MHASIBU KCMC ASIMAMISHWA KAZI BAADA YA KUMTUMIA UJUMBE MFUPI RAIS KIKWETE, IKULU YAVUJISHA SIRI ?.


 

Moshi. Mhasibu wa Hospitali ya Rufaa KCMC, Paul Mhumba amesimamishwa kazi kwa tuhuma za kutuma ujumbe wa simu ya mkononi (sms) kwa Rais Jakaya Kikwete. 


Kuvuja kwa ujumbe huo na nambari ya simu iliyotuma, kumeibua hisia tofauti kuhusu usiri wa ofisi ya Rais katika kushughulikia malalamiko nyeti ya wananchi na kuwaweka njiapanda watoa habari za siri.


Mhumba, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Afya na Serikali Kuu (Tughe) Tawi la KCMC anadaiwa na Menejimenti ya KCMC kuwa ndiye aliyetuma ujumbe huo.


Katika barua yake ya Mei 5, yenye kumbukumbu PF.4515/22, KCMC ilidai uchunguzi umebaini kuwa Mhumba ndiye mtumaji wa ujumbe huo.


“Uongozi umepokea taarifa iliyotumwa mwishoni mwa Aprili na mwanzoni mwa Mei mwaka huu kwa njia ya ujumbe wa simu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete,” ilidai.


KCMC imedai katika barua hiyo, taarifa hiyo ya sms ilibeba ujumbe unaohusiana na matumizi mabaya ya fedha za hospitali hiyo unaofanywa na baadhi ya viongozi na Shirika la Msamaria Mwema (GSF).


Mbali na tuhuma hizo, lakini pia KCMC inadai taarifa hiyo ilimweleza Rais kuwa KCMC na GSF linalomiliki hospitali hiyo, zinajitosheleza kwa mapato, hivyo hakuna haja kwa Serikali kuendelea kuipatia ruzuku.


Pia, menejimenti imedai taarifa hiyo ilidai wafanyakazi wa KCMC wanatumikishwa kama watumwa, hivyo ni maombi yao (watumishi) Serikali ilegeze masharti ili ajira zao zichukuliwe na Serikali.


“Uchunguzi umeonyesha kuwa taarifa hiyo (kwa Rais), umeituma kwa kutumia simu ya kiganjani ambayo ulikabidhiwa kama mojawapo ya zana ya kuleta ufanisi katika majukumu yako,” imedai.


Mei 8, KCMC ilimwandikia barua Mhumba yenye kumbukumbu PF.4515/28 iliyotiwa saini na Profesa Raimos Olomi ikimjulisha kuwa amesimamishwa kazi kuanzia Mei 8 hadi Mei 14.


Katika barua hiyo, Profesa Olomi alidai menejimenti imepokea taarifa ya kutofanyika kwa kikao cha kamati ya nidhamu baada ya Mhumba kumkataa mwenyekiti kutokana na kukosa imani naye.


Pia, kikao hicho hakikufanyika baada ya Mhumba kuomba kamati hiyo iahirishwe kwa sababu mwakilishi wake hakuwapo na kikao kingine kupangwa Mei 15.


Hata hivyo, bado mhasibu huyo hajarejeshwa kazini na vikao vilikuwa vinaendelea kuhusu hatua za kinidhamu zinazostahili dhidi yake.


“Wakati hayo mambo mawili yanafanyiwa kazi, menejimenti imeamua kukusimamisha kazi. Kabla hujaondoka unatakiwa ukabidhi vitendea kazi pamoja na simu ya mkononi uliyokabidhiwa,” imedai.


Ofisa Uhusiano wa KCMC, Gabriel Chisseo alipoulizwa kuhusu sakata hilo alisema kwa nafasi yake, hawezi kulizungumzia.


Mhumba alipotafutwa wiki iliyopita, alikiri kusimamishwa kazi kwa tuhuma za kumtumia Rais ujumbe wa simu ya mkononi, ingawa alikanusha kuhusika.


“Maudhui hayo kama ni kweli yalitumwa, hayana matatizo. Nimeongea na katibu mkuu kumuuliza kama alipokea sms kutoka kwa Rais na kuwapa KCMC na namba ya mtumaji amekanusha,” alidai.


Hata hivyo, alidai yeye akiwa mwenyekiti wa Tughe, amekuwa akionekana kama adui pale anapojaribu kutetea masilahi ya watumishi, likiwamo suala la kutopandishwa daraja tangu mwaka 2007 hadi 2015.


“Ni kweli, watumishi hawajapandishwa madaraja tangu 2007. Sisi (Tughe) tumekuwa tukilipigania kwa sababu linachangia wastaafu kulipwa pensheni ndogo,” alisema.


“Mimi kama kiongozi wa wafanyakazi, niko tayari kupeleka ushahidi kwa mambo ambayo Tughe tumekuwa tukipambana nayo, ikiwamo mahali zilipo fedha za mashine ya CT-Scan,” alisema Mhumba.


Tawi la Tughe KCMC, limemwandikia barua katibu mkuu wa Tughe, ikiomba Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama aingilie kati suala hilo ili haki itendeke.


Gama alipoulizwa kuhusu suala hilo, alikiri kupigiwa simu na Mhumba akimueleza lakini alimshauri aziandikie mamlaka husika.


Gama alisema akiwa mwakilishi wa Rais mkoani Kilimanjaro, atachunguza nini kimetokea baada ya kupata malalamiko rasmi kutoka kwa Mhumba au Tughe 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI