila Mtoto kwa Maendeleo ya Taifa”. Kauli mbinu hii ni muafaka kabisa  kwa kuwa kupata elimu ni moja ya haki ya msingi ya mtoto. Tena lazima apate elimu iliyo bora. Aidha kauli mbiu inaakisi kwa usahihi madhumuni na malengo ya Serikali katika hatua inazochukua kuendeleza elimu nchini. Kuwapatia Watanzania elimu bora ndiyo shabaha   ya msingi ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 niliyoizindua mapema mwaka huu.  Pia ndiyo shabaha ya Sera zilizokuwepo kabla ya hii tangu uhuru mpaka sasa.  Tulichokifanya katika awamu hii ni kutoa msukumo mkubwa zaidi katika kuendeleza elimu.  Kama ilivyokuwa kauli mbiu yetu ya ari Mpya, Nguvu Mpya na Ari Mpya na baadae ile ya Ari Zaidi, Nguvu Zaidi na Kasi Zaidi.
Ni ukweli ulio wazi kuwa tumepata mafanikio ya kutia moyo ingawaje bado tuna kazi kubwa ya kufanya mbele yetu.  Tuliamua kuanzisha maadhimisho ya Wiki ya Elimu nchini kwa malengo mawili. Kwanza,  kuelimisha Watanzania kuhusu jitihada zinazoendelea kufanyika na hatua tunazopiga katika kuboresha elimu na kuongeza fursa kwa watoto wetu na Watanzania kwa ujumla kupata elimu.  Pili, kutambua na kuwatunza waliofanya vizuri katika nyanja mbalimbali za elimu.

Chanzo cha Maadhimisho ya  Wiki ya Elimu

Ndugu Wananchi;
Katika kuboresha utendaji wa Serikali na kutekeleza mipango na ahadi zake tulibuni Mkakati wa Matokeo Makubwa Sasa (Big Results Now - BRN). Katika mpango huo Elimu ilikuwa miongoni mwa sekta sita za mwanzo, nyingine zikiwa maji, kilimo, nishati, miundombinu na mapato ya serikali.  Baadae tumeongeza mazingira ya uwekezaji na afya.
Baada ya kufanya uchambuzi wa hali ilivyo na kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizopo katika elimu ilikubaliwa mambo tisa kupewa kipaumbele. Mambo hayo ni:-
(i)              Upangaji wa shule kwa ubora kwa matokeo ya mtihani kitaifa kuanzia shule iliyoongoza hadi ya mwisho.
(ii)           Uratibu wa utoaji wa tuzo kwa shule zilizofanya vizuri,
(iii)        kuwa na kiongozi cha usimamizi wa shule,
(iv)        Upimaji wa kitaifa wa stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu,
(v)           Mafunzo kwa walimu kwa stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu,
(vi)        Kujenga uwezo wa walimu na wanafunzi katika ufundishaji na ujifunzaji,
(vii)     Ujenzi wa miundo mbinu muhimu ya shule; madarasa,
(viii)  Utoaji ya ruzuku wa uendeshaji wa shule na,
(ix)         Utoaji wa motisha kwa walimu.
Kuhusu utoaji wa tuzo naipongeza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa uamuzi wa busara kuwa tuzo hizo zitolewe kwenye kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya elimu.
Ndugu Wananchi;
Ni matazamio yetu kuwa utoaji wa tuzo hizi utakuwa kichocheo cha kujenga ari, hamasa na tabia ya ushindani wa kitaaluma ndani ya mfumo wa Elimu. Jambo hilo litasaidia kuinua ubora na ufanisi katika ngazi zote za elimu.  Ushindani wa kitaaluma utasababisha kuongezeka kwa ufanisi na uwajibikaji katika kufundisha na kujifunza na hatimaye kuendelea kuboresha uelewa wa wanafunzi na kuwafanya wawe na matokeo mazuri.
Tuzo kwa Waliofanya Vizuri katika Mitihani ya Taifa ya
Mwaka 2014 na Uandishi wa Insha za Jumuiya ya Afrika
Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC)

Ndugu wananchi;
Napenda kutumia nafasi hii kutoa pongezi nyingi kwa wale wote waliopata Tuzo. Wahenga wamesema “mcheza kwao hutunzwa”. Siku hii ya leo, jumla ya shule 20 na wanafunzi 20 waliofanya vizuri katika matokeo ya mitihani ya Taifa ya darasa la saba na kidato cha nne mwaka 2014 wamepokea zawadi na tuzo. Nazipongeza sana shule zetu hizi na wanafunzi wote hawa kwa ushindi waliopata. Aidha jumla ya shule 3,090 yaani 2,166 za msingi na 924 za sekondari zilizopata ufaulu uliotukuka na nyingine kuongeza ufaulu kwa kiwango cha juu zitapata tuzo na zawadi stahiki.
Mheshimiwa Waziri;
Ndugu wananchi;
Niruhusuni pia nitoe pongezi kwa vijana 13 walioitoa nchi yetu kimasomaso katika mashindano ya uandishi wa insha yanayoendeshwa na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Umoja wa Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC). Hongereni Sana.
Hali kadhalika, natoa pongezi maalum kwa wale vijana watatu (3) waliopata ushindi kwa kuandika insha bora na wengine watatu (3) waliochora picha bora kuhusiana na kauli Mbiu ya maadhimisho ya mwaka 2015. Naomba Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi wakishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuongeza wigo wa mashindano ya kitaaluma kwa wanafunzi. Naamini kufanya hivyo kutasaidia kuibua vipaji vya watoto wetu tangu wakiwa wadogo. Tusiishie hapo, nawasihi walimu, wazazi, walezi na jamii nao wahakikishe kuwa vipaji hivi vinaendelezwa.
Ndugu Wananchi;
Maadhimisho haya yanatukumbusha sote juu ya wajibu wa kila mwananchi kushiriki katika shughuli za maendeleo ya shule na ufuatiliaji wa karibu wa shughuli zote zinazofanyika shuleni kwa lengo la kumuwezesha kila mtoto kupata elimu bora. Ni ukweli ulio wazi kwamba wajibu wa kuhakikisha watoto wetu wanapata elimu bora si wa Serikali pekee, bali pia ni wa wazazi na walezi wanaoishi na watoto na jamii kwa ujumla. Daima tukumbuke kuwa watoto hawaishi Serikalini bali kwenye familia na jamii hivyo wazazi, walezi na jamii ina nafasi maalum katika maendeleo ya mtoto kwa upande wa elimu na mambo mengine maishani.
Maendeleo katika Sekta ya Elimu Nchini
Ndugu Wananchi;
Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita tumeweza kupiga hatua kubwa katika sekta ya elimu nchini. Ninyi mliopo hapa ni wadau muhimu hivyo ni mashahidi wa mafanikio tuliyoyapata ambayo ni matokeo ya kuongezeka kwa shule, idadi ya wanafunzi, idadi ya walimu, vitabu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia. Katika kipindi hicho, Shule za msingi zimeongezeka kutoka shule 14,257 mwaka 2005 hadi kufikia shule 16,343 mwaka 2014. Hii imefanya idadi ya wanafunzi kuongezeka kutoka milioni 7.54 hadi kufikia milioni 8.23. Kwa upande wa shule za sekondari, idadi yake imeongezeka kutoka shule 1,745 mwaka 2005 hadi kufikia shule 4,576 mwaka 2014. Hali kadhalika, idadi ya wanafunzi wa shule za sekondari imeongezeka kutoka wanafunzi 524,325 mwaka 2005 hadi kufikia wanafunzi 1,804,056 mwaka 2014.
 Jumla ya walimu wote wa msingi na sekondari idadi imeongezeka kutoka 153,767 mwaka 2005 hadi 301,960 mwaka 2015.  Katika kipindi hicho, vyuo vya ufundi vimeongezeka kutoka 184 mwaka 2005 hadi 744 mwaka 2015.  Wanafunzi wa elimu ya ufundi nao wameongezeka kutoka 40,059 mwaka 2005 hadi 145,511 mwaka 2015. Kwa upande wa elimu ya juu, wanafunzi wa vyuo vikuu wameongezeka kutoka 40,719 mwaka 2005 hadi 200,986 mwaka 2014. Hii ni kutokana na kuongezeka kwa vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki vimeongezeka kutoka 26 mwaka 2005 hadi 52 mwaka 2015.  Upanuzi huu mkubwa katika udahili wa wanafunzi wa vyuo vikuu umewezekana kutokana na kuongezeka kwa bajeti ya Bodi ya Mikopo ya wanafunzi na kuruhusu wanafunzi wa vyuo vikuu vya binafsi navyo wapatiwe mikopo.  Bajeti iliongezwa kutoka shilingi bilioni 56.1 mwaka 2005 hadi shilingi bilioni 345 mwaka 2015 na kunufaisha wanafunzi 98,000 mpaka sasa.


Ndugu Wananchi;
Mafanikio haya ni matokeo ya kutoa kipaumbele cha kwanza kwa elimu katika bajeti ya serikali. Leo hii bajeti ya sekta ya elimu ndiyo kubwa kuliko zote nchini ambayo sasa imefikia shilingi trilioni 3.4 ikilinganishwa na shilingi bilioni 669.5 mwaka 2005. Tumefanya hivyo kwa kutambua kwamba kuwekeza kwenye elimu ni kuwekeza kwenye uhai na maendeleo ya taifa na watu wake sasa na miaka mingi ijayo. Tusipowekeza kwenye elimu, Watanzania hawataweza kutawala mazingira na raslimali zao na kuzitumia kujiletea maendeleo. Taifa lisilowekeza katika elimu, halina nafasi huko tuendako.
Ndugu wananchi;
Ukiacha sababu hizo, jambo lingine lililotufanya tuongeze sana bejeti ya elimu ni ule ukweli kwamba, wakati Serikali ya Awamu ya Nne inaingia madarakani mwaka 2005 Tanzania ilikuwa nyuma kwa wanafunzi wa elimu ya msingi, sekondari na vyuo vikuu kuliko Kenya na Uganda. Lakini nchi yetu ndiyo kubwa kuliko nchi zote katika Jumuiya ya Afrika ya Mashariki.  Takwimu zilizopo zinaonesha kuwa mwaka 2005, Tanzania ilikuwa na wanafunzi wa shule za sekondari 524,325 wakati Uganda ilikuwa na wanafunzi 728,393 na Kenya 925,341. Kwa upande wa vyuo vikuu Tanzania ilikuwa na wanafunzi 40,719, wakati Uganda ilikuwa na wanafunzi 124,313 na Kenya ilikuwa na wanafunzi 108,407.    
Kwa kuwa nyuma ya wenzetu katika utoaji wa fursa ya elimu kwa vijana wetu kulituweka pagumu katika kutoa ushindani katika soko la jumuiya ya Afrika Mashariki.  Wakati ule wazazi wengi walilazimika kupeleka watoto wao kusoma Uganda na Kenya. Tukafanya uamuzi wa makusudi kuongeza uwekezaji kwenye elimu ili fursa ya kupata elimu ya msingi, sekondari na chuo kikuu ziongezeke hapa hapa nchini.  Kwa upande wa elimu ya msingi tulijenga shule mpya na kuongeza madarasa pale ilipohitajika.  Kwa upande wa sekondari tukaanzisha mkakati wa kujenga shule ya sekondari kwa kila kata na kwa elimu ya juu tulihimiza wadau wengine kujenga vyuo vikuu na serikali kutoa mikopo ya elimu ya juu kwa wote.  Sisi tulionesha mfano kwa kujenga Chuo Kikuucha Dodoma, Chuo cha Nelson Mandela na kuanzisha Chuo cha Mbeya na sasa tunajenga Chuo Kikuu cha Kilimo Butiama.
Matokeo ya uamuzi huo na hatua hizo ni kuongezeka sana kwa shule za sekondari na vyuo vikuu nchini. Kwa sababu hiyo ilipofikia mwaka 2013 hali ilikuwa tofauti kabisa. Wanafunzi katika shule za sekondari Tanzania walifikia milioni 1,804,056 na vyuo vikuu 200,986. Wenzetu wa Kenya bado wanatuzidi kwa kuwa na wanafunzi wa sekondari 2,104,300 na vyuo vikuu 324,600. Lakini, tuliweza kuipita Uganda iliyokuwa na wanafunzi wa shule za sekondari 1,362,739 na wa vyuo vikuu 140,403. Leo tuko mahala ambapo tunaweza kusema   tunashindana kisawa sawa na wenzetu.
Mafanikio hayo makubwa katika sekta ya elimu hayakutokana na nguvu za Serikali peke yake.  Haya ni mafanikio yaliyotokana na mchango mkubwa wa wananchi na wadau wengine. Wananchi walijitolea nguvu zao na chochote walichokuwa nacho kujenga shule za sekondari na msingi nchini kote. Aidha, huwezi kutaja mafanikio haya bila ya kutambua mchango mkubwa wa taasisi na mashirika ya dini na sekta binafsi ambao wamejenga shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo vikuu.
Tunayo kila sababu ya kujipongeza na kujivunia matokeo haya na matunda ya kazi yetu nzuri. Wakati huo huo tunaendelea kukumbushana umuhimu wa kuendelea na kazi muhimu ya kuongeza ubora wa elimu waipatayo watoto wetu katika ngazi zote.
Suala la kuongeza ufaulu katika mitihani ya darasa la saba na kidato cha nne ni miongoni mwa malengo makuu ya Mkakati wa Matokeo Makubwa sasa. Kwa mujibu wa BRN malengo ya   ufaulu kwa kidato cha nne umetakiwa uwe asilimia 60 mwaka 2013 na asilimia 80 mwaka 2014. Kiwango cha ufaulu kwa kidato cha nne hivi sasa ni asilimia 69.7. Kwa upande wa darasa la saba, malengo yalikuwa kufikia asilimia 60 mwaka 2013 na asilimia 80 mwaka 2014 mpaka sasa tumefikia asilimia 56.9.
Kwa jumla ufaulu umekuwa unaongezeka lakini bado hatujafika pale tunapopataka.  Ufaulu wa wanafunzi ni kielelezo cha ubora wa elimu wanayopata.  Hivyo basi, tunayo kazi kubwa ya kufanya kuinua ubora wa elimu ncini.  Katika BRN kuongeza ubora wa elimu lilikuwa agenda mama na yote tunayofanya shabaha yake ni hiyo.  Tunaendelea na utekelezaji wake na sina shaka kwamba tukifanikiwa kutekeleza kwa ukamilifu elimu nchini siyo tu itamfikia kila anayeistahili bali itakuwa ya ubora wa hali ya juu.  Hakuna lisilowelezekana, kinachotakiwa ni kila mmoja wetu kutimiza wajibu wake.
Ndugu Wananchi;
Napenda kutumia fursa hii pia, kuzipongeza Halmashauri zote na mikoa yote kwa kuitikia wito wangu wa kujenga maabara katika shule zetu za sekondari ambazo hazina. Aidha, nawashukuru wazazi, walezi na wadau kwa kujitolea kuchangia nguvu kazi katika ujenzi wa maabara. Wasivunjwe moyo na wale wachache wanaojaribu kutukatisha tamaa. Kwa viongozi wa mikoa, Wilaya na Halmashauri, nakumbusha kwa mara ya mwisho kuwa ujenzi wa maabara zilizokuwa hazijakamilishwa uwe umekamilika ifikapo Juni 30, 2015.  Nimeona nirudie hili kuweka msisitizo.
Hitimisho
Ndugu Wananchi;
Hapana shaka kuwa tuko katika njia sahihi katika azma yetu ya kuleta mapinduzi katika sekta ya elimu, na kuwaandaa vijana wetu kukabiliana na changamoto za maisha za kujiletea maendeleo yao, ya jamii wanayoishi na nchi yao. Kila mmoja na atimize wajibu wake ipasavyo. Mafanikio ya kuleta mapinduzi ya elimu yanategemea mkusanyiko wa jitihada za wanafunzi, wazazi walezi, walimu, wamiliki wa shule na vyuo ikiwemo serikali.  Kila mmoja akilima mraba wake vizuri katika shamba hili kubwa, matunda yake na neema zake ni faraja kwetu. Tukifanya kinyume chake madhara yake ni hasara kwetu sote.  Hivyo basi,  kila mtu atambue  wajibu wake katika  kuhakikisha elimu inapatikana kwa watoto wetu wote na ni wa ubora ya hali ya juu.  Njia nzuri ya kutimiza wajibu wako ni kuanza na shule ya msingi na sekondari iliyoko katika eneo lako na kata yako maana hakuna  eneo wlala kata isiyo na shule hizo na hakuna Mtanzania asiyeishi katika kata.
Kila mmoja wetu na ajiulize, amechangia nini katika kuboresha shule ya eneo na kata yake? Amechangia nini katika kusimamia na kufuatilia mahudhurio na maendeleo ya kitaaluma ya mtoto aliyeko kwenye kaya yake? Elimu bora inawezekana na inaanza na wewe.  Timiza wajibu wako.
Mungu ibariki Tanzania!
Ahsanteni Sana kwa Kunisikiliza

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA